Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akizungumza na Uongozi wa Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais,Tawala za Mikoa,Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ katika mkutano wa utekelezaji wa mpango kazi wa Mwaka wa Fedha kwa kipindi cha Julai 2018-Juni 2019 na mpango kazi wa mwaka 2019-2020 uliofanyika leo katika ukumbi wa Ikulu Mjini Zanzibar,[Picha na Ikulu.] 04/09/2019.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Ali Mohamed Shein ameutaka uongozi wa
Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ
kuongoza kwa kufuata sheria, kanuni na Katiba ya nchi ili watekeleze vyema majukumu
yao.
Rais Dk. Shein aliyasema
hayo leo wakati alipokutana na uongozi wa Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali
za Mitaa na Idara Maalum za SMZ ulipowasilisha Taarifa za Utekelezaji wa Mpango
Kazi wa mwaka 2018/2019.
Katika maelezo yake, Rais Dk. Shein alisema kwamba
uteuzi alioufanya kwa viongozi wa Ofisi
hiyo hakuangalia uzuri wa mtu ukiwemo wa sura bali ni kwa uaminifu wao, uwezo wao
walionao wa kufanya kazi, nidhamu pamoja na taaluma walizonazo.
“Bado nina imani na uongozi huu hivyo nakuhimizeni
mtekeleze wajibu wenu kwa kutumia Sheria za Zanzibar, kanuni zilizopo pamoja na
Katiba kwani hata mimi natumia nyenzo hizi hizi kutekeleza majukumu yangu”,
alisema Dk. Shein.
Aliwaeleza viongozi hao kuwa matatizo yote
watakayopambana nayo yatatatuka kirahisi iwapo watafuata sheria zikiwemo sheria
za ardhi na kusisitiza kuwa iwapo watafuata sheria hizo hawatopata ugumu katika
kutekeleza majukumu yao.
Kuhusu suala zima la ugatuzi, Rais Dk. Shein
alisema kuwa Serikali imeamua kuanza na sekta tatu za afya, elimu na kilimo lakini
hata hivyo umeanza vizuri na fedha nyingi zimepelekwa katika Halmashauri hivyo,
aliutaka uongozi huo kuzisimamia vyema kwani hizo ni fedha za wananchi kwa
ajili ya huduma zao.
Rais Dk. Shein alitoa pongezi kwa uongozi wa Ofisi
hiyo Mamlaka ya Serikali za Mitaa kwa kukusanya mapato ya TZS Bilioni 12.032
sawa na asilimia 93.55 ya makadirio jambo ambalo ni mafanikio makubwa.
Aidha, Dk. Shein aliwataka viongozi wa Ofisi hiyo kukiri
na kutambua kwamba mwaka huu fedha walizoingiziwa katika Bajeti yao ni za
kutosha jambo ambalo limewapelekea kufanya kazi zao kwa ufanisi mkubwa jambo
ambalo halijawahi kutokea hapo siku za nyuma.
Aidha, Rais Dk. Shein alieleza hatua za makusudi
zitakazochukuliwa katika kuhakikisha huduma za afya zinaimarika katika
hospitali zilizopo visiwani ikiwa ni pamoja na kuwapeleka madaktari wakiwemo
wakunga.
Rais Dk. Shein aliupongeza uongozi huo huku akisisitiza
haja ya kufanya utafiti juu ya zao la korosho Kusini mwa kisiwa cha Pemba kwani
zao hilo linaweza kukubali hasa ikizingatiwa mazingira ya eneo hilo.
Dk. Shein alieleza haja ya kuimarisha mafunzo na
kuzitaka Wilaya na Mikoa kuzingatia haja ya kuwafundisha wafanyakazi wao ili
waweze kufanya kazi vizuri kwani Ofisi haiwezi
kufanya kazi vizuri iwapo wafanyakazi wake hawana ujuzi.
Rais Dk. Shein alisisitiza faida za kufanya
utafiti kwani kuna umuhimu katika kutekeleza majukumu ya kila siku ya Ofisi
hiyo na Ofisi nyengine za Serikali.
Aliongeza kuwa Serikali imeanzisha Jiji na yeye kumteua
Mkurugenzi wa Jiji la Zanzibar kutokana na vigezo vinavyohitajika kufikiwa hivyo,
matumaini yake kuwa kazi ya kuliendeleza na kuliimarisha jiji hilo itafanywa kwa
mashirikiano ya pamoja katika kuhakikisha azma hiyo inatekelezeka.
Nae Kaimu Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu
Mkuu Kiongozi Salum Maulid Salum alieleza haja ya mashirikiano na kukaa pamoja
kati ya taasisi za Serikali katika kutekeleza miradi inayokusudiwa ili kuepuka
hasara zisizo za lazima.
Mshauri wa Rais wa Zanzibar Pemba Dk. Maua Abeid
Daftari kwa upande wake alitoa pongezi na shukutani kwa Rais kwa kujenga
majengo ya Ofisi za Wizara za Serikali Gombani Pemba pamoja na kumpongeza kwa
kujengwa kwa makaazi ya Madaktari katika hospitali ya Mkoani jambo ambalo
litaimarisha huduma za afya kwa wananchi.
Mapema Waziri wa Nchi
Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ Haji
Omar Kheir akisoma muhtasari wa utekelezaji wa Mpago Kazi wa Ofisi hiyo alisema
hali ya usalama katika Wilaya na Shehia imeimarishwa na wananchi wanaendelea
kufanya shughuli zao za kujiletea maendeleo kwa amani na utulivu.
Alieleza kuwa ahadi
alizotoa Rais Dk. Shein za kujenga barabara ya Kinuni kutokea Makondeko
zzimetekelezwa na Mkandarasi kwa sasa yupo katika hatua ya uwekaji wa lami wa
barabara hiyo ya Kinuni yenye urefu wa kilomita 0.95 na kwamba kazi hiyo
itakamilika ndani ya mwezi wa Septemba, 2019.
Alisema barabara ya
Mwera Wilayani hadi Fuoni Mambosasa yenye urefu wa kilomita 3.4 Ofisi hiyo
imekamilisha hatua za kumpata Mkandarasi na Mkataba wa ujenzi wa barabara hio
umeshatumwa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu kwa hatua za Kisheria.
Aidha, alieleza kuwa
Ofisi hiyo imekamilisha ujenzi wa Kituo cha Daladala Kijangwani kwa uwekaji wa
lami ili kuhamisha Kituo cha Daladala cha Michenzani pia, ujenzi wa barabara ya
kuelekea Tume ya Uchaguzi Zanzibar yenye urefu wa kilimoita 1.8 ipo hatua ya
uwekaji wa kifusi na itakamilika katika hatua ya lami ifikapo Novemba 2019.
Alieleza kuwa Ofisi
imesimamia na kuutekeleza ugatuzi kwa lengo la kuimarisha huduma kwa wananchi
ambapo kwa mwaka 2018/2019 imefanikiwa kukamilisha muundo wa Serikali za Mitaa
kwa mujibu wa Sheria na miongozo kutoka Serikalini.
Waziri huyo alieleza
kuwa Ofisi hiyo ilipokea na kutiliana saini hati za makabidhiano ya ugatuzi kwa
majukumu yaliogatuliwa kutoka Wizara ya Elimu, Afya na Kilimo jambo
lililoondosha mgongano wa utekelezaji wa shuguli zilizogatuliwa.
Katika kuimarisha
taarifa za usajili wa matukio ya Kijamii, Waziri huyo alisema kuwa Ofisi
imesimamia zoezi la uandikishaji wa vitambulisho vipya vya Mzanzibari Mkaazi
ambalo lilifanyika katika Shehia zote 388 za Zanzibar.
Alisema kuwa Ofisi hiyo
tayari imeshaanza kazi ya kuzisimamia Jumuiya zisizo za Kiserikali (NGOs) kwa
kuzisajili zile tu ambazo zina sifa ya kusajiliwa.
Nae Katibu Mkuu wa Ofisi
hiyo Radhia Rashid Haroub akisoma taarifa ya Utekelezaji wa Mpango Kazi wa
mwaka 2018/2019 alieleza mafanikio yaliopatikana sambamba na juhudi
zinazoendelea kuchukuliwa na Ofisi hiyo.
Nao uongozi wa Ofisi
hiyo walieleza kuwa tayari wamefanya kazi ya kuwaelimisha na kuwaeleza wananchi
umuhimu wa utalii wa ndani na tayari wananchi hao wameanza kuuelewa hasa katika
maeneo ya Kaskazini Pemba ikiwemo Wilaya ya Micheweni.
Wakati huo huo, Rais Dk. Shein
alikutana na uongozi wa Idara Maalum za SMZ ambapo katika maelezo yake
aliupongeza uongozi huo kwa kuendelea kuwajenga vijana pamoja na Maofisa kuwa
na nidhamu, uadilifu na uzalendo mkubwa zaidi.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment