Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, Ahutubia Maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani Mei Day.



Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, akihutubia Wafanyakazi na Wananchi Zanzibar katika Maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani Mei Day katika ukumbi wa Dk. Ali Mohamed Shein, Chuo Kikuu cha Taifa SUZA Tunguu Zanzibar Wilaya ya Kati Unguja.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, amesema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Awamu ya Saba tangu ilipoingia madarakani mwishoni mwa mwaka 2010 imechukua hatua mbali mbali katika kuyaimarisha mazingira ya watumishi ya kufanyia kazi na kuyashughulikia maslahi yao.

Alisema kuwa kuimarika kwa uchumi kumewesha katika awamu hii kuyafanya maslahi ya wafanyakazi yawe bora kwa mara nne pamoja na kuubadilisha mshahara wa kima cha chini kwa asilimia mia moja.
Aliyasema hayo wakati akihutubia wafanyakazi katika maadhimisho ya siku ya wafanyakazi duniani, yaliofanyika ukumbi wa Dk. Ali Mohamed Shein, uliopo katika Kam;pasi ya Chuo Kikuu cha Taifa (SUZA) Tunguu  Mkoa wa Kusini Unguja.
Hivyo, alisisitiza kuwa kutokana na mafanikio yaliyopatikana ya  kuimarika kwa uchumi, kuyasimamia mapato vizuri hapana shaka suala la kuyaimarisha maslahi  wafanyakazi ataendelea kulipa uzito unaostahiki suala la kuimarisha maslahi ya wafanyakazi.
Alisema ujumbe wa mwaka huu wa siku ya wafanyakazi unaosema ‘kuimarika kwa uchumi wa taifa, kuendane na kuongezeka kwa maslahi ya wafanyakazi’ utaendelea kuzingatiwa na kufanyiwa kazi na serikali kadiri hali ya ukuaji wa uchumi utakavyozidi kuimarika.
Aidha, alisema  kuimarika kwa  amani na utulivu, imeifanya Zanzibar kuwa katika karne mpya ambapo changamoto zote zinazojitokeza  hutatuliwa kwa njia ya  majadiliano na hatimae kupatiwa ufumbuzi.
Alisema viongozi wa serikali na taasisi binafsi  wanaamini kwamba njia pekee ya kutatua matatizo ni kukaa pamoja na kujadiliana kwa busara na  sio kutumia mapambano au mivutano isiyo na tija.
Aidha alisema, mfumo huo ndio unaotekelezwa baina ya Serikali na Shirikisho la Vyama Huru vya Wafanyakazi, kutokana na pande zote mbili kuelewa kwamba watu wote ni wamoja na wanategemeana katika kuleta maendeleo. 
“Leo tuko katika karne nyengine,karne ambayo kwa mnasaba wa kudumisha amani na utulivu katika sehemu zetu tunazoishi ,inatupasa tuzitatue changamoto zinazotukabili kwa utaratibu wa kukaaa pamoja na kujadiliana kwa busara hadi kufikia ufumbuzi,”alisema.
Alisema serikali inazingatia haja ya kuendeleza na kuimarisha ushirikiano na vyama vya wafanyakazi sambamba na kuchukua hatua zinazostahiki kwa dhamira ya kuyashughulikia masuala ya wafanyakazi ili kuongeza kasi ya maendeleo, kukuza uchumi na kuimarisha ustawi wa jamii.
“Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa awamu zote saba za uongozi,imekuwa ikithamini na kutambua kuwa wafanyakazi ni nguzo kubwa na msingi wa kukuza uchumi na kuongeza kasi ya maendeleo ya nchi yetu,” alisema.
Katika hatua nyengine alisema,hoja zote zinazowasilishwa serikalini na shirikisho la vyama vya wafanyakazi Zanzibar  zinafanyiwa kazi  na kutekelezwa.
Alisema miongoni mwa hatua zilizochukuliwa kwa wafanyakazi  mara baada ya kuimarika kwa uchumi ni pamoja na  kuimarisha mazingira  mazuri ya watumishi na kuyashughulikia maslahi yao.
Alisema kwa kutambua kwamba mazingira mazuri ya kufanyia kazi yanasaidia kuleta utulivu na kufanya kazi kwa umakini na hatimae kuleta ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi, serikali inaendelea na zoezi la ujenzi wa majengo ya ofisi za kisasa zinazokwenda na wakati.
Katika kuimarisha zaidi mfumo wa utumishi serikalini, alisema serikali imetunga na kuzifanyia mapitio sera, kanuni na sheria mbali mbali zinazohusiana na utumishi bora.
Aliwasisitiza viongozi na wafanyakazi kuzisoma sheria ili waweze kuzielewa na  kufanyakazi kwa kuzingatia miongozo ya kisheria  na kuleta ufanisi zaidi katika maeneo yao ya kazi.
“Natumia fursa hii kukusisitizeni viongozi na wafanyakazi wenzangu kwamba zitafuteni,zisomeni,mzifahamu na muyazingatie maudhui yaliomo katika nyaraka hizo ili muweze kufanyakazi zenu kwa kuzingatia miongozo ya sheria,”alisisitiza.
Alihimiza wafanyakazi kuzingatia maadili ya utumishi kwa lengo la kuhakikisha kuwa wananchi wanapatiwa huduma bora.
Aliwaasa wafanyakazi kuepuka vitendo vya ubadhilifu,wizi na uhujumu wa mali ya umma,rushwa,uzembe na unyanyasaji kwa wale wanaostahiki kuhudumiwa.
Akizungumzia mwenendo wa uchumi wa Zanzibar, alisema yapo mafanikio katika ukuaji uchumi na huduma za jamii na nyengine zimeimarika.
Alisema katika mwaka 2018 uchumi wa Zanzibar ulikuwa kwa kasi ya asilimia 7.1, mfumko wa bei uliendelea kushuka kutoka kasi ya asilimia 5.6 mwaka 2017 hadi asilimia 3.9 mwaka 2018.
Kuhusu makusanyo na matumizi, alisema yamezidi kuwa bora ambapo hali ya utegemezi wa bajeti ipo chini ya asilimia sita kutoka asilimia 43 iliyokuwa mwaka 2010 wakati serikali ya awamu ya saba ilipoingia madarakani.
Waziri wa Kazi,Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto, Maudline Castico, alizipongeza juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi wa Rais Dk. Shein kwa kuyashughulikia maslahi ya wafanyakazi huku akipongeza mashirikiano makubwa yaliopo kati ya Wizara yake na Shirikisho la Vyama vya Wafaanyakazi.
Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (ZATUC), Khamis Mwinyi Mohamed. alisifu juhudi zinazochukuliwa na serikali katika kusimamia migogoro na haki za wafanyakazi na kutatua changamoto 21 kati ya 23 zilizowasilishwa.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.