Habari za Punde

Uzinduzi wa Skuli Tisa za Sekondari Mpya Zilizojengwa Unguja na Pemba


 
MUONEKANO wa Jengo la Skuli  mpya ya Sekondari ya Rahaleo Wilaya ya Mjini Unguja iliofunguliwa leo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, kwa niaba ya Skuli Tisa za Unguja na Pemba, ikiwax ni shamrashamra za Kusherehekea Miaka 56 ya Mapinduzi ya Zanzibar.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amesema Zanzibar imepata mafanikio makubwa katika sekta ya elimu, kutokana na misingi bora iliyowekwa na muasisi wa Taifa hili, marehemu Abeid Amani Karume.

Dk. Shein amesema hayo katika hafla ya Ufunguzi wa Skuli ya Sekondari ya Mwembeshauri, ikiwa ni shamra shamra za maadhimiisho ya miaka 56 ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Alisema ukombozi uliofanywa na Chama cha ASP chini ya Uongozi thabiti wa marehemu mzee Abeid Amani Karume mwaka 1964, umeweka misingi bora ya upatikanaji wa elimu nchini, na kubainisha kuwa itaondelea kutolewa bure katika awamu zijazo.


Alisema kabla ya Mapinduzi ya 1964, elimu ilitolewa kwa malipo, hivyo watoto wa wazalendo wa Zanzibar, hususan  wanyonge  walishindwa kupata fursa ya kusoma, sambamba na kutolewa kwa misingi ya  ubaguzi kutegemea na kabila  la mtu alikotoka.

Alisema kupitia Ilani ya uchaguzi wa ASP, marehemu Abeid Amani Karume alitangaza elimu kutolewa bure  nchini kote, pale chama hicho kitakaposhinda na kukamata hatamu, jambo ambalo limeeendelea kutekelezwa hadi leo.   

Dk. Shein alisema katika awamu tofauti za Uongozi, Serikali imekuwa ikifanya juhudi kubwa kuendeleza sekta ya elimu kwa kuimarisha miundombinu ya elimu, ikiwemo ujenzi wa skuli hadi kufikia 381 hivi sasa kati yake skuli 284 zikiwa za Sekondari.

Alisema Zanzibar inasifika kwa kuwa na mfumo bora wa utoaji wa elimu katika ukanda wa Mashariki ya Afrika na Bara lote kwa ujumla.

Alisema ujenzi wa Skuli  tisa mpya, utaondoa kabisa tatizo la mlundikano la wanafunzi katika skuli mbali mbali, akitowa mfano wa baadhi ya skuli, walimu watatu kufundisha  darasa moja  kwa wakati mmoja, kutokana na wingi wa wanafunzi.

Aidha, alisema Serikali  inaendelea kufanya juhudi kubwa kuzipatia ufumbuzi changamoto mbali mbali zinazokwaza maendeleo ya elimu nchini, ikiwemo upatikanaji wa vitabu na madawati, akibainisha awamu ya pili ya uagizaji madawati 42,135 kutoka nchini China kwa ajili ya skuli za msingi.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa  Serikali inaendelea kukimarisha Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) kwa kuongeza vitivo na program mbali mbali za masomo ili kuhakikisha Taifa linapata wataalamu wengi kupitia nyanja tofauti.

Alisema Serikali imelipa kipaumbele suala la elimu na kubainisha  katika Bajeti ya mwaka huu wa fedha 2019/2020 Serikali imetenga Shilingi Bilioni 178.9 kwa ajili ya sekta ya elimu nchini.

Aidha, alisema changamoto ya upungufu wa walimu wa Sayansi inafanyiwa kazi ambapo tayari limeanza kupatiwa ufumbuzi kwa msaada wa wahisani mbali mbali.

Katika hatua nyengine, Dk. Shein alipingana na mitazamao ya baadhi ya watu wanaodai elimu imeshuka nchini, akisema haijulikani kipimo gani kilichotumika kuhusisha  ya dhana hiyo, kwa kuzingatia kuwa hivi sasa Zanzibar imekuwa na Vyuo vikuu kadhaa, wakati ambapo zamani havikuwepo.

