Habari za Punde

Rais Dk Shein Afungua Mradi wa Maji na Usafi wa Mazingira wa Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja Ikiwa Shamrashamra za Miaka 56 ya Mapinduzi ya Zanzibar.


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akiondoa kipazia kuashiria kulizindua Mradi wa Maji Safi na Salama na Usafi wa Mazingira Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja  katika eneo la Saateni Jijini Zanzibar ikiwa ni  shamrashamra za kusherehekea Miaka 56 ya Mapinduzi ya Zanzibar, (kulia kwa Rais) Waziri wa Ardhi Nyumba Maji na  Nishati.Mhe.Salama Aboud Talib na (kushoto kwa Rais) Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi Nyuma Maji na Nishati.Ndg. Ali Halil na Mkurugenzi Mkuu (ZAWA) Ndg. Mussa Ramadhan Haji.

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar inafanya juhudi kubwa katika kuendeleza miradi ya maji safi na salama na si muda mrefu changamoto ya upatikanaji huduma hiyo itakuwa ni historia.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein aliyasema hayo leo katika hotuba yake wakati wa ufunguzi wa Mradi wa Maji na Usafi wa Mazingira wa Mkoa wa Mjini Magharibi (ZUWSP)-ADF 12 huko Saateni Wilaya ya Mjini Unguja ikiwa ni shamrashamra za miaka 56 ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Rais Dk. Shein alisema kuwa Awamu ya Saba imeanza mikakati kabambe ya kuimarisha miradi ya maji na kueleza kuwa Awamu zijazo zitaendeleza mikakati hiyo kwa azma ya kuwapatia wananchi huduma hiyo muhimu hapa nchini.

Rais Dk. Shein alisema kuwa huduma za maji safi na salama kabla ya Mapinduzi ya Januari 12, 1964 zilikuwa zikitolewa kwa ubaguzi licha ya kuwa ni neema aliyoileta MwenyeziMungu kwa waja wake.

Alisema kuwa kwa Zanzibar wakati huo huduma zote muhimu zilianza katika nyumba za mawe zilizokuwepo katika eneo la MjiMkongwe pekee yake.

Rais Dk. Shein alieleza umuhimu wa maji kwa wanaadamu, wanyama na miti na kueleza kuwa ndio maana Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ikafanya juhudi za makusudi kuhakikisha huduma hiyo inaimarika hasa ikizingatiwa kuwa maji hayana mbadala.

Aidha, Rais Dk. Shein alieleza jinsi ya Washirika wa Maendeleo wakiwemo nchi rafiki ikiwemo Ras al Khaimah, Sharja, Japan, China, India  na wengineo walivyoiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha miradi ya maji safi na salama hapa nchini.

Alisema kuwa Zanzibar ina historia kubwa ya upatikanaji wa maji safi na salama kwani historia hiyo inaonesha kuwa zilikuwa zikija meli maalum kuchukua  maji kutoka nje ya nchi kutokana na sifa za maji ya Zanzibar.

Alieleza jinsi ya ongozeko la watu lilivyochangia uhaba wa maji  hapa Zanzibar na kueleza jitihada za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuhakikisha fedha zinapatikana kwa ajili ya kuimarisha miradi ya maji katika eneo la mji wa Zanzibar na hatimae kupatikana kwa kiasi cha USD Milioni 268 kwa ajili ya miradi hiyo.

Alieleza kuwa azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kuhakikisha kiwango cha maji kinaongezeka kwa kiasi kikubwa ili wananchi wapate huduma hiyo ipasavyo na kusisitiza kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Awamu ya Saba imetekeleza malengo ya Mapinduzi sambamba na Utekelezaji wa Ilani ya CCM kwa vitendo.

Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kumpongeza Waziri wa Wizara hiyo kwa kuiongoza Wizara hiyo pamoja na watendaji wengine wote wa Wizara hiyo kwa kushirikiana, “Namie kidogo nimeubwaga moyo katika kufanikisha mradi huu wa maji”alisema Rais Dk. Shein katika hotuba yake hiyo.

Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kueleza historia ya Mapinduzi hapa Zanzibar na jisni jitihada za akusudi zilivyochukuliwa katika kuhakikisha ukoloni unaondoshwa na wananchi wa Zanzibar wanaishi maisha bora na wanaodokana na dhulma iliyokuwepo.

Alieleza kuwa Mapinduzi yaliyofanyika Januari 12, 1964 ni Mapinduzi halali na lengo lake ni kuhakikisha wananchi wanaishi maisha bora ya amani sambamba na furaha na kushirikiana hatua ambayo iliwapelekea nchi kadhaa duniani kuyatambua.

Aliwanasihi wananchi na kueleza kuwa si busara na wala si vizuri wakaunganisha maji katika nyumba zao bila ya kufuata sheria na utaratibu uliowekwa.

