Habari za Punde

Wadau: Toeni ushahidi msiogope changamoto mahakamani


NA HAJI NASSOR, PEMBA

JAMII nchini, imetakiwa kufanya kila mbinu, ili kuhakikisha inafika mahakamani kutoa ushahidi, hasa kwenye mashauri ya udhalilishaji, na kutovunjika moyo na changamoto zilizopo mahakamani.

Ushauri huo umetolewa na wadau wa masuala ya kupinga udhalilishaji wa kijinsia kisiwani Pemba, kwa nyakati tofauti walipokuwa wakizungumza na waandishi wa habari, juu ya sababu zinazowafanya kutopenda kutoa ushahidi mahakamani.

Wadau hao walisema iwapo jamii, watachoka kwenda mahakamani kwa sababu mbali mbali zilizopo mahakamani, inaweza kuwarahisishia na kuwapa mwanya wanaofanya matendo hayo, ikiwemo ubakaji na ulawiti.

Mratibu wa wanawake na watoto shehia ya Mchanga mdogo, Siti Khatib Ali, alisema lazima jamii iungane kisawa sawa kama ilivyokwenye mambo mengine, na kufika mahakamani kutoa ushahidi.

Alisema wanaotenda matendo kama ya ubakaji wamekuwa wakifuatilia watu iwapo wanafika mahakamani kutoa ushahidi, na kama wanachoka, na wao hupata nguvu ya kuyaendeleza matendo hayo.

“Lazima jamii ione kuwa, suala la kutoa ushahidi mahakamani ni moja ya haki ya msingi katika kutokomeza jinai, na kama wakikaa majumbani kwa kukosa nauli,na udhalilishaji utanoga”,alifafanua.

Sheha wa shehia ya Kiungoni wilaya ya Wete Omar Khamis Othman, aliitaka jamii ndani ya shehia yake, kuhakikisha wanajipanga hata kwa kusaidiana na nauli, ili kufika mahakamani kutoa ushahidi.

“Ushahidi mahakamani ndio kigezo cha mtuhumiwa kutiwa hatiani, hivyo jamii ikiona ni shida, wajuwe na udhalilishaji nao unanawirika”,alifafanua.

Mwanasheria dhamana wa Ofisi ya Mkurugenzi wa mashitaka Pemba, Ali Rajab Ali alisema, hakuna mashitaka ambayo mtu atatiwa hatiani, bila ya kuwepo kwa mashahidi.

Alisema waendesha mashitaka, Polisi na hata mahakimu ni wageni wa makosa yote yanayotokea, hivyo ili wayafahamu ni lazima mashahidi kufika mahakamani, kuwaeleza mwanzo hadi mwisho wa tukio.

“Sisi waendesha mashitaka, hatufahamu lolote iwapo kuna kosa limefanyika huko vijijini, sasa kama wakija watu kutoa ushahidi au kupinga juu ya tendo fulani, sasa hapo ndio ukweli hupatikana”,alieleza.

Afisa miradi kutoka TAMWA, Asha Abdi Makame alisema, wapo wananchi wamekuwa wasugu kutoa ushahidi, kisha kusingizia vyombo vya sheria, kuchukua rushwa.

“Ijapokuwa harufu ya rushwa hutajwa kwa mahakimu, waendesha mashitaka na DPP, lakini hata hivi kukataa kutoa ushahidi ni hatua ya kuziua kesi za udhalilishaji”,alifafanua.

Katika hatua nyengine Afisa huyo, alisema TAMWA katika kuunga mkono juhudi za kupambana na udhalilishaji ndani ya jamii, wamekuwa na mradi endelevu wa GEWE.

Alifafanua kuwa, ingawa kwa awamu hii ya Mradi huo wa kuwawezesha wanawake na kupinga udhalilishaji, GEWE, unalenga zaidi kuwawezesha waandishi wa habari kuibua habari zilizojificha.

“Wapo waandishi wameshapewa taaluma na sasa wako kwenye shehia mbali mbali za Unguja na Pemba, wakifanya uchunguuzi wa habari za aina tofauti juu ya udhalilishaji ndani ya jamii, maana habari za kina ilikuwa hazijaandikwa”,alifafanua.

Afisa ustawi wa jamii wilaya ya Wete Haroub Suleiman Hemed, alisema mradi wa GEWE umesaidia sana wilaya ya Wete na hasa zile shehia sita, zilizpotiwa na mradi.

Alisema walau jamii imepata mwamko na kujua wajibu wao, katika mapambano ya kutokomeza udhalilishaji wa kijinsia, jambo ambalo kabla, walidhani ni kazi za taasisi husika.

“Sasa inaonekana jamii, imepata uthubutu wa alau kutoa ushirikianao na wahusika wanapopita kwenye jamii, maana wanaona kuwa, kushughulikia metendo haya ni jukumu la kila mmoja”,alifafanua.

Hakimu wa Mahakama ya mkoa Chakechake Khamis Ali Simai, alisema, mashahidi wote wanaofika mahakamani, wamekuwa wakipewa nauli zao kama kawaida.

Hata hivyo alisema, kukosekana kwa nauli hiyo kusiwarejeshe nyumbani mashahidi, maana suala la kutoa ushahidi ni haki yao, hasa katika kuusaidia muhimili wa mahakama, kufanikisha kazi zake.

“Jamii ijipange vyema kuhakikisha wanakuwa na hamu kufika mahakamani kutoa ushahidi, kwani hakuna kesi ambayo itafikia tamati, pasi na kuwepo kwa mashahidi”,alifafanua.


Shehia ambazo zimo kwenye mradi wa GEWE ni Kiungoni, Shengejuu, Mchanga mdogo, Mjini ole, Kangagani na Kinyikani ndani ya wilaya ya Wete kisiwani Pemba.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.