Habari za Punde

Misingi ya Utawala Bora Inafuatwa ili Kukuza Uchumi na Kujenga Jamii Yenye Imani na Upendo -Dk.Shein.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein akihutubia wakati wa hafla ya Ufunguzi wa Kongamano la Kitaifa la Utawala Bora na Kuadhimisha Siku ya Maadili na Haki za Binadamu lililofanyika katika Ukumbi wa Sheikh Idriss Abdul Wakil Kikwajuni Jijini Zanzibar leo.16-12-2019.

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar Awamu ya Saba imefanya bidii kubwa kuhakikisha misingi ya utawala bora inafuatwa ili kukuza uchumi na kujenga jamii yenye imani, upendo na mshikamano baina yao, serikali na nchi yao kwa jumla.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein aliyasema hayo leo katika hotuba yake aliyoitoa huko katika ukumbi wa Sheikh Idrisa Abdul Wakili, Kikwajuni mjini Zanzibar katika maadhimisho ya Siku ya Maadili na Haki za Binaadamu.

Katika hotuba hiyo, Rais Dk. Shein aliitaja misingi hiyo kuwa ni ushirikishwaji wa umma, utawala wa sheria, haki na usawa kwa watu wote,uwazi katika kuendesha shughuli za maendeleo pamoja na uwajibikaji katika utendaji na uadilifu.

Rais Dk. Shein alieleza hatua mbali mbali zilizochukuliwa na Serikali kuona kwamba utawala bora unaimarika ikiwa ni pamoja na kupitisha Sera ya Utawala bora ya mwaka 2011, ambayo utekelezaji wake unasaidia katika kuyafikia malengo ya mkataba wa haki za binaadamu na ule wa mapambano dhidi ya rushwa.

Alieleza kuwa Tanzania ni nchi ya mwanzo kuanzisha Wizara ya Utawala Bora katika nchi za Bara la Afrika hatua ambayo imeijengea sifa kubwa ndani na nje ya Afrika.

Alieleza kuwa katika msingi wa ushirikishwaji wa umma, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Nchi,Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Idara Maalum za SMZ imeanisha mfumo wa Ugatuzi kwa kuzingatia umuhimu wa utekelezaji wa Sheria Namba 7 ya mwaka 2014 ili kukasimu baadhi  ya madaraka kwa wananchi.

Kwa madhumuni ya kuzilinda haki za watoto, Rais Dk. Shein alisema kwamba Serikali imewajengea watoto mazingira mazuri ya kutoa ushahidi kwa kuanzisha Mahakama za Watoto katika Mikoa yote mitano ya Zanzibar.

Alisema kwamba kuweko kwa utekelezaji wa haki sawa kwa kila binaadamu na utawala bora wa sheria ni miongoni mwa misingi ya utawala bora kwani mambo matatu haya ambayo ni maadili, haki za binaadamu na Utawala Bora yana uhusiano unaotegemeana.

Alisema kwamba harakati za usimamizi na ulinzi wa haki za binaadamu hapa Zanzibar zilianza zamani kabla ya Mapinduzi matukufu ya Januari 12, 1964 ambapom katika hatua hiyo Rais wa Mwanzo wa Zanzibar, Marehemu Mzee Abeid Amani Karume mara tu baada ya Mapinduzi alipiga marufuku utaratibu wa mikopo ya fedha kwa njia ya kuweka vitu rahani (pawn).

Aliongeza kuwa katika kuhakikisha haki na usawa vinatekelezwa kwa wote, Serikali imeanzisha Tume ya Utumishi Serikalini katika jitihada za kuhakikisha haki za wananchi zinalindwa, utendaji wa kazi unafanywa na vitendo vya unyanyasaji vinaondoka sehemu za kazi.

