Habari za Punde

TUME YATEUA MBUNGE NA MADIWANI WATATU (3) WANAWAKE WA VITI MAALUM.


NEC
7/9/2017. Dar es salaam.
Tume ya Taifa ya Uchaguzi imemteua Ndugu Rehema Juma Migilla kuwa Mbunge wa Viti Maalum katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chama Cha Wananchi (CUF) ,kujaza nafasi iliyoachwa wazi na Ndugu Hindu Hamisi Mwenda aliyefariki  dunia Septemba 1, 2017.

Akizungumzia uteuzi huo, Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi Bw. Kailima Ramadhani amesema kuwa Tume imemteua Ndugu Rehema Juma Migilla mara baada ya kupokea taarifa ya kuwepo kwa nafasi wazi ya Mbunge wa Viti Maalum kutoka Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Amesema kwa mujibu wa kifungu cha 37 (3) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, Sura ya 343 Mhe. Spika aliitaarifu Tume ya Taifa ya Uchaguzi juu kuwepo kwa nafasi wazi ya mbunge wa Viti Maalum kupitia Chama cha Wananchi CUF baada ya aliyeteuliwa kuwa Mbunge wa Viti Malum kupitia chama cha CUF Ndugu Hindu Hamis Mwenda kufariki dunia.

Katika hatua nyingine Mkurugenzi  huyo amesema kuwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwa mujibu wa kifungu cha 86 A (8) cha Sheria ya Uchaguzi ya Serikali za Mitaa imewateua Madiwani Wanawake wa Viti Maalum watatu (3) kujaza nafasi wazi za madiwani katika Halmashauri tatu za Tanzania Bara.

Madiwani walioteuliwa ni Ndugu Jane I. Chungwa kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Itigi kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndugu Rosana S. Mwinyi kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Bahi kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Ndugu Pili M.Mfaume kupitia Chama Cha Wananchi CUF kutoka Halmashauri ya Temeke.

Amesema uteuzi huo umefanyika baada ya Tume kupokea taarifa kutoka kwa Waziri mwenye dhamana ya Serikali za Mitaa ambaye kwa kuzingatia masharti ya kifungu cha 13 (1) cha Sheria ya Uchaguzi ya Serikali za Mitaa, Sura ya 292 aliitarifu Tume ya Taifa ya Uchaguzi kuhusu uwepo wa nafasi wazi za madiwani.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.