Habari za Punde

Watuhumiwa madawa ya kulevya wapandishwa kizimbani Chakechake


Na Salmin Juma, Pemba

MAHAKAMA ya Mkoa Chakechake, imemsweka rumande mwanamke mwenye mtoto mchanga wa siku 20, akituhumiwa kukutwa na kete 3,621 zinazodhaniwa kuwa ni dawa za kulevya, pamoja na mwenzake mmoja.

Mama huyo Zuhura Ahmed Ali (29) mkaazi wa Jadida na mwenzake Seif Ali Seif (30) mkaazi wa Mtemani wote wilaya ya Wete, walipandishwa mahakamani jana, majira ya saa 7:40 mbele ya hakimu Hussein Makame Hussein wa mahakama hiyo.

Mara baada ya watuhumiwa hao kupanda juu ya kizimba cha mahakama, Mwendesha Mashitaka kutoka Afisi ya Mkurugenzi wa mashitaka Ramadhan Suleiman Ramadhan, alidai kuwa wote kwa pamoja, Septemba 9, mwaka huu walipatikana na dawa hizo za kulevya.

Alidai kuwa, walipatikana na kete hizo 3,621 kituo cha Polisi Mkoani Pemba, majira ya saa 6: 45 mchana mara bada ya kupekuwaliwa, wakijua kuwa hilo ni kosa.

Mwendesha mashitaka huyo, aliiambia mahakama hiyo kuwa, kufanya hivyo ni kosa, kinyume na kifungu cha 15 (1) (a) sheria no 9 ya mwaka 2009, kama ilivyofanyiwa marekebisho na kifungu cha 11 (a) cha sheria no 12 ya mwaka 2011 sheria ya Zanzibar.

Mara baada ya kusomewa mashitaka yao, watuhumiwa hao kwa pamoja, walikana kuhusika na kosa hilo na kuiomba mahakama hiyo, iwapatie dhamana ombi ambalo lilipingwa.

Mtuhumiwa Zuhura Ahemed Ali, aliiomba mahakama hiyo kumpa dhamana, kutokana na kuwa ananyonyesha mtoto aliejifungua siku 20 zilizopita.

“Muheshimiwa hakimu, naomba unipe dhamana, maana mimi kwanza hali yangu sio nzuri, lakini kisha nna mtoto mchanga nanyonyesha na tokea juzi ninae Polisi, na kuna mbu”,aliomba mtuhumiwa huyo.

Kwa upande wake mtuhumiwa Seif Ali Seif, aliomba dhamana hasa kutokana na kwamba, yeye hahusiki na tukio hilo, na siku tatu kamili, alikuwa kituo cha Polisi na hajapata mlo.

“Muheshimwa, kwa vile mimi sihusiki na tukio hili naomba dhamana, maana kwanza nna njaa na hali yangu sio mzuri”,aliomba dhamana hiyo, maombi ambayo yamekataliwa mahakamani.

Baada ya maombi hayo ya dhamana kukataliwa na Hakimu Hussein Makame wa mahakama hiyo ya Mkoa Chakechake, ndipo alipowaamuru watuhumiwa hao, kwenda rumande hadi Septemba 20 mwaka huu.

Aidha Hakimu huyo, alisema kwa vile tayari upelelezi umeshakamilika, siku hiyo mashahidi wote waitwe na barua za wito zitolewe kwao.

Hata hivyo Hakimu huyo alisema, siku hiyo ndio Mahakama itaangalia taratibu na uwezekano wa kuwatajia masharti yao ya dhamana juu ya shauri linalowakabili.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.