Kadhalika alisema Serikali imekuwa ikiongeza nafasi za uongozi kwa wanawake na kutolea mfano kuwa katika Baraza la Wawakilishi la mwaka 2015-2020 la hivi sasa idadi ya wajumbe wanawake imefika 32 ikilinganishwa na wajumbe 26 wa Baraza la wawakilishi la mwaka 2010-2015 na lile la 2015-2010 ambalo lilikuwa na wajumbe 20.

Alisema kuwa miongoni mwa wajumbe hao wanawake wapo watano wanaoongoza  Wizara mbali mbali za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na kuwepo kwa nafasi za Makatibu Wakuu, Makatibu Watendaji na Wakurugenzi.

Aidha, alisema kuwa Serikali imeweka chombo chake kikuu ambacho kila mwaka huwa kinafanya uhakiki wa fedha za umma zilizotumika ili kubaini jinsi zilivyotumika kufuatana na sheria zilizowekwa pamoja na mipango ya maendeleo iliyopangwa.

Rais Dk. Shein alieleza kuvutiwa kwake na kauli mbinu ya maadhimisho hayo isemayo “Maadili katika Utumishi wa Umma ni msingi wa Utawala Bora, Haki za Binaadamu na Mapambano dhidi ya Rushwa”, na kupongeza Kauli mbiu hiyo.

Rais Dk. Shein alisema kwamba katika suala zima la uadilifu na uwazi katika kuendesha shughuli za maendeleo na kuzilinda rasilimali za nchi ikiwemo rasilimali fedha na kusisitiza haja kwa viongozi kuwatumikia watu.

Katika hotuba yake hiyo, Rais Dk. Shein aliwasisitiza viongozi kuhakikisha wanawatumikia watu kwani ndio waliowachagua viongozi hao na kuwataka kusimamia wajibu wao sambamba na kufanya kazi kwa ufanisi zaidi. “Utawala Bora si nyimbo bali ni kazi”,alisisitiza Dk. Shein.

Akieleza mafanikio ya Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na Uhujumu Uchumi (ZAECA), alisema kwamba Mamlaka hiyo imefanikiwa kuokoa na kuzirejesha Serikalini jumla ya TZS Milioni 238 ambazo zilitoweka kwa njia ya ubadhurifu kati ya Januari hadi Oktoba mwaka huu 2019.

Rais Dk. Shein alieleza jinsi Serikali  ilivyounda Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma, kwa sheria namba 4 ya mwaka 2015 ambayo ni Taasisi inayojitegemea ambayo ina jukumu la kutekeleza na kusimamia maadili ya viongozi wa umma hapa Zanzibar.

Hivyo, Rais Dk. Shein alitoa wito kwa Taasisi zote za umma, za binafsi, asasi za kiraia na wananchi wote kuziunga mkono jitihada za Serikali katika kushirikiana na Taasisi hiyo ili hatimae mizizi ya rushwa ing’olewe hapa nchini.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kumpongeza Rais Mstaafu wa Awamu ya Sita, Dk. Amani Abeid Karume kwa kumuamini na kumteua kuwa Waziri wa Mwanzo wa Wizara inayohusiana na Utawala Bora katika Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Nae Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma na Utawala Bora Haroun Ali Suleiman alitoa pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa jitihada zake za kuimarisha Utawala Bora akiwa ni muwasisi wa Wizara hiyo.

Katika hafla hiyo pia, Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma na Utawala Bora walimtunuku Rais Dk. Shein, Tunzo ya Heshima kwa kutambua na kuthamini mchango wake mkubwa katika kusimamia na kuwa muanzilishi wa Taasisi ya Utawala Bora.

Akitoa neno la shukurani Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ, alieleza historia ya Taasisi ya Utawala Bora na kusisitiza kwamba jamii yote ina jukumu la kusimamia Utawala Bora

Tumbuizo mbali mbali zilitumbuiza katika maadhimisho hayo, ikiwemo Mchezo wa Kuigiza kutoka kikundi cha JUFE Film Production kinachoongozwa na msanii maarufu Kachara kutoka Kaskazini Pemba pamoja na utenzi maalum wenye mnasaba wa shughuli hiyo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.