Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk.Ali Mohamed Shein, akihutubia wakati alilifungua Kongamanola Pili la Kiswahili la Kimataifa lililoandaliwa na Baraza la Kiswahili la Taifa Zanzibar,(BAKIZA) katika Ukumbi wa Sheikh Idrissa Abdulwakil Kikwajuni Zanzibar, na kuwashirikisha Watunzi wa Vitabu kutoka Sehemu mbalimbali.
Rais wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, amesema Kongamano la
Kiswahili linaloendelea lina mchango muhimu katika kuendeleza historia, maendeleo
ya Kiswahili pamoja na kuitambulisha Zanzibar kimataifa.
Alisema kongamano hilo hutoa fursa ya kuendeleza uhusiano kati ya
wataalamu wa lugha hiyo popote walipo
duniani .
Dk. Shein amesema
hayo leo katika Ukumbi wa Sheikh Idrissa Abdul-wakil Kikwajuni mjini hapa,
alipofungua Kongamano la Pili la Kimataifa la Kiswahili.
Kongamano hilo la
siku mbili, limeandaliwa na Baraza la Kiswahili Zanzibar (BAKIZA) na
kuwashirikisha wataalamu na mabingwa wa lugha ya Kiswahili, watunzi wa vitabu,
waandishi wa riwaya;tamthilia na mashairi pamoja na wapenzi wa lugha hiyo kutoka
maeneo mbali mbali ndani na nje ya nchi.
Alisema Zanzibar
inatambulika duniani kote kuwa ndio
chimbuko la Kiswahili fasaha kinachotokana na lahaja ya Kiunguja mjini
ambayo ilipitishwa mwaka 1930, hivyo
akatowa wito wa Kongamano hilo litumike
kuiendeleza historia hiyo.
Alisema kukuwa, kuenea na kuimarika kwa matumizi ya
kiswahili fasaha, kumechangiwa na sababu mbali mbali, na kubainisha kuwa hatua
hiyo inategemea sana kuwepo kwa juhudi za makusudi za kitaasisi pamoja na
makundi maalum ya wataalamu.
"Ni dhahiri
kuwa jambo hili haliwezi kufanikiwa kwa sadfa au fuluku, bali ni lazima iwepo
dhamira ya dhati, mipango na mikakati madhubuti pamoja na ari ya kuwa tayari
katika utekelezaji wake", alisema.
Akinasibisha hali
hiyo na kauli yake, Dk. Shein alisema Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius
Kambarage Nyerere na marehemu mzee Abeid Amani Karume walikuwa na dhamira ya
dhati ya kuimarisha lugha hiyo na ndio maana
kwa nyakati tofauti lugha hiyo ilitangazwa kuwa lugha rasmi ya Taifa na Zanzibar mwaka 1964 , sambamba na
Lugha ya Taifa la Tanzania (1967).
Alisema Serikali
zote mbili muda wote zimekuwa zikihikimiza matumizi sahihi ya lugha hiyo katika
vikao vyote rasmi pamoja na mikutano ya Kimataifa ndani ya nchi.
Aidha alieleza kuwa
ni jambo zuri kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki nayo kutambuwa jitihada
zinazochukuliwa katika kukiendeleza kiswahili, hivyo kuchukua hatua ya
kuanzisha Ofisi ya Kamisheni ya Kiswahili ya Afrika Mashariki hapa Zanzibar
mwaka 2007.
Dk. Shein ,
alipongeza juhudi za nchi za Rwanda na Afrika Kusini katika kuimarisha matumizi
ya lugha hiyo, kwa kuanza kufundishwa katika skuli zao.
Aliwataka vijana
wanaochukuwa masomo ya Kiswahili katika vyuo vikuu mbali mbali nchini,
kuchangamkia fursa za ajira zilizopo katika maeneo mbali mbali ya Ukanda wa Afrika
Mashariki.
Vile vile
alisisitiza haja ya taasisi zinazoendeleza matumizi bora ya lugha ya kiswahili
pamoja na wasomi, kutumia machapisho ya
lugha hiyo kufanya tafiti ili kujenga
uwezo wa kiutafiti na kuandika mambo mbalimbali yanayohusu ukuaji wa lugha hiyo
na utamaduni wake.
Aidha alisisitiza
umuhimu wa kuelekeza nguvu katika
kufanya tafiti nyingi zaidi kwenye fani mbali mbali za Isimu, fasihi na
Utamaduni wa kiswahili.
Alisema tafiti
zitasaidia sana katika kufanikisha dhamira ya kuendeleza lugha hiyo pamoja na
kuchangia upatikanaji wa maarifa mapya kwa wataalamu wa lugha na kujifunza
matumizi fasaha ya ya lugha hiyo.
"Hali hiyo
itapunguza kama sio kumaliza kabisa tatizo liliopo la kulazimisha utowaji wa
misamiati bila ya kurejea katika usuli wenyewe wa lugha", alifafanua.
Alibainisha kuwa
utafiti utawasaidia wataalamu wa lugha hiyo kuzungumza kwa hoja na kusimamia
hoja zao badala ya kuzungumza mambo kwa mazoweya.
