Na Veronica Kazimoto. Simiyu
Meneja wa Elimu kwa Mlipakodi kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Diana
Masalla amesema kuwa, mwananchi yeyote atakayefichua wakwepa kodi na TRA ikafuatilia
na hatimaye kodi hiyo ikagundulika ni kweli ilikuwa imekwepwa na ikakusanywa,
mwananchi aliyetoa taarifa hizo za ukwepaji kodi atalipwa asimilia 3 ya kodi iliyokusanywa
lakini haitazidi shilingi milioni 20.
Masalla ameyasema hayo wakati wa Jukwaa la Biashara na Uchumi lililofanyika katika
Wilaya ya Busega mkoani Simiyu ambalo lengo lake ni kujadili fursa, changamoto na kero
mbalimbali zinazowakabili wafanyabiashara na wawekezaji wilayani humo na kuzitafutia
ufumbuzi.
“Natoa wito kwa wananchi na washiriki wa jukwaa hili kuhakikisha mnawafichua wakwepa
kodi wote kwa sababu watu hao wanaiibia Serikali yetu mapato na wanarudisha nyumba
jitihada za Serikali za kuwaletea maendeleo wananchi wake,” Amesema Masalla.
Aidha, Masalla amewahimiza wafanyabiashara na wawekezaji walioshiriki jukwaa hilo
kuhakikisha kuwa wanatoa taarifa pindi wanapokuwa wamefunga biashara kutokana na
sababu mbalimbali ili kuepuka kuendelea kutozwa kodi au kuonekana wamekaidi kulipa
kodi.
“Ni muhimu kutoa taarifa TRA pale ambapo mfanyabiashara amefunga biashara yake lakini
pale anapofungua ni muhimu pia kuitaarifu TRA ili kuepuka kuendelea kutozwa kodi
unapofunga biashara na pia kuanza kutozwa kodi sahihi pale unapofungua biashara,”
amesisitiza Masalla.
Naye, Mwenyekiti wa wafanyabiashara Wilaya ya Busega David Mateko amempongeza
Meneja wa TRA Mkoa wa Simuyu kwa kutoa elimu ya kodi kwa makundi mbalimbali ya
wafanyabiashara mkoani humo pamoja na Mkuu wa Wilaya hiyo kwa kuwahamasisha
wafanyabiashara kulipa kodi kwa hiari na hatimaye kuifanya Wilaya ya Busega kuwa wilaya
ya pili kati ya wilaya 5 za mkoani Simiyu kwa ukusanyaji wa mapato ya Serikali
yanayosimamiwa na TRA.
“Nampongeza Meneja wa TRA katika Mkoa wetu wa Simiyu kwa kuwatembelea
wafanyabiashara na kuwapatia elimu ya kodi na pia nachukua fursa hii kumpongeza Mkuu
wetu wa Wilaya Mheshimiwa Tano Mwera kwa kutuhamasisha kulipa kodi kwa wakati na
sasa wilaya yetu imekuwa ya pili hapa mkoani kwa ukusanyaji Mapato yanayosimamiwa na
TRA,” alibainisha Mateko.
Jukwaa hili la biashara na uchumi wilayani Busega limewakutanisha wafanyabiashara na
wawekazaji zaidi ya 200 ambapo taasisi mbalimbali za Serikali zimealikwa kutoa mada
ikiwa ni pamoja na Mamlaka ya Mapato Tanzania.
No comments:
Post a Comment