Habari za Punde

Sururu: ‘Jitengeni na Viashiria vya Migogoro na Vurugu’

Na.Haji Nassor - Pemba.
WANANCHI wa wilaya ya Micheweni kisiwani Pemba, wameshauriwa kujitenga mbali na viashiria vinavyoweza kusababisha migogoro na kisha vurugu, kwani gharama ya kuirejesha amani iliotoweka, ni kubwa kuliko urahisi wa kuichafua.
Ushauri huo umetolewa na Afisa Mdhamini wa Wizara ya Elimu na Mfunzo ya Amali kisiwani humo, mwalimu Salim Kitwana Sururu, alipokuwa akifungua mkutano wa siku moja, wa kujengewa uwezo mpana wa kutatua na kukinga migogoro, uliotayarishwa na Jumuia ya Zanzibar Youth Forum na kufanyika skuli ya sekondari Micheweni.
Alisema, ni jukumu la kila mmoja kwa nafasi yake na mahala anapofanyia kazi, kuhakikisha anajikinga na viashiria vya aina mbali mbali, ambavyo vinaweza kusababisha migogoro na hatimae vurugu, vinavyoweza kupelekea hata vifo.
Alisema, kujenga utamduni wa kusameheana, kuvumiliana, kuoneana huruma na kuthamini utu wa mtu, ni miogoni mwa njia sahihi za kuzuia migogoro na kisha vurugu, ndani ya jamii.
Hata hivyo, alisema lazima waelewa kuwa, viashiria hivyo vinaweza kuanzia ngazi ya familia, jamii, shehia, majimbo, wilaya, mkoa na hata taifa na hatimae, kusababisha kupotea kwa amani na utulivu.
“Jamii lazima tujenge utamaduni wa kuheshimiana na kuvumiliana kwa dhati ya moyo, ili kuhakikisha hatusababishi migogoro yanayoweza kupelekea vurugu hapo baadae”, alifafanua.
Katika hatua nyengine, Afisa Mdhamini huyo, alisema mradi wa kuwajengea uwezo jamii, kwenye wilaya nne za Micheweni, Magharibi A, Kaskazini A na wilaya ya Mjini Unguja, itasaidia kupunguza migogoro na vurugu, kuanzia ngazi ya familia hadi taifa.
Mapema Mratibu wa mradi wa kukuza uwelewa juu ya kuishi kwa amani, maelewano, na ututuzi wa migogoro katika jamii, kutoka Jumuia ya Zanzibar Youth Forum, Almas Mohamed Ali, alisema ujio wa mradi huo, utakapomalizika utasaidia jamii kupata uwelewa, ili wajikinge na migogoro na vurugu.
Alisema katika mradi huo, Zanzibar Youth Forum imechagua wilaya nne, ili kutekeleza mradi huo, kwa kuwapa mafunzo waalimu wa skuli za sekondari, waalimu wa madrassa, wanajumuia za kiraia, vijana na hata watendaji serikali, kwa vile maeneo yote hayo, hutokea migogoro na kisha vuruga.
Akiwasilisha mada ya utatuzi na migogoro na viashiria vyake, muwezeshaji Hassan Jani Massoud, alisema migogoro inaweza kusabishwa na mambo kadhaa, ikiwa ni pamoja na kukoseshwa huduma, kutengwa, kujenga dhana ya kukosa haki pamoja na kunyimwa uhuru.
“Wakati mwengine vurugu na migogoro husababishwa na kutokuwepo kwa taarifa endelevu, baina ya pande moja na nyengine, jambo ambalo ndio lililotawala katika maeneo kadhaa”,alisema.
Baadhi ya washiriki wa mkutano huo, walisema migogoro hijitokeza pindi haki isipotekelezwa kwa upande mmoja, na hatimae kujitokeza vurugu, inayosababishwa na migogoro iliodumua kwa muda mrefu.
Mwalimu wa madrassa Ahmad Hassan Bakar, alisema jambo la kwanza katika kuzuia migogoro na hatimae vurugu, ni kuhakikisha kwanza haki inatekelezwa kwa mwenye haki, ili kumuweka akiwa na amani.
Nae Sharif Ahmad Mwinyi alisema, waalimu wa skuli, madrassa na viongozi wa jumuia za kirai, ndio watu sahihi wanaoweza kuwaelimisha jamii, juu ya kujitenga na viashiria vinavyoweza kusababisha migogoro na kisha vurugu.

Jumuia ya Zanzibar Youth Forum ambayo imaeanzishwa mwaka  2001, tayari imeshawaokoa vijana kadhaa na utumiaji wa dawa za kulevya, kuwajengea uwezo katika kuingia kwenye safu ya uongozi, wakiwemo wanawake na wanaume. 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.