Habari za Punde

Milioni 16 Zakusanywa Kupitia Mpango Maalum Kulipia Benki.

Na.Said Abdurahaman Pemba.

ZAIDI  ya Tsh, milioni 16 zimekusanywa  kwa muda wa mwezi mmoja tokea Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar,  kuanzisha kwa mpango maalum wa kulipia Benki rasilimali mchanga.


Akitoa taarifa mbele ya Waziri wa Kilimo, Maliasili,Mifugo na Uvuvi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar,Mhe.Hamad Rashid Mohamed, Ofisa mipango kutoka Idara ya Misitu Pemba, Mussa Said Bakar, alisema kuwa fedha
hizo zilikusanywa tokea mpango huo uanzishwe na fedha hizo zinatumwa kwa akaunti ya Unguja.



Alifahamisha kuanzia mwezi huu wa Julay 2017,sasa malipo hayo yatalipiwa  katika akaunti ya Pemba na wala sio tena ilivyokuwa hapo awali.


Mussa,  alisema  changamoto kubwa inayowakabili kwa sasa ni kwa upande wa Mkoa wa Kusini Pemba, kupata sehemu ya kuchimbia mchangakwani eneo ambalo walikuwa wakilitumia huko Ging’ingi Chambani kuwa
na mgogoro.



Aliitaja  changamoto nyengine ni deni ambalo wanadaiwa na wafanyakazi waliopo katika eneo la shimo na hawajalipwa tokea mpango huo uanze.


“Mheshimiwa tokea tuanze mpango huu hawa wafanyakazi waliopo hapa hawajalipwa na wanatudai kiasi cha Tshilingi milioni 3,900,015,”alisema, Afisa huyo.


Kwa upande wake , Waziri Hamad aliutaka uongozi wa Wizara hiyo kufuatilia fedha zote za makusanyo na kuwataka kila sehemu kuhakikisha wanapata haki zao bila matatizo.


Hata hivyo  aliitaka Wizara ya Kilimo kuweka hadharani bei ya mchanga ili kila mtu aelewe juu ya kulipa mapato yake ili kutowapa mwanya walanguzi kuuza mchanga kwa bei ya juu.


Nae, Ali Said Ali (kiro) dereva wa gari ya kubebea Mchanga, aliiomba Serikali kutengenezewa barabara inayoingia katika sehemu za kuchimbia mchanga (shimoni) kutokana na njia wanayotumia haiko sahihi.


“Mfumo huu wa kwenda kulipa benki kwa sisi  wengine unatuwia vigumu kwani inabidi tuondoke huku Konde twende Wete kwa ajili ya kufanya malipo na pengine siku mzima unapata gari moja tu,’alisema Kiro.


Hivyo waliomba Wizara kuandaa mpango madhubuti wa malipo ambao hautotowa usumbufu kwa wananchi wanaohitajia kulipa .

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.