STATE
HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF
THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 04.07.2017
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amelitaka Shirika la Umeme Zanzibar (ZECO)
kufanya biashara isiyo na hasara na badala yake kuhakikisha linapata faida ili
kuweza kuendesha vyema Shirika hilo.
Dk. Shein aliyasema hayo
Ikulu mjini Zanzibar wakati alipokutana na uongozi wa Wizara ya Ardhi, Maji,
Nishati na Mazingira pamoja na Bodi ya Wakurugenzi ya Shirika la Umeme Zanzibar
(ZECO) pamoja na uongozi wake.
Katika maelezo yake, Dk.
Shein alieleza kuwa umefika wakati kwa Shirika hilo kuhakikisha linafanya
biashara zake kwa lengo la kuleta tija kwani iwapo Shirika hilo litafanya
juhudi za makusudi hilo linawezekana.
Aidha, Dk. Shein
aliongeza kuwa lazima Shirika hilo la (ZECO) lihakikishe linaendesha vyema
huduma zake kwa wananchi na wale wote wanaodaiwa na Shirika hilo ni vyema
wakalipa madeni yao na wakishindwa kulipa hatua za makusudi zichukuliwe na
Shirika hilo ikiwemo kuwakatia umeme kwa wale wadaiwa sugu.
Alisisitiza kuwa iwapo
watafanya kazi vizuri mafanikio makubwa watayapata huku akiwasisitiza kuwa ni
lazima deni linalodaiwa na (TANESCO) lilipwe ambapo Serikali kwa upande wake
itaendeleza utaratibu ulioweka katika kuhakikisha kila mwezi deni hilo
linalipwa.
Sambamba na hayo Dk.
Shein alieleza haja ya kushughulikiwa kwa wafanyakazi wakorofi ambao wamo ndani
ya Shirika hilo ambao husababisha ukosekanaji wa mapato huku akitumia fursa
hiyo kueleza matumaini yake makubwa aliyonayo kwa Bodi ya Wakurugenzi ya (ZECO).
Dk. Shein aliongeza kuwa
ni vyema kwa Shirika hilo la Umeme Zanzibar (ZECO) likajitayarisha kufanyakazi
katika mazingira ya ushindani kibiashara kutokana na mpango wa Serikali wa
kuishirikisha sekta binafsi katika miradi mbali mbali ya maendeleo ambapo wawekezaji
wengi wameonesha nia ya kutaka kuwekeza kwenye sekta hiyo.
Nae Makamo wa Pili wa
Rais Balozi Seif Ali Idd, alieleza haja kwa Shirika hilo kuhakikisha linakusanya
vyema mapato yatokanayo na huduma hiyo hasa katika hoteli kubwa kubwa kwani
hoteli ni nyingi lakini mapato yanayotokana na hoteli hizo ni kidogo.
Katibu Mkuu Kiongozi na
Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee alilitaka ZECO kuangalia
vyema umadhubuti wa vifaa vya umeme vinavyotolewa na Shirika hilo
ikilinganishwa na bei zake huku akieleza haja ya kuondosha ubinafsi kwa uongozi
na wafanyakazi wake, ambao hupelekea kufanya kazi kwa mazoea na hatimae kulitia
hasara Shirika hilo.
Nao uongozi wa (ZECO)
ulieleza hatua inazozichukua katika kuhakikisha inakusanya mapato yake sambamba
na hatua za kusambaza huduma ya umeme kwa wananchi Unguja na Pemba.
Aidha, Mkurugenzi Mkuu
wa Shirika la (ZECO) Hassan Ali Mbarouk, alieleza hatua zilizofikiwa kati ya Shirika
hilo na Kampuni zitakazouza umeme kwa kufungua vituo katika maeneo mbali mbali
Unguja na Pemba ili kuwarahisishia wananchi kupata huduma hiyo kwa ufanisi tofauti
na ilivyo hivi sasa.
Mkurugenzi huyo alitumia
fursa hiyo kueleza mafanikio na changamoto zilizopo katika Shirika hilo ikiwa
ni pamoja na zile za matumizi ya umeme na kueleza haja ya kuendeleza utaratibu
wa kuwepo kwa umeme mbadala hasa umeme wa gesi.
Nao uongozi wa Wizara
ulieleza hatua za makusudi zinazoedelea kuchukuliwa katika kuhakikisha Shirika
hilo linapata mafanikio sambamba na kuimarisha mahusiano na Bodi hiyo ya (ZECO).
Mapema Mwenyekiti wa
Bodi ya Wakurugenzi katika Shirika hilo la (ZECO) Shafi Mussa Haji alieleza
majukumu, utendaji wa kazi za Bodi hiyo, mafanikio pamoja na changamoto
zilizopo.
Alieleza kuwa katika
kipindi cha mwaka mmoja wa Bodi, Shirika limeweza kusambaza huduma ya umeme
katika jumla ya vijiji 47 kwa Unguja na Pemba pamoja na kufungua vituo vya
Gamba na Makunduchi vinavyotoa huduma za kiufundi kwa wateja wa maeneo ya
karibu na hivi karibuni Shirika linatarajia kufungua vituo kama hivyo eneo la
Dunga, Wilaya ya Kati.
