Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb), akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Mpango wa Elimu kwa Umma kuhusu Sera, Sheria na Kanuni za Huduma Ndogo za Fedha, kutoka kushoto ni Mkurugenzi wa Benki Kuu (BoT), Kanda ya Kati Bw. Richard Wambali, Kaimu Kamishna Msaaidizi Idara ya Maendeleo ya Sekta ya Fedha wa Wizara ya Fedha naMipango Bi. Dionisia Mjema, , kutoka kulia ni Mkurugenzi wa Uendeshaji wa Mfuko wa Kuendeleza Sekta ya Fedha (FSDT) Bi. Irene Mlola na Mkurugenzi wa Sera na Mipango wa TAMISEMI Bw. John Cheyo.
Na. Peter Haule na Josephine Majura, WFM, Dodoma
Waziri wa Fedha na Mipango
Dkt. Philip Mpango, ameiagiza Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kusimamia Sekta Ndogo
ya Fedha kikamilifu ili kukomesha michezo michafu inayofanywa na baadhi ya watoa huduma ndogo za fedha nchini
na kusababisha upotevu wa mali za
wananchi.
Ametoa maagizo hayo,
wakati akizindua Mpango wa Elimu kwa Umma kuhusu Sera, Sheria na Kanuni za
Huduma Ndogo za Fedha, uliowakutanisha wadau mbalimbali zikiwemo Wizara, Idara,
Taasisi na watoa huduma za fedha.
Alisema kuwa kuna taasisi za huduma ndogo za
fedha ambazo zinatoa mikopo kwa masharti magumu ikiwa ni pamoja na viwango
vikubwa vya riba na tozo ambazo huanzia
asilimia 3 mpaka asilimia 20 kwa mwezi ambayo ni sawa na asilimia 36 mpaka 240
kwa mwaka na pia kukosekana kwa uwazi na masharti ya mikataba ya mikopo.
‘’Naiagiza Benki Kuu ya Tanzania ifuatilie kwa
makini mwenendo wa utoaji wa huduma ndogo za fedha kupitia mitandao (Digital
Microfinance Services) na pia elimu kwa umma ya huduma hiyo ya fedha iwe
endelevu na itolewe nchi nzima”, alieleza Dkt. Mpango.
Dkt. Mpango alisema kuwa
kwa muda mrefu takribani wananchi milioni 15.4 sawa na asilimia 55.3 ya nguvu
kazi ya Taifa walikua wanatumia huduma ndogo za fedha bila kuwepo kwa Sheria ya
kutambua na kulinda haki zao.
Aidha alisema kutokuwepo
kwa sheria inayosimamia huduma hizo za kifedha kulisababisha kukosekana kwa
uwazi wa masharti ya mikataba ya mikopo kwa kutopatikana kwa takwimu sahihi za
uendeshaji za watoa huduma hizo
Dkt. Mpango alisema kuwa ili kukabiliana na changamoto
hizo, Serikali ilitunga Sheria ya huduma Ndogo za Fedha ya mwaka 2018 pamoja na
Kanuni zake zilizotungwa mwaka 2019, ambazo lengo lake ni kuhakikisha watumiaji
wa huduma hizo wanalindwa kikamilifu.
‘’Sheria hii inatambua
madaraja manne ya taasisi zinazotoa huduma za fedha ambapo Daraja la Kwanza ni
zile zinazopokea amana, daraja la pili ni taasisi zisizopokea amana, daraja la
tatu linahusu vyama vya Ushirika wa Akiba na Mikopo (SACCOS) na daraja la nne
ni vikundi vya kijamii vya huduma ndogo za fedha”, aliongeza Dkt. Mpango.
Kwa upande wake Mkurugenzi
wa BoT tawi la Kanda ya Kati, Bw. Richard Wambali, ambaye alimwakilisha Gavana
wa Benki hiyo Prof. Florens Luoga, amewataka watoa huduma ndogo za fedha kuisoma
na kuielewa sheria na kanuni zake ili wazitekeleze kwa ufanisi.
Pia amewataka wadau hao
kutumia muda wa miezi 12 iliyotolewa na Sheria kuweka mifumo na taratibu za biashara
kuendana na matakwa ya Sheria na Kanuni ili ifikapo Oktoba 31, 2020, muda mbao
umeainishwa kisheria kuwa ni mwisho wa kutekeleza masharti hayo wawe wamepata
leseni hizo kutoka BoT au kwa mamlaka zilizokasimishwa majukumu hayo.
Aidha amewataka kuzingatia
mazingira na fursa mbalimbali zinazotokana na uwepo wa Sheria na Kanuni
kuongeza kasi ya utoaji huduma kwa wananchi ambao hawajafikiwa na sekta rasmi
ya fedha.
Naye Mkurugenzi wa
Uendeshaji wa Mfuko wa kuendeleza Sekta ya Fedha (FSDT), Bi. Irene Mlola,
alisema kuwa Mfuko huo utaendelea kushirikiana kwa karibu na Wizara ya Fedha na
Mipango kwa kuwa anaamini nafasi ya
huduma za kifedha katika kumkomboa mwananchi kwenye hali ya uchumi na
kumsaidia kimaendeleo katika kupunguza umasikini.
Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb), akizungumza na vyombo vya habari jijini Dodoma wakati wa hafla ya uzinduzi wa Mpango wa Elimu kwa Umma kuhusu Sera, Sheria na Kanuni za Huduma Ndogo za Fedha, Jijini Dodoma.
Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb), akimkabidhi nakala za vitabu Kaimu Kamishna Msaaidizi wa Idara ya Maendeleo ya Sekta ya Fedha wa Wizara ya Fedha na Mipango Bi. Dionisia Mjema, baada ya uzinduzi wa Mpango wa Elimu kwa Umma kuhusu Sera, Sheria na Kanuni za Huduma Ndogo za Fedha, Jijini Dodoma.
Mkurugenzi wa Benki Kuu (BoT), Kanda ya Kati, Bw. Richard Wambali, akizungumza jambo wakati wa hafla ya uzinduzi wa Mpango wa Elimu kwa Umma kuhusu Sera, Sheria na Kanuni za Huduma Ndogo za Fedha, Jijini Dodoma.
Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb) (katikati) na wadau wengine wakiangalia makala kabla ya uzinduzi wa Mpango wa Elimu kwa Umma kuhusu Sera, Sheria na Kanuni za Huduma Ndogo za Fedha, Jijini Dodoma.
Baadhi ya Wakuu wa Idara, Vitengo na Wawakilishi wa Wakuu wa Idara na Vitengo wakisikiliza hotuba ya Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb), (hayupo pichani), wakati wa hafla ya uzinduzi wa Mpango wa Elimu kwa Umma kuhusu Sera, Sheria na Kanuni za Huduma Ndogo za Fedha jijini Dodoma.
Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb), akiwa katika picha ya pamoja na Wawakilishi wa Taasisi mbalimbali baada ya kuwakabidhi nakala za vitabu alivyozindua kuhusu Mpango wa Elimu kwa Umma kuhusu Sera, Sheria na Kanuni za Huduma Ndogo za Fedha jijini Dodoma.
(Picha na Josephine Majura – WFM Dodoma).
No comments:
Post a Comment