Habari za Punde

Kiongozi wa Mbio za Mwenge: Awataka Wananchi Kisiwani Pemba Kufanya Kazi Kuacha Soga

Na.Haji Nassor - Pemba.
Wananchi wa wilaya ya Chakechake kisiwani Pemba, wametakiwa kufanya shughuli zao mbali mbali za kimaendeleo ikiwemo kilimo, ili kujihakikishia maisha bora, badala ya kukaa barazani na kupiga soga.

Kauli hiyo imetolewa na kiongozi wa mbio za mwenge wa uhuru, Amour Ahmada Amour kabla ya kuweka jiwe la msingi la nyumba bora kijiji cha Matuleni, kwenye mbizo za mwenge zilizoanza wilayani humo, ukitokea wilaya ya Mkoani.

Alisema kila mwenye uwezo wa kufanya kazi, basi ahakikishe hilo analifanya kwa nafasi yake, badala kukaa bila ya kujishughulisha, kwani hawatowezi kufikia maendeleo.

Alisema kazi ndio msingi mkuu wa mwanadamu kuwepo ulimwenguni, hivyo ikiwa wataamua kukaa barazani na kuachana na hilo, wasitarajie mabadiliko kati yao.

“Mimi nimefuatana na mwenge wetu huu wa uhuru, kazi kubwa ni kuwakumbusha na kuwaamsha kuwa, kila mmoja afanye kazi, maana matokeo yake ni manufaa ya kweli”,alieleza.

Aidha kiongozi huyo wa mbizo za mwenge, wamewataka wanafunzi kote nchini, kuweka pembeni anasa na michezo isiokuwa na tija kwao, na badala yake washughulike masomo yao.

Alisema wazazi na walezi wao, wamekuwa wakihangaika huku na kule kuhakikisha wanapata mlo, hivyo kazi iliopo mbele yao ni kusoma na sio vyenginevyo.

Wakati huo huo kiongozi huyo wa mbio za mwenge na ujumbe wake, mara baada ya kukifungua kituo cha afya Pujini na kutoa matone ya vitamin ‘A’ kwa watoto waliochini ya umri wa mwaka, alikataa kugawa vyandarua kwa wazee na watoto hao.

Mara baada ya tukio hilo la kutoa matone na kukitembelea kituo hicho cha afya,wakati ukafika wa kugawa vyandarua ndipo, alipomba orodha ya wanaostahiki na kukosekana.

“Nimemaliza kutoa matone, sasa naomba orodha (majina) ya wananchi hao 10, wanaopaswa kugawawi vyandarua, jamani orodha iko wapi, nahitaji hayo majina ili nipate kugawa, au vipi, mbona sipaji jibu”,alihojia Kiongozi huyo wa mbio za mwenge.

Wakati hayo yakijiri Afisa wa afya wilaya ya Chakechake, Kombo Omar Abdalla, alikuwa tayari na vyandarua 10 mkononi mwake, huku akimshawishi kiongozi huyo wa mbio za mwenge kuvigawa, ingawa ilishindikana.

“Muheshimiwa vyandarua ndio hivi unavyopaswa uvigawe kwa wananchi hawa wakiwemo na wazee, lakini orodha hatuna isipokuwa walengwa wenyewe ndio hawa, au unajua majina yapo, lakini, sasa vipi, hivi vyandarua”,aliomba bila ya mafanikio.

Baada ya dakika tatu kupitia bila ya kitolewa orodha, kiongozi huyo wa mbio za mwenge pamoja na wakimbiza mwenge wake na mkuu wa wilaya ya Chakechake, waliondoka kituoni hapo, na kuendelea na ratiba yao kwenye wilaya hiyo.

Afisa wa Afya wilaya ya Chakechake, baadae aliwaomba radhi wazee hao waliopaswa kukabidhiwa vyandarua hivyo, kwa hilo lililojitokeza na kuahidi kukabidhiwa kwenye mkesha wa mwenge, uwanja wa Gombani.

Ujenzi wa kutuo hicho cha afya daraja la pili, ulianza mapema Feubuari 11,  mwaka jana kwa ushirikiano wa wananchi, serikali na wafadhili IDC Foundation kutoka Itali, kwa thamani ya zaidi ya shilingi milioni 138.

Kati ya fedha hizo shilingi milioni 7, zimetolewa na Serikali, shilingi milioni 4 wananchi na wafadhili husika wametoa shilingi milioni 127, 237,520 ambapo kituo hicho, kinatarajiwa kuwahudumia wananchi 9,843 kutoka shehia za Pujini na vijiji jirani.

Awali Mkuu wa wilaya ya Mkoani Hemed Suleiman Abdulla, alimkabidhi  mwenge huo Mkuu wa wilaya mwenzake wa Chakechake Rashid Hadid Rashid, kwa ajili ya kuutembeza wilayani mwake.


Mbio za mwenge wa uhuru mwaka huu 2017, zilizinduliwa katika viwanja vya Kumbu kumbu mjini Mpanda mkoani Katavi, April 2, hivyo baada ya kukimbizwa kwenye mikoa 31,  na halmashauri 195, utahitimishwa mbizo zake kwa kuzimwa Mkoa wa mjini Magharibi Unguja hapo Oktoba 14 mwaka huu, ambapo ujumbe wa mwaka huu’ 

SHIRIKI KUKUZA UCHUMI WA VIWANDA KWA MAENDELEO YA NCHI YETU'

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.