Alisema weledi wa kuzungumza lugha ya Kiingereza sio kigezo cha kupimwa kiwango cha elimu akibainisha kuwepo nchi kadhaa duniani zilizopiga hatua kubwa za maendeleo ambapo hutumia lugha zao za Taifa katika kufundishia  hadi vyuo vikuu.

Nae, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali, Riziki Pembe Juma alisema ujenzi wa skuli hiyo ya ghorofa mbili una lengo la kuondokana na ufinyu wa nafasi, na kubainisha kuwa  zitatumika na wanafunzi wa skuli mbili na kuondokana na kadhia ya mazingira mabaya yaliopo katika skuli za Darajani na Vikokotoni, ambazo zimezungukwa na shughuli za kibiashara.

Aisema majengo hayo yatawasaidia sana walimu kufundisha katika mazingira mazuri na wanafunzi kupokea vyema kile wanachofundishwa, na hivyo kuwa katika nafasi nzuri zaidi ya kufaulu masomo yao.

Alieleza kuwa Wizara imeweka mikakati kabambe ili kuhakikisha wanafunzi wanaendelea kufanya vyema katika mitihani yao na kueleza kuwa hatua hiyo imeilanza kuleta mafanikio kwa kupunguza kiwango kikubwa cha wanafunzi wanaofeli  (Divisheni zero).

Waziri Pembe alitoa ombi rasmi kwa Rais  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Skuli hiyo ya Mwembeshauri iitwe kwa jina la Dk. Ali Mohamed Shein, lengo likiwa ni kumuenzi kiongozi huyo kwa mchango wake mkubwa katika kuimarisha sekta ya elimu nchini.

Mapema, Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Dk. Idriss Muslih Hijja alisema Skuli mpya ya Mwembeshauri ni miongoni mwa skuli tisa zilizokamilika ujenzi wake Unguja na Pemba.

Alisema ujenzi huo umetekelezwa kwa mashirikiano kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na wahisani Opec Fund for International Developement (OFID), kupitia mradi wa Zanzibar Third Education  Project (ZATEP).

Alieleza kuwa ujenzi wa skuli hizo unaendana na utekelezaji wa Ilani ya CCM, ukiwa umegharimu jumla ya shilingi Bilioni 26.3, kati ya hizo shilingi Bilioni 23.4 ni mkopo kutoka OPEC Fund na shilingi Bilioni 2.9 ni mchango wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Aidha, alisema ujenzi wa skuli ya Mwembeshauri pekee imegharimu zaidi ya shilingi Bilioni 3.5, kati ya hizo shilingi Bilioni 3.2 zimetumika kwa shughuli za ujenzi na zaidi ya shilingi Milioni 361.1 ni gharama za ununuzi wa vifaa mbalimbali, zikiwemo komputa na vifaa vya maabara.

Alisema skuli hiyo ya ghorofa mbili iliyojengwa na Kampuni ya ‘Group Six International Limited’ kutoka China ina uwezo wa kuchukuwa wanafunzi 2,560 kupitia  mikondo miwili  kwa wastani wa wanafunzi 40 kwa darasa.

Katibu Mkuu alisema mradi wa ujenzi wa skuli tisa unalengo la kukuza ubora wa elimu nchini kupitia uimarishaji wa miundombinu na samani na kubainisha hatua hiyo itaongeza nafasi za masomo na kupunguza msongamano wa wanafunzi madarasani.

Alisema kwa ujumla skuli hizo (tisa) zina uwezo wa kuandikisha wanafunzi 11,520, watakaopata fursa ya kusoma kupitia mikondo miwili ya masomo.

Alizitaja skuli nyengine zinzohusika na mradi huo, kuwa ni pamoja na Kinuni, Chumbuni , Bububu na Fuoni kwa Unguja na  Wara, Mwambe, Kizimbani na Micheweni za Kisiwani Pemba, ambazo nazo zimepewa majina mbali mbali ya Viongozi wa Kitaifa.
        
Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 
 E-mail: abdya062@gmail.com

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.