Waziri wa Mifugo na
Uvuvi Luhaga Mpina (wa kwanza kushoto)
akimkabidhi Mbunge wa Kyela ambaye pia ni Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na
Michezo Dkt. Harrison Mwakyembe injini ya boti iliyotolewa na Serikali kwa
ajili ya kikundi cha wavuvi cha Kyela mkoani Mbeya wakati wa hafla ya
makabidhiano ya injini hiyo leo jijini Dodoma.
Waziri wa Mifugo na
Uvuvi Luhaga Mpina (wa pili kushoto)
akimkabidhi Mkuu wa wilaya ya Kaliua Abel Yeji Busalama injini ya boti
iliyotolewa na Serikali kwa ajili ya kikundi cha wavuvi wilayani humo wakati wa
hafla ya makabidhiano ya injini hiyo leo jijini Dodoma.
Waziri wa Mifugo na
Uvuvi Luhaga Mpina (wa pili kushoto)
akimkabidhi Mbunge wa Mtwara Vijinini Hawa Ghasia (wa kwanza kulia) moja ya
injini ya boti kati ya mbili zilizotolewa na Serikali kwa ajili ya kikundi cha
Vita Fishing group cha Msanga Mkuu na Kikundi cha Jiwezeshe cha Nanyumbu vya
mkoni Mtwara wakati wa hafla ya makabidhiano ya injini hizo leo jijini Dodoma.
Na Eleuteri Mangi,
WHUSM, Dodoma
Serikali kupitia
Wizara ya Mifugo na Uvuvi imekabidhi injini nane za boti awamu ya pili kwa
wabunge wa majimbo mbalimbali kwa lengo la kuvipatia vikundi vya ushirika vya
uvuvi vilivyopo katika majimbo yao ili kusawaidia kuboresha utendaji kazi wao na
kufanya shughuli za uvuvi wenye tija.
Awali wizara hiyo
ilitoa injini za boti tano na kufanya jumla ya injini zilizotolewa na wizara
hiyo kufikia 13 ambazo jumla zimegharimu kiasi cha Sh. milioni 60.
Akikabidhi injini
hizo za boti leo jijini Dodoma, Waziri wa Mifugo na Uvuvi Luhaga Mpina amesema
kuwa Wizara yake inahimiza vyama vingine vya ushirika viboreshe utendaji wao wa
kazi ili navyo viweze kupata ruzuku ya Serikali.
“Mtakubaliana na mimi
kwamba wavuvi wetu wengi wanatumia zana duni sana na wanashindwa kufanya kazi
zao za uvuvi kutokana na zana duni wanazotumia katika uvuvