Habari za Punde

Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, Amesisitiza Viongozi wa CCM wa Majimbo Kwenda Kwa Wananchi Waliowapigia Kura Kwa Lengo la Kusikiliza Changamoto Zinazowakabili.


 



RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein  ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar amewasisitiza viongozi wa CCM wa Majimbo kisiwani Pemba kwenda kwa wananchi waliowapigia kura kwa lengo la kuwasilkiliza changamoto zinazowakabili.

Rais Dk. Shein aliyasema hayo wakati akizungumza na viongozi wa CCM wa Wilaya ya Wete Pemba pamoja na kufanya Majumuisho ya ziara yake kwa Wilaya hiyo, yaliyofanyika katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi Wete, Mkoa wa Kaskazini Pemba ambapo viongozi mbali mbali walihudhuria akiwemo Mke wa Rais wa Zanzibar Mama Mwanamwema Shein.

Makamu Mwenyekiti alitumia fursa hiyo kuwasisitiza viongozi wa Majimbo wakiwemo Wawakilishi wote ambao ni wa CCM na Wabunge wa Viti Maalum wa CCM kwenda kwa wananchi wao ili wajue changamoto zinazowakabili na kuzitafutia ufumbuzi sambamba na kuwa nao karibu ili kukiimarisha chama chao.

Alieleza kuwa CCM hatomridhia kiongozi wa Jimbo ambaye amechaguliwa na wananchi lakini kwa kipindi hichi amekuwa haonekani Jimboni kwake kwenda kuwasaidia wananchi na kusahau wajibu wake wa kwenda kuwatumikia wananchi.

Alieleza kuwa iwapo viongozi hao wataendelea kuwa karibu na wananchi pamoja na kwenda kuwasikiliza changamoto zinazowakabili hali hiyo itawapelekea wananchi hao waendelee kukiunga mkono chama chao cha CCM na kuendeleza ushindi katika uchaguzi mkuu ujao wa 2020.

Aidha, Makamu huyo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inayoongozwa na CCM itaendelea kutekeleza majukumu yake ya kuwapelekea maendeleo endelevu wananchi wote wa Unguja na Pemba tena bila ya ubaguzi.

Alieleza kuwa CCM itahakikisha wananchi wote wanapata huduma sawa na sio kwa upandeleo kama ilivyokuwa wakati wa ukoloni ambapo huduma za maendeleo zilikuwa zikitolewa kwa upendelea zikiwemo huduma za elimu,afya na nyenginezo.

Aidha, Rais Dk. Shein aliwataka viongozi wa Chama na Serikali kufanya ziara za kuwatembelea wananchi ili kujua matatizo waliyonayo na kuyatafutia ufumbuzi badala ya kukaa ofisini.

Aliongeza kuwa kuwafuata wananchi na kutatua shida zao ni agizo la CCM, ambalo lilitolewa katika Mkutano Mkuu wa CCM huko Dodoma ikiwa ni moja ya Utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM.

Alisisitiza kuwa viongozi wa Chama na Serikali kwa pamoja wanapaswa kwenda kwa wananchi kwa lengo la kuwaeleza matatizo na mafanikio ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na mipango ya Serikali.

Aliwataka viongozi hao kuwa karibu na wananchi na kwenda kuwasaidia katika masuala yao ya kijamii hasa wale Wawakilishi na Wabunge wa Viti Maalum kisiwani humo kwani chama chao ndio kinachoongoza Serikali.

Rais Dk. Shein aliwakumbusha viongozi wa CCM kufanya kazi za chama na kuwataka kwa kila mmoja kufanya kazi kwa kuzingatia wadhifa wake ikiwa ni pamoja na kufanya ziara kwa pamoja kati ya viongozi wa Chama na Serikali na baadae kufanya tathmini.

Dk. Shein aliwataka viongozi hao wa Chama na Serikali kuwabainisha watendaji wote waliokuwa hawafanyi kazi ipasavyo na wamekuwa wakifanya kazi kwa maslahi yao binafsi.

Makamu Mwenyekiti huyo wa CCM alieleza kuvutiwa na taarifa ya Chama na Serikali ya Wilaya hiyo na kutoa pongezi zake na kusifu ushirikiano uliopo kati ya pande mbili hizo hatua ambayo imepelekea mafanikio makubwa.

Sambamba ya hayo, Makamu Mwenyekiti huyo alisisitiza kuwa kwenye siasa za vyama vingi hakuna kutishana na wala kutukanana na kuwataka viongozi wa CCM Wilaya hiyo ya Wete na Mkoa wote wa Kaskazini Pemba kufanya kazi zao za kukiimarisha chama chao bila ya hofu.

Pia, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuupongeza uongozi wa Mkoa huo kwa kuendelea kusimamia amani na utulivu na kuwaeleza wananchi kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kusimamia amani na utulivu kwa wananchi wote wa Unguja na Pemba popote pale walipo.

Pia, aliupongeza uongozi wa Serikali wa Wilaya hiyo kwa kutekeleza vyema Ilani ya Uchaguzi ya CCM kwa kukusanya vyema mapato yake.

Nao uongozi wa CCM Wilaya na Mkoa wa Kaskazini Pemba ulitoapongezi zake kwa Rais Dk. Shein kwa jinsi anavyotekeleza Ilani ya Uchaguzi na kusisitiza kuwa CCM katika Wilayaya Wete iko imara.

Rajab Mkasaba, Ikulu
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.