Mbunge
wa Jimbo la Chamwino Mhe. Joel Mwaka akifungua mafunzo kwa wakulima
waliorasimisha mashamba yao na kupata hati za kimila za kumiliki ardhi kupitia
Ofisi ya Rais, Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge
Tanzania (MKURABITA) leo Wilayani
Chamwino mkoani Dodoma.
Mratibu
wa MKURABITA Bi. Seraphia Mgembe akisisitiza umuhimu wa wananchi kutumia hati
za kimila za kumiliki ardhi kujiletea maendeleo wakati wa ufunguzi wa mafunzo
yakuwajengea uwezo wakulima zaidi ya 100 wa vijiji vya Membe na Mahama Wilayani
Chamwino mkoani Dodoma.
Meneja urasimishaji ardhi vijijini kutoka MKURABITA Bw. Antony Temu akieleza faida za mafunzo
yakuwajengea uwezo wakulima wa Wilaya ya Chamwino katika Kijiji cha Membe ili waweze kutumia hati milki za kimila za kumiliki ardhi
walizopata kujiletea maendeleo.
Mratibu
wa MKURABITA Bi. Seraphia Mgembe akisisitiza jambo kwa Mwenyekiti wa Kijiji cha
Membe Bw. Yoram Majenda leo Wilayani Chamwino mara baada ya ufunguzi wa mafunzo
kwa wakulima zaidi ya 100 na viongozi 10 yakilenga kuwajengea uwezo wa kutambua
fursa zilizopo baada ya kurasimisha mashamba yao na kupata hati milki za kimila
za kumiliki ardhi.
Sehemu
ya wanachi walioshiriki hafla ya kufungua mafunzo kwa wakulima zaidi ya 100 na
viongozi 10 katika kijiji cha Membe wilayani Chamwino mkoani Dodoma
wakifuatilia hotuba ya mgeni rasmi ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Chamwino mkoani Dodoma Mhe.
Joel Mwaka leo Wilayani humo.
(Picha
zote na MAELEZO)
Mbunge
wa Jimbo la Chamwino mkoani Dodoma Mhe. Joel Mwaka akiwa kwenye picha ya pamoja
na sehemu ya wananchi waliopatiwa hati za kimila za kumiliki ardhi baada ya kurasimisha
mashamba yao katika Kijiji cha Membe.
Frank
Mvungi – MAELEZO, Dodoma.
Mpango wa Kurasimisha
Rasilimali na Biashara za Wanyonge Tanzania (MKURABITA) umepongezwa kwa
kuwawezesha wananchi Wilayani Chamwino mkoani Dodoma kwa kuwajengea uwezo ili
waweze kutumia hati za kimila za kumiliki ardhi kujiletea maendeleo.
Akizungumza leo
Wilayani humo wakati akifungua mafunzo kwa wakulima zaidi ya 100 wa Kijiji cha Membe mbunge wa jimbo hilo Mhe.
Joel Mwaka amesema kuwa wananchi wanajengewa uwezo ili waweze kutumia hati hizo kujiletea
maendeleo ikiwemo kuzitumia kama dhamana kuchukua mikopo katika Taasisi za
fedha kama mabenki.
“ Nawapongeza Ofisi ya Rais- MKURABITA kwa kuwezesha mashamba 1145 kupimwa na tayari
hatimiliki za kimila 1000 zimeweza kuandaliwa ili kuwawezesha wananchi
kuzitumia kujikwamua kiuchumi” Alisisitiza
Mwaka.
Akifafanua amesema
kuwa kuna umuhimu wa kuunga mkono juhudi
za MKURABITA kwani kati ya vijiji 107 vilivyopo katika halmashauri hiyo ni viwili tu vimebahatika kupata fursa ya
kurasimishiwa ardhi na kujengewa uwezo kupitia mafunzo yanayoendeshwa na mpango
huo kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya hiyo.
Aliongeza kuwa kuna
umuhimu mkubwa kwa wananchi kujitokeza kuchukua hati zao ili wazitumie
kujikwanua kiuchumi kwa kuwa zimeshandaliwa na ziko tayari.
“ Faida za hati hizi
ni pamoja na kuhakikisha usalama wa milki ya mkulima, kuongeza thamani ya ardhi
na pia itasaidia kukuza uchumi wa Wilaya ya Chamwino na Taifa kwa ujumla”
Alisisitiza Mwaka.
Alibainisha kuwa wakulima
hao zaidi ya 100 watakuwa chachu ya kutosha kwa Wilaya hiyo na kuleta
mabadiliko makubwa katika uzalishaji kwenye kilimo na ufugaji na hivyo kuongeza
tija na kipato kwa wakulima wilayani humo.
Kwa upande wake
Mratibu wa MKURABITA Bi. Seraphia Mgembe amesema kuwa Dhamira ya Serikali ya
Awamu ya Tano ni kuhakikisha kuwa wanachi wanajikwamua kiuchumi kupitia
uwezeshaji unaofanywa kwa kurasimisha mashamba ya wananchi na kuwapa hati ili
waweze kuzitumia kujiletea maendeleo.
“ Mkitumia hati hizi
vizuri kama Serikali ilivyodhamiria mtajikwamua kichumi kwani hapa kila
aliyepewa tayari ajihesabu kuwa yeye ni mmiliki wa ardhi yenye thamani na
inayoweza kuleta mageuzi makubwa katika maisha yake” Alisisitiza Bi. Mgembe.
Akifafanua zaidi
amesema kuwa ni vyema wananchi wakaepuka vitendo vya kuuza ardhi zao kiholela
badala yake wazitumie kwa tija hata pale wanapoamua kuuza sehemu ya maeneo yao
walenge kujiletea maendeleo ili kuendana na dhana ya kujenga uchumi jumuishi
inayosisistizwa na Serikali .
MKURABITA itaendesha
mafunzo hayo kwa siku tatu yakilenga kuwajengea uwezo wakulima wa kijiji cha
Membe kuzalisha kwa tija kupitia kilimo cha alizeti, ufugaji na pia watapata
kujengewa uwezo kuhusu namna ya kutunza kumbukumbu, utafutaji fursa na namna ya
kuzitumia, uandishi wa mpango wa biashara na uundaji wa vikundi vya hiari,
utunzaji wa kumbukumbu na uthamini wa ardhi na utunzaji wa mazingira.
No comments:
Post a Comment