Habari za Punde

Taka za palastiki ni tatizo la duniani


Rundo la taka za Plastiki katika moja ya madampo ya Marekani.
Na Ali Shaaban Juma
Katika kipindi cha miaka Hamsini iliyopita, dunia imeshuhudia ongezeko kubwa la uzalishaji wa bidhaa za plastiki. Katika mwaka 2013, jumla ya tani 299 Milioni za plastiki zimezalishwa duniani ikiwa ni ongezeka la asilimia 4% ikilinganishwa na uzalishaji wa mwaka 2012.  Kwa mujibu wa Shirika la Uhifadhi Mazingira la Umoja wa Mataifa UNEP,  (United Nations Environmental  Programme) matumizi ya plastiki yameongezeka duniani kutoka tani  Milioni 5.5 katika miaka ya 50 hadi tani Milioni 110 Milioni mwaka 2009.
Licha ya kuongezeka kwa uzalishaji wa plastiki kwa kiwango kikubwa, kiwango cha taka za plastiki zinazovurugwa kwa matumizi mengine ni madogo kulinga na uzalishaji. Matumizi ya bidhaa za plastiki yamekuwa yakiongozeka kwa kasi kwa vile bidhaa hizo zinachukua nafasi ya bidhaa za chuma na kigae zilizotumiwa kabla.
Taka na uchafu wa plastini “Plastic pollution”  ni mrundikano wa mabaki ya plastiki za aina mbalimbali zinazotokana na matumizi ya vifaa vilivyotengenezwa kwa bidhaa  hiyo ambazo huleta athari mbalimbali  kwa viumbe hai, binaadamu na mazingira. Kuna aina mbalimbali za palastiki ambapo kutokana na gharama ndogo za kutengeneza bidhaa za palastiki, matumizi ya palastiki yameongezeka sana duniani na kufanya bidhaa hiyo kuwa ni miongoni mwa vitu vinavyochafua mazingira.
Uchafuzi wa mazingira kutokana na taka za plastiki huathiri na kuharibu mazingira ya miji, ardhini, mito, maziwa, mashambani na hata baharini. Kutokana na kuenea kwa taka hizo, viumbe kadhaa wa baharini huathiriwa na kemilaki zitokanazo na taka hizo au kwa kula mabaki ya plastiki. Mara nyingi ng’ombe, mbuzi, kondoo na mifugo mengineyo huathirika kutokana na kula takataka za plastiki.
Nchi za viwanda zilizoendelea hasa  huzalisha taka nyingi za palastiki kuliko nchi za ulimwengu wa tatu, hali hiyo  inatokana na ukweli kwamba asilimia kuwa ya  bidhaa za kawaida katika mataifa hayo ni zile zilizofungwa katika mikebe au mifuko ya palastiki.
Katika mwaka 2007, Marekani ndiyo iliyozalisha taka nyingi za plastiki ambapo ilizalisha tani 230 Milioni za taka hizo.
Taifa la pili lilikuwa ni Urusi ambayo mwaka huo ilizalisha 200 Milioni na kufuatiwa na Japan iliyozalisha tani 52.36 Milioni za taka za plastiki. Tani 48.84 Milioni za taka zilizalishwa huko Ujerumani na kufatiwa na Uingereza iliyozalisha tani 34.85 Milioni, Mexico tani  32.17 Milioni  kiwango ambacho pia kilizalishwa na Ufaransa.  Italia kwa upande wake ilizalisha tani 29.74 za taka hizo.
Utafiti uliofanywa mwaka 2014 na Chuo Kikuu cha Georgia, Chuo Kikuu cha California na Shirika liitwalo “Sea Education Association” nchini Marekani  na kuchapishwa katika jarida la Sayansi liitwalo  “Journal Science” la mwezi wa Februari,2015 umeonesha kuwa  zaidi ya tani Milioni 8 za taka za plastiki zinatupwa baharini kila mwaka. Utafiti huo umeonesha kuwa  nchi 192 zilizo kando ya bahari katika bahari za Atlantiki, Pasifiki, Bahari ya Hindi, Meditereniani na bahari Nyeusi zinazalisha tani bilioni 2.5 za taka ambapo tani  275 kati ya hizo ni plastini zinazoishia baharini.
Utafiti huo umeonesha kuwa  tani 99.5 za plastiki huzalishwa katika miji iliyo kando ya bahari, ambapo tani 31.9 kati ya hizo kutupwa ovyo. Utafiti huo umebainisha kuwa  taka za plastiki zinazoelea baharini  duniani kote ni  wastani wa tani 245,000.