Wakati huo huo, Dk. Shein
ameeleza kuwa mabadiliko yaliyofanywa na Serikali ndani ya Shirika la Biashara
la Taifa la Zanzibar (ZSTC) ikiwemo kutungwa kwa Sheria yamelipelekea Shirika
hilo kupata mafanikio makubwa ikiwa ni pamoja na kuimarika kwa biashara ya
karafuu.
Dk. Shein aliyasema hayo
Ikulu mjini Zanzibar alipokutana na uongozi wa Wizara ya Biashara, Viwanda na
Masoko, Bodi ya Wakurugenzi ya Shirika la Biashara la Taifa la Zanzibar (ZSTC)
pamoja na uongozi wake.
Katika maelezo yake, Dk.
Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Shirika la (ZSTC), kwa mafanikio
makubwa iliyoyapata tokea kuanzishwa kwa mabadiliko makubwa ikiwa ni pamoja na kutunga
Sheria ya Shirika la Biashara la Taifa Zanzibar (ZSTC) Namba 11 ya mwaka 2011
na ile Sheria ya Maendeleo ya karafuu Namba 2 ya mwaka 2014.
Dk. Shein alieleza kuwa
azma ya Serikali ya kurekebisha vituo vya kununua karafuu vya ZSTC sambamba na
kuimarisha miundombinu ya barabara kwa maeneo yanayozalisha karafuu kwa wingi
ni miongoni mwa hatua muhimu za kuliimarisha zao hilo na kukuza bishara ya
karafuu.
Alieleza kuwepo Sheria
hizo ndani ya Shirika hilo zitalisaidia katika kufikia lengo la kuimarika kwa biashara ya karafuu
pamoja na biashara nyenginezo ambazo zina maslahi na wananchi huku wananchi na
wauzaji wa karafuu nao wakiendelea kufaidika.
Pia, Dk. Shein aliutaka
uongozi wa (ZSTC) kutambua kuwa maghala yote ya Shirika hilo yaliopo Unguja na
Pemba ni mali yao hivyo ni lazima wayasimamie vyema na kuyatunza.
Nae Makamo wa Pili wa
Rais, Balozi Seif Ali Idd, alitoa pongezi kwa Shirika hilo kwan kuendelea
kufanya vizuri na kueleza haja ya kuendelea kufanya vizuri kwani ni shirika la
zamani na lina historia yake.
Waziri wa Wizara ya
Biashara, Viwanda na Masoko Balozi Amina Salum Ali alisema kuwa Shirika hilo ni
miongoni mwa mashirika yaliopata mafanikio makubwa nchini Tanzania ambalo
halijawahi kupata misuko suko hatua ambayo imetokana na miongozo mizuri ya Rais
Dk. Shein.
Balozi Amina alieleza
kuwa masoko ya bidhaa zinazozalishwa na ZSTC yapo hata nje ya nchi na
kusisitiza haja ya kuongeza uzalishaji wa bidhaa kwa kuwashirikisha wakulima
pamoja na vijana kulima mazao ya biashara yakiwemo viungo huku akieleza
uwezekano wa kuzalisha asali, mbazi na dengu badala ya karafuu peke yake.
Aidha uongozi wa ZSTC
ulieleza changamoto zilizopo sambamba na mafanikio yaliopatikana huku ukieleza
hatua zilizopatikana za mafanikio kwa kupata mununuzi wa bidhaa za kwianda cha
makonyo kutoka nchini China ambaye ameahidi kunua bidhaa hizo tani 40 kila
mwezi.
Katibu Mkuu Kiongozi na
Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee alieleza haja ya
kukiangalia kwa mtazamo wa uzalishaji wenye tija kiwanda cha makonyo kilichopo
Wawi kwa kukifanyia ukarabati ama kukijenga upya ikiwa ni pamoja na kuweka
mashine za kisasa kwa lengo la kuweza kuzalisha bidhaa kwa wingi.
Mapema Mwenyekiti wa
Bodi ya Wakurugenzi ya Shirika la Biashara la Taifa la Zanzibar (ZSTC) Kassim
Maalim Suleiman, alisifu mashirikiano makubwa yaliopo kati ya Bodi na uongozi
wa Wizara huku akieleza miongoni mwa mafanikio yaliopatikana ikiwa ni pamoja na
kuwa na hakiba ya TZS Bilioni 5.2 kuanzia Julai mwaka 2016 hadi Machi 2017.
Mwenyekiti huyo alisema
kwa mwaka huo wa 2016 hadi 2017 Shirika limeuza karafuu tani 2156 zenye thamani
ya TZS Bilioni 36.6 huku akieleza haja ya kutotegemea zao loa karafuu peke na
badala tyake kutafuta mazao mengine ambayo yatalipunguzia mzigo zao hilo.
Rajab Mkasaba, Ikulu
Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment