Habari za Punde

Mjumbe wa Kamati Kuu CCM Balozi Seif Amewataka Viongozi Kuwakemea Wanachama Wanaojikita Katika Makundi Ndani ya Chama.

Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi Balozi Seif Ali Iddi kuzungumza na Viongozi wa CCM  wa Mikoa Miwili ya Pemba ngazi ya Wenyeviti, Makatibu na Wajumbe wa NEC hapo katika Ukumbi wa Mikutano wa Makonyo Wawi Chake Chake Pemba.
Kulia ya Balozi Seif ni Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kaskazini Pemba Mzee Mberwa Hamad Mberwa na Kushoto ya Balozi ni Mjumbe wa Kamati ya Siasa na Mkoa Kaskazini Pemba Mh. Omar Khamis Othman.
Wajumbe wa Kamati za Siasa za CCM Mikoa Miwili ya Pemba wakifuatilia hotu ba ya Mjumbe wa Kamati Kuu ya Taifa ya CCM  Balozi Seif hayupo pichani alipokutana nao kubadilishana mawazo.
Baadhi ya Viongozi wa CCM Pemba wakiendelea na Mkutano wao wa kawaida wa kubadilishana mawazo uliopata baraka ya kuhudhuriwa na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi Balozi Seif Ali Iddi.

Picha na – OMPR – ZNZ.

Na. Othman Khamis OMPR.
Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi Balozi Seif Ali Iddi amewataka Viongozi na Wanachama wa CCM kuwakemea Wanachama waliojikita  katika kuendeleza makundi ndani ya chama wakijiandaa kwa ajili ya kujenga safu ya Uongozi kwenye uchaguzi Mkuu ujao.

Alisema makundi yanayojipanga wakati huu ambapo  kwa sasa Taifa linatarajia Wananchi waongeze nguvu zao katika uzalishaji kwenye  miradi ya maendeleo kamwe hayatamsaidia Kiongozi atakayechaguliwa wakati ukifika wa Uchaguzi Mkuu kuongoza Dola.

Balozi Seif Ali Iddi alitoa wito hilo wakati akizungumza na Viongozi wa Chama cha Mapinduzi wa Mikoa Miwili ya Pemba ngazi ya Wenyeviti, Makatibu na Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM hapo katika Ukumbi wa Mikutano wa Makonyo Wawi Chake Chake Pemba.

Alionya kwamba Chama katika Uongozi wa Ngazi ya Juu kimejipanga kuwaondoa kwenye mchakato wa kuwania Uongozi wanachama wote watakaoendeleza tabia hiyo mbaya inayozalisha Viongozi Matapeli na wasio na uwezo wa kuongoza.

Balozi Seif alisema wakati umefika kwa Viongozi  kuacha tabia ya kupakana matope na badala yake wawaachie Wanachama wenyewe kuamua  kumpendekeza na hatimae kumchagua Mwanachama watakayehisi ana uwezo na uzalendo wa kuwatumikia.

Alitahadharisha kwamba makundi yanayodhoofisha nguvu za Chama yanapaswa kuelewa kwamba yanahatarisha uhai wa Chama  sambamba na kutishia  Amani ya Taifa baada ya kukosa utulivu utakaosababishwa na sintofahamu baina ya makundi hayo.

Balozi Seif aliwapongeza Wanachama wa Chama cha Mapinduzi kwa hatua nzuri waliyofikia katika uendeshaji wa Uchaguzi wa ndani kuanzia ngazi ya shinda na kufikia Tawi na kuwataka kutumia busara, hekima na utulivu katika chaguzi za ngazi ngenine za Chama hicho.

Aliwashauri wanachama hao kuzingatia kwa makini Viongozi watakaowateuwa wanawavusha vyema na kuepuka kasoro nyingi zilizojitokeza za kukaribisha baadhi ya Wapindani kujipenyeza kwenye Mikutano na Kamati za Chama hicho.

Balozi Seif Seif alionyesha masikitiko yake kutokana na  tabia zilizowahi kujitokeza zilizoashiria mmong’onyoko wa ukosefu wa siri za Vikao vya Chama hicho ambazo zilitolewa na wapinzani hao.

Akizungumzia kuhusu suala la Zao la Karafuu lilioanza kupea wakati huu Balozi Seif Ali Iddi ambae pia ni Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliwaagiza Viongozi wa Serikali Mikoa na Wilaya kwa kushirikiana na Vikosi vya Ulinzi kutaifisha mali na vyombo vyote vitakavyokamatwa kuhusika na Magendo ya zao la Karafuu.

Alisema zipo dalili za wazi za hujuma dhidi ya zao la Karafuu zinazoendelea kufanywa na baadhi ya Watu kwa kulisafirisha zao hilo na kuliuza Nchi jirani wakati Serikali Kuu tayari imeshaongeza Bei mara dufu ya zao hilo na kukidhi soko lililopo.

Mapema Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Mkoa Kaskazini Pemba ambae pia ni Kaimu Mwenyekiti wa CCM Mkoa Kusini Pemba Mzee Mberwa Hamad Mberwa alisema Wanachama na Wananchi Mikoani na Wilayani wanaridhika na kasi ya Serikali katika utekelezaji wa Ilani ya CCM YA Mwaka 2015 – 2020.

Mzee Mberwa alisema kasi hiyo imeongeza ari kwa wanachama hao pamoja na kutoa matumaini waliyoyatarajia wakati wa kuwamua kukipadhamana chama hicho katika kuongoza Dola Zanzibar na Tanzania kwa ujumla.

Mwenyekiti huyo wa CCM Mkoa Kaskazini Pemba alimuhakikishia Mjumbe huyo wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chanma cha Mapinduzi kwamba  Wana CCM  bado wanaimani na chama chao na daima wataendelea kukiunga mkono katika adha ya chama hicho ya kuongoza Dola kila baada ya Uchaguzi Mkuu.

Balozi Seif amemaliza ziara yake ya siku mbili Kisiwani Pemba kuangalia harakati za Maendeleo sambamba na kuimarisha uhai wa Chama cha Mapinduzi akiwa ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.