Habari za Punde

MAENDELEO YA UBUNIFU WA MJI WA SERIKALIYAJADILIWA

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Waziri Mkuu na Bunge) Bw. Tixon Nzunda akizungumza wakati wa kikao kazi cha makatibu Wakuu na Wataalam wa Ubunifu na Usanifu wa majengo leo Aprili, 20, 2020,  kujadili mpango kabambe wa Ujenzi wa Ofisi za Wizara Awamu ya Pili katika eneo la Mji wa Serikali Mtumba Dodoma, Kikao kimefanyika katika Ukimbi wa Mkutano wa ofisi yake Dodoma, wa kwanza kushoto ni Katibu wa kikosi kazi cha kuratibu zoezi la Serikali kuhamia Dodoma Bw. Meshack Bandawe.
Baadhi ya wajumbe wa kikao cha kujadili mpango kabambe wa Ujenzi wa Ofisi za Wizara Awamu ya Pili katika eneo la Mji wa Serikali Mtumba Dodoma,  wakifuatilia kikao hicho leo tarehe 20, Aprili, 2020 katika Ukumbi wa Mikutano wa ofisi ya Waziri Mkuu, Dodoma.


Ofisi ya Waziri Mkuu inaendelea na zoezi la kuratibu awamu ya pili ya uendelezaji wa mji wa serikali eneo la Mtumba, makao makuu ya nchi jijini Dodoma. Awamu hii ya pili inahusisha Ubunifu na ujenzi wa majengo makubwa ya Ofisi zitakazotumiwa na Wizara za serikali.
Akiongea, leo tarehe 20 Aprili, 2020,  katika kikao cha Kamati ya Makatibu wakuu na Wataalamu wa michoro ya Ubunifu na usanifu , Katibu Mkuu ofisi ya Waziri Mkuu, (Waziri Mkuu na Bunge), Tixon Nzunda, amefafanua kuwa awamu hii ya pili ya mpango huo inajikita katika kuboresha ubunifu na usanifu wa mji wa serikali, ulioko Mtumba, Jijini Dodoma.

Aidha, kufanikiwa kwa  mpango huo ni kutachangiza jiji la  Dodoma kuwa jiji bora na la kisasa linaloendana na mahitaji na mifumo ya majiji bora duniani. Ili kufikia azma hiyo, tayari Timu ya Wataalam  imepitia michoro ya ubunifu na usanifu. Pia Wakala wa majengo Tanzania (TBA), inaendelea kufanya kazi kwa karibu na  Taasisi nyingine zinazohusika na miundo mbinu katika mji wa Serikali kama vile TARURA, DOWASA, TANESCO, ZIMAMOTO, TPDC, TTCL na eGA.

Hivi karibuni , Mwezi Februari mwaka huu, 2020, Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa alizindua Mpango Kabambe wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, ambapo aliwataka wadau mbalimbali kutoa ushirikiano kwa kiwango cha juu katika utekelezaji wa Mpango Kabambe wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa lengo la kulifanya kuwa jiji bora na la kisasa nchini.
Serikali, kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu inaendelea kutekeleza zoezi la kuhamishia shughuli za Serikali Kuu Dodoma. Tangu utekelezaji wa zoezi hilo uanze mwezi Septemba 2016.
Uamuzi wa kuhamishia shughuli za Serikali Dodoma ulifanyika mwaka 1973 ikiwa ni maelekezo ya Chama cha TANU kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa utawala wa awamu ya kwanza chini ya Uongozi wa Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.