Kwa mujibu wa utafiti huo  katika mwaka 2010 nchi ambayo imeongoza duniani kwa kutupa taka nyingi za platiki baharini ni China ambayo ilitupa  baharini tani Milioni 8.8za taka za plastiki  na kufuatiwa na Indonesia iliyotupa tani Milioni 3.2. Nchi ya tatu kwa kutupa kwa wingi taka hizo ni Philippines iliyotupa baharini tani Milioni 1.9 za taka za plastiki na kufuatiwa na Vietnam iliyotupa tani Milioni 1.8.  Nchi nyengine za bara la Asia zilizotupa kwa wingi taka hizo ni  Sir Lanka iliyotupa tani  Miloni 1.6 za taka hizo  na Thailand iliyotupa tani Milioni moja.
Barani Afrika Misri ndiyo iliyotupa taka nyingi za plastiki bahari ambapo katika mwaka huo wa 2010, taifa hilo lilitupa tani milioni moja za taka hizo na kufuatiwa na Nigeria iliyotupa tani  Laki tisa. Huko Marekani ya kusini kinara wa kutupa taka za plastiki baharini ni Brazil ambayo ilitupa tani laki tano za taka hizo.
Marekani inazalisha tani  33.6 Milioni za taka za plastiki kila mwaka ambapo asilimi 6.5% ya taka hizo huvurugwa na kutengenezwa vitu vyengine na asilimia 7.7% hutumika kuzalisha umeme. Taka zilizobaki huishia mitaani na baharini.
Kwa upande wa matumizi ya mifuko na chupa za plastiki, utafiti huo umeonesha kuwa jumla ya mifuko ya plastiki Trilioni moja hutumika kila mwaka duniani.
Mifuko ya plastiki bilioni tatu hutumika kila siku huko China. Utafiti huo umeongeza kuwa nchini Marekani  jumla ya mifuko ya plastiki Bilioni 100 inatumiwa na raia wa taifa hilo kila mwaka. Jumla ya chupa za plastiki mia tano hutumiwa na kila familia kwa mwaka huko Marekani.
Kutokana na kuongezeka kwa matumizi makubwa ya bidhaa za plastiki duniani, taka zitokanazo na bidhaa hiyo huchangia asilimia kumi ya taka zinazotupwa ovyo mitaani na katika fukwe za bahari. Taka za plastiki hubaki muda mrefu ardhini na baharini bila kuoza ikitegemea aina ya plastiki iliyotumiwa kutengenezea bidhaa iliyotupwa.
Plasiki iliyofukiwa ardhini hutoa kemikali ambazo baada ya muda fulani huharibu  maji  ardhini na hivyo kupunguza ubora wa kiwango hicho cha maji hasa kwa watumiaji. Katika sehemu nyingi duniani hivi sasa kumejitokeza tabia ya  kufukia ardhi kwa kutumia takataka vinazokusanywa katika maeneo ya miji. Nyingi ya taka hizo huwa na mchanganyiko wa aina mbalimbai za plastiki ambazo baadhi  yake ni hatari kwa mfumo wa udongo.
Katika  bahari kuu duniani kuna taka nyingi za plastiki.  Taka hizo ni pamoja na taka zilizotupwa kwa makusudi na meli kubwa za mizigo zinazosafiri katika bahari hizo. Vilevile manowari na meli za utafiti hutupa bahari  shehena kubwa ya taka za plastiki ambazo hazina matumizi. Kutokana na udogo wake, mara kadhaa boti za kutembelea baharini ambazo hukosa nafasi  ya kuweka takataka hutupa baharini mabaki ya plastiki na kuchangia uchafuzi wa mazingira. Mbali ya aina zote hizo za uchafuzi, mchafuzi mkubwa wa mazingira ya bahari kwa kuputa taka za plastiki ni meli za uvuvi ambazo hutupa baharini  nyavu na aina nyengine za mitego.
Ingawa taka nyingi za plastiki zinazotupwa baharini hutupwa na vyombo vinavyosafiri au kuvua baharini, lakini pia kuna taka za plastiki zinazochafua bahari ambazo hutoka ardhini. Mara nyingi taka za plastiki za aina hii ni mabaki ya chupa, mifuko na makopo  yanayoelea ambayo hukokotwa na maji  hadi baharini. Pia taka hizo hutupwa kutoka  nyumba zilizo karibu na fukwe za bahari.

Maisha ya viumbe kadhaa wa baharini wakiwemo kasa, seal, samaki na ndege hufariki dunia kwa kunasa katika jarife ambazo zilizokwama chini ya bahari.
Ripoti iliyochapishwa mwaka 2006  iliyopewa jina “Plastic Debris in the World’s Oceans” imeonesha kuwa zaidi ya viumbe Laki nne wa  aina mbalimbali wa baharini wanakufa kila mwaka kutokana na kuathiriwa na taka za plastiki zilizomo baharini. Baadhi ya kasa huishi kwa kula mayavuyavu ya baharini  (jelly fish). Lakini baadhi ya wakati kasa hao hula vipande vya taka za plastiki vinavyofanana na  Mayavuyayu ya baharini na hivyo hufariki kwa vile kipande hicho cha plastiki huziba njia ya kupitishia chakula ya  kasa huyo. Mara kadhaa Nyangumi wanaofariki na kupwelewa ufukweni na kufanyiwa utafiti hukutwa na vipande vya plastiki katika matumbo yao ikiwa ni kiashiria kuwa nyangumi huyo amefariki kutokana na kula plastiki hiyo.
Taka za plastiki zinazotupwa baharini haziathiri samaki na viumbe wengine wa habarini peke yao, lakini pia huleta madhara kwa ndege wa pwani. Katika mwaka 2004, Mashakwe kadhaa walokufa  katika bahari ya kaskazini walikutwa na vipande vya plastiki katika matumbo yao. Uchunguzi ulionesha kuwa vipande vya plastiki vinavyoelea baharini huwababaisha ndege hao na kudhani kuwa ni chakula na hivyo humeza plastiki hizo.
Wataalamu wa mazingira nchini Marekani wanakisia kwamba kiasi  Mashakwe milioni moja waitwao’ “Laysan albatrosses wanaoishi katika kisiwa kidogo kiitwacho Midway Atoll  kilichoko huko Hawaii nchini Marekani wana mabaki ya plastiki katika matumbo yao. Ndege hao hula vipande vya plastiki vyenye rangi nyekundu, buluu,waridi na rangi ya udongo kwa vile rangi hizo hufanana na aina mbalimbali za vyakula wanavyokula . Tatizo hilo lilijulikana baada ya idadi kubwa ya ndege hao kufa na mizoga ya kukutwa katika ufukwe wa kisiwa hicho. Baada ya kuchunguzwa, ndipo mabaki mengi ya ndege hao yalikutwa na vipande kadhaa vidogo vidogo vya plastiki walivyokula.

Mwandishi wa makala haya ni Mwalimu wa Chuo cha Uandishi wa Habari cha ZJMMC, Kilimani mjini Zanzibar.
E-Mail: Rafikifumba1@hotmail.com

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.