Habari za Punde

‘Walimu wa Kiswahili Fundisheni Kwa Weledi’

Na Ali Issa Maelezo, Zanzibar 
WALIMU wa somo la Kiswahili katika skuli za sekondari, wametakiwa kufuata misingi na taratibu za ufundishaji ili wanafunzi wanaowafundisha waweze kufaulu somo hilo kwa kiwango cha juu.
Akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Kiswahili Zanzibar kwenye ofisi Baraza la Kiswahili Zanzibar (BAKIZA) Mwanakwerekwe, Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Mmanga Mjengo Mjawiri, amesema wanafunzi wengi wamekuwa wakifeli mitihani ya somo hilo kutokana na walimu kutofuata misingi ya taaluma na taratibu za ufundishaji.
Amesema kimsingi, wanafunzi wa lugha ya Kiswahili hawapaswi kufeli somo hilo kwa idadi kubwa ikizingatiwa kwamba hiyo ni lugha yao ya asili na wanaitumia katika harakati zao zote za maisha.
“Lugha ya Kiswahili ni taaluma kama nyengine, ina kanuni na misingi yake ya kufundishia ambayo isipotumika vyema kitachofuata ni kufeli kwa wanafunzi,” alisema Mjawiri.
Alieleza kuwa, iwapo walimu wa somo la Kiswahili wanataka kupasisha wanafunzi wengi, ni lazima wasomeshe kwa ubora, kiwango na utaalamu unaostahili.
Naibu Waziri huyo alisema, utafiti unaonesha kuwa hali ya ufundishaji wa somo la Kiswahili iko chini kielimu na kiutaalamu, jambo alilosema linasababishwa na walimu kutokuwa na bidii ya kufundisha.
Aidha alisema walimu wengi hawapendi kujisomea, akieleza kuwa jambo hilo linawafanya kutokuwa na tabia ya kuwauliza maswali  wanafunzi.
Kwa hivyo aliwahimiza walimu kujifunza njia na mbinu mbalimbali za kufundishia, pamoja na kuwapima wanafunzi kwa kuwapa kazi nyingi za kufanya ili kujiridhisha na ufahamu wao.
Mapema, Mwenyekiti wa BAKIZA Dk. Mohammed Seif Khatib, alisema ni aibu kubwa kwa Wazanzibari kufeli mitihani ya Kiswahili wakati wao ndio wataalamu wa lugha hiyo.
Lakini hata hivyo, alishauri walimu wa somo hilo wapewe nyenzo za kufanyia kazi iwapo kuna dhamira ya kweli kutoa idadi kubwa ya wanafunzi wanaofaulu somo hilo.
Kwa upande mwengine, Mwenyekiti huyo ambaye pia ni gwiji wa lugha ya Kiswahili aliyeandika vitabu  mbalimbali, alisema mashindano ya wanafunzi ni miongoni mwa njia nzuri za kuinua vipaji na kuzalisha  wataalamu wazuri wa baadae.
Akizungumza katika hafla hiyo, Kaimu Katibu Mtendaji wa BAKIZA Dk.  Omar Abdalla Adam, alisema bajeti finyu inachangia baraza hilo kushindwa kutoa machapisho ya vitabu na vipeprushi.
Kwa hivyo aliiomba serikali ifikirie uwezekano wa kuliongzea bajeti Baraza la Kiswahili Zanzibar ili liweze kutekeleza vyema mipango yake ya kuiendeleza lugha ya Kiswahili nchini.
Aidha aliiomba jamii hasa walimu, wachapishaji wa magazeti na watangazaji wa vyombo vya habari, kujenga utamaduni wa kupenda kununua na kusoma vitabu vya Kiswahili, sambamba na kukitumia vizuri katika kazi zao.  
IMETOLEWA NA IDARA YA HABARI MAELEZO
ZANZIBAR.
MACHI 13, 2018  

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.