Aidha, aliagiza
kutumiwa fursa ya kuwepo kwa Tume ya Taifa ya sayansi na Tdeknolojia katika
kufanikisha tafiti hizo.
Alieleza kuwa
katika kutilia mkazo suala la kufanya utafiti, kwa kuanzia katika mwaka wa
fedha wa 2018/2019 Serikali imetenga jumla ya shilingi Milioni 500 kwa ajili ya
tafiti za aina zote, hivyo akatowa wito
kwa wanaohitaji kufanya utafiti kutumia fedha hizo zilizotengwa.
Dk. Shein aliwataka
washiriki wa Kongamano hilo kujivunia lugha hiyo, kwa vile haiihitaji mwega wa
kusaidiwa ili kukamilisha mawasiliano.
Alieleza kuwa
Kiswahili ni lugha inayojitosheleza kwa msamiati na kuwezesha mawasiliano
katika nyanja zote, hivyo kukidhi haja
na hoja za watumiaji wa lugha hiyo katika mawasiliano.
Aliwataka wataalamu
wa lugha ya kiswahili kulitumia Kongamano lililoandaliwa ipasavyo, kwa
kubainisha changomoto zilizopo na kupendekeza mbinu sahihi za kukabiliana nazo.
Alisema ni wakati
muafaka wa kuangalia mafanikio yaliofikiwa na kuibuwa mbinu za kuyakuza na
kuyadumisha.
Aidha, alisema
amefurahishwa na hatua ya wandaaji wa kongamano hilo ya kuwahusisha
wachapishaji wa vitabu, na kubainisha kuwa hatua hiyo itawezesha kuwatambuwa na
kuona baadhi ya kazi zao.
"Ni matumaini
yangu kuwa Kongamano hili la siku mbili lililosheheni wataalamu na
mabingwa wa lugha litazingatia hoja na
ukumbi huu utarindima mijadala moto moto
ya kitaalamu", alisema.
Aidha alisema Kongamano
hilo litatowa mbinu muafaka zitakazoweza kukabiliana na changamoto mbali mbali
zinazoikumba lugha hiyo, ikiwemo uchapishaji wa kazi za waandishi, hususan wale
wanaochipukia.
Katika hatua
nyengine, Dk Shein aliwatunuku vyeti vya heshima, magwiji wa tungo za mashairi
ya taarabu asilia Zanzibar, ambao kazi zao zimeendelea kutambulika kwa
ubora na kutumika hadi leo hii.
Aliowatunuku (kwa
niaba) ni pamoja na Marehemu Bakar Abeid Ali, Marehemu Hijja Saleh Hijja,
marehemu Idd Abdalla Farahan na Masauni Yussuf.
Aidha, aliwatunuku
vyeti vya heshima waandishi wa Vitabu vya Riwaya maarufu, ambao ni Mohammed
Said Abdalla, Mohamed Suleiman Mohamed, Pro. Said Ahmeid Mohamed, Adam Saffi
Adam na Marehemu Seif Salim.
Mapema Waziri wa
Vijana, Utamaduni, Sanaa na Michezo Balozi Ali Karume alisema Wizara kupitia
BAKIZA inaendelea na mchakato wa kukusanya orodha ya wataalamu wa lugha ya
kiswahili, ili kuwa na kumbu kumbu sahihi kwa lengo la kuwatambuwa na kuwatumia
pale watakapohitajika.
Alisema kiswahili
ni bidhaa adhimu, hivyo ni vyema kwa wanafunzi kujifunza kutoka kwa watangulizi
kupitia makala mbali mbali, ili kubaini chimbuko na asili ya Kiswahili fasaha.
Aliwataka vijana na
wapenzi wa lugha hiyo kutumia fursa ya kujifunza kutoka kwa magwiji na
wataalamu wa lugha hiyo kupitia kazi mbali mbali walizofanya.
Nae, Mwenyekiti wa
Baraza la kiswahili Zanzibar (BAKIZA) Dk. Mohamed Seif Khatib alisema ni wakati
muafaka kwa serikali kulazimisha matumizi fasaha ya lugha ya kiswahili, kwa
kutambuwa kuwa ni bidhaa yenye thamani kubwa kiuchumi na utamaduni.
Alisema kuna
umuhimu mkubwa wa kuendelea kuwaenzi na kutahmini kazi za wataalamu w alugha ya
kiswahili kwa kuwawekea makumbusho
pamoja na majina yao kutumika katika mitaa mbali mbali kutokana na mchango wao
mkubwa wa kukuza lugha hiyo.
Aidha, Katibu
mtendaji wa BAKIZA, Mwanahijja Juma Ali alisema uchapishaji wa vitabu kupitia
lugha ya kiswahili unainuwa mapato na uchumi wa nchi, hivyo akaiomba Serikali
kuendelea kuwahamasisha wananchi kusoma vitabu.
Abdi
Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822
E-mail: abdya062@gmail.com
No comments:
Post a Comment