Alisisitiza kuwa Zanzibar  maji hayalipiwi bali  yanachangiwa katika kupatikana kwa huduma hiyo na kuwataka wananchi pale Serikali inapoelekeza kuchagia huduma hiyo basi wananchi wasirudi nyuma kwani hatua hiyo itaisaidia (ZAWA) kufikisha na kutengeneza miundombinu ya maji kwani ina lengo na nia nzuri huku akisisitiza haja ya kutunzwa kwa miundombinu hiyo ya maji.

Aliendelea kusisitiza haja ya kuzihifadhi na kuvitunza vyanzo vya maji kwani hivi sasa vimekuwa vikivamiwa kwa kujengwa nyumba katika maeneo hayo likiwemo eneo la Mwanyanya huku akisisitiza umuhimu wa kupandwa miti na kukemea kukatwa miti ovyo.

Pia, Dk. Shein aliitaka (ZAWA)  kuwa na wataalamu wa maji kutokana na kuwepo kwa miundombinu mipya ya maji hivi sasa hivyo, ni lazima wajiandae kuwapa elimu na mafunzo watendaji wake katika vyuo kadhaa vikiwemo vya nje ya nchi vinavyosomesha kada hiyo.

Aliwataka wafanyakazi wa (ZAWA) kutofanya kazi kwa mazoea na kusistiza kuwa ni vyema wakawepo watu wenye utaalamu wa kutosha katika kada hiyo ili kupelekea  ufanikishaji wa utoaji wa uhakika wa maji safi na salama.

Rais Dk. Shein alisisitiza haja ya kuwepo kwa hakiba ya vifaa katika Mamlaka ya (ZAWA) ili kuepuka uhaba wa vifaa pamoja na kuwepo timu kabambe ya kufuatilia matatizo ama uvujaji wa ovyo na si kutegemea taarifa kutoka kwa wananchi.

Alisisitiza haja ya kuwaajiri vijana ili wafanye kazi kwani wako wengi hawana kazi ili lengo la kufanikisha utoaji wa huduma hiyo lifikiwe.

Alitumia fursa hiyo kumpongeza Mkurugenzi wa (ZAWA) na timu yake kwa hatua inazozichukua hasa wakati wa mwezi mtukufu wa Ramadhani kwa kuwapelekea maji wananchi katika mwezi huo mtukufu na kuwataka waendelee na utaratibu huo.

Aliipongeza Serikali ya Japan kwa kusaidia hatua ya mwanzo ya mradi wa maji katika Mkoa wa Mjini, Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) kwa kuendelea kutoa msaada wake ikiwemo pale Serikali inapotaka kukopa, Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China ambao wameanza kusaidia tokea mwaka 1964 pamoja na Serikali ya India.

Mara baada ya kuwasili katika eneo la Saateni, Rais Dk. Shein alipata maelezo juu ya mradi wa maji  kwa tangi la Saateni na tangi la Mnarawambao kutoka kwa Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA) Mussa Ramadhan Haji.

Nae Waziri wa Wizara ya Ardhi, Nyumba, Maji na Nishati Salama Aboud Talib alieleza kuwa hatua hiyo ni lengo na madhumuni ya Rais Dk. Shein katika kuhakikisha anawaletea maendeleo wananchi wake ikiwa ni pamoja na kuwapelekea huduma ya maji safi na salama.

Alisema kuwa jitihada hiyo ni matokeo ya pamoja kwani kumekuwa na mashirikiano mazuri kati ya Wizara na Idara zake husika kwa mashirikiano ya Washauri na Waelekezi wa Ujenzi wa Miradi hiyo pamoja na Mwenyekiti wa Badi ya Wakurugenzi kwa mashirikiano inayotoa katika kuhakikisha kazi hiyo inafanyika.

Alisema kuwa katika majaribio yaliofanyika, imeonesha kwamba tatizo la maji lime kupungua na kupongeza ahadi ya Rais Dk. Shein aliyoitoa kwa wananchi wake juu ya mradi huo na kusifu dhamira na miongozo yake ambayo ndio imekuwa dira.

Alieleza kuwa kwa Afrika Mashariki ni nchi ya mwanzo kujenga matangi ya maji ya aina hiyo na kupongeza jitihada za Rais Dk. Shein kwa kazi hiyo kubwa ya mradi huo  iliyofanyika ya kuhakiisha huduma ya maji inaimarika katika mjiwa Zanzibar.

Aliwapogeza  viongozi waliokuwa wakitoa mashirikiano katika uhakikisha mradi huo unafanikiwa wakiwemo Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Hassan Khatib, Masheha wa Mkoa huo ambao wamefanya kazi kubwa kwa kusimamia miradi hiyo na kupelekea kufanya kazi bila ya bughudha katika kufanikisha mradi huo.

Sambamba na hayo, Waziri huyo alikipongeza Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika kusimamia Ilani ya chama hicho kwa kuweza kusaidia kufanikisha mradi huo ikiwa ni pamoja na ziara mbali mbali walizozifanya wakati wa ujenzi wa mradi huo.
  
Akisoma taarifa ya kitaalamu Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba, Maji na Nishati Ali Halil Mirza aliipongeza Seruiiklai ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi wa Rais Dk. Shein kwa uongozi wake mahiri kwa kuamua kutekeleza Mradi wa Maji na Usafi wa Maziringira wa Mkoa wa Mjaini Magharibi.

Alisema kuwa uwamuzi huo ulikuwa ni wa busara na wa msingi katika kuodosha kero zinazowakabili wananchi, unaokwenda sambamba na utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi wa CCM 2015-2020, Mkatkati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini Zanzibar (MKUZA III), Dira ya Maendeleo ya 2020 na Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDG), katika kuimarisha huduma za maji safi na salama Zanzibar.

Aidha, alisema kuwa mradi huo utawanufaisha wananchi wapatao 283,198 wa Mjini zikiwemo Shehia 27  za Mji   Mkongwe na Ngambo ya zamani ambao umetekelezwa kwa pamoja kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) ulioanza rasmi mwezi Julai 2013 na kukamilika mwezi Disemba 2019.

Shehia hizo ni Shangani, Mkunazini, Kiponda, Malindi, Mchangani, Vikokotoni, Mwembetanga, Kisiwandui, Kikwajuni Bondeni, Kikwajuni Juu, Kisima Majongoo, Mlandege, Mwembeladu, Rahaleo, Mikunguni, Mkele, Mwembeshauri, Shaurimoyo, Mwembe Makumbi, Kwaalamsha, Gulioni, Miembeni, Kilimani, Kwahani, kwaalinato, Makadara na Migombani.

Kwa maelezo ya Katibu Mkuu huyo Mradi huo umesimamiwa na Mshauri Mwelekezi kutoka Kampuni ya Don Consult Ltd na ujenzi wa matangi na ulazaji wa mabomba umefanywa na Mkandarasi kutoka Kampuni ya Stcol Corporation ambapo uchimbaji na ukarabarti wa visima umefanywa na Kampuni ya NSPT  Ltd.

Alisema kuwa mradi huo umejumuisha uchimbaji wa visima 6 vipya vyenye uwezo wa kuzalisha wastani wa lita 150,000 kwa saa kwakila kisima, ukarabati wa visima vikongwe 23, ujenzi wa matangi 2 yenye ujazo wa lita milioni 2 Saateni na milioni 1 Mnarawambao.

Pia, unajumuisha ulazaji wa mabomba yenye urefu wa kilomita 75.7 ambapo kilomita 20.6 ni mabomba ya usafirishaji maji yenye kipenyo kuanzia inchi 12 hadi 24 yaliyolazwa kutoka visimani Bubwisudi hadi Welezo matangini na kutoka visimani Karurikikombe hadi tangi la Mnarawambao.

Mradi huo hadi kukamilika kwake umegharimu jumla ya TZS Bilioni 37.142 ambapo kwa upande wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imetoa TZS Bilioni 3.809  na Benki ya Maendeleo ya Afrika imetoa TZS Bilioni 33.332 ambapo tangi la Saateni limegharimu jumla ya TZS Bilioni 2.937 na kwa upande wa tangi la Mnarawambao limegharimu TZS Milioni 908.536.

Katibu Mkuu huyo alisema kuwa baada  ya kukamilika kwa mradi uzalishaji wa visima 23 vilivyofanyiwa marekebisho umeongezeka kutoka lita Milioni 32.789 hadi kufikia lita milioni 36.755 sawa na ongezeko la asilimia 12.

Alisema kuwa visima vipya 6 kwa sasa vinazalisha lita milioni 22.550 hivyo kufanya jumla ya lita zote hizo kwa siku kuwa ni milioni 59.305 sawa na ongezeko la asilimia 36, uzalishaji ambao unatarajiwa kuwanufaisha wakaazi wapatao 283,000 ambapo kazi hiyo ni endelevu.

Alieleza kuwa Serikali kupitia Wizara ya Ardhi, Nyumba,Maji na Nishati inatarajia  kwamba Mradi huo utaendeshwa na kutunzwa vizuri kwa mshirikiano kati ya Mamlaka ya Maji Zanzibar,Wananchi, Uongozi wa Majimbo na Ofisi za Wakuu wa Wilaya.  

Aliitaja Miradi mengine iliyobuniwa na inayotegemewa kutekelezwa katika kipindi cha karibuni ukiwemo  Mradi wa Uhuishaji wa Mfumo wa Usambazaji maji Zanzibar, Mradi wa Uhuishaji wa Huduma za Usambaji Maji Safi wa Mazingira Miji 26 ya Tanzania ikiwemo Zanzibar na Mradi wa Uimarishaji wa Miundombinu ya Maji Mkoa wa Mjini Magharibi yenye gharama za Dola za Kimarekani 247.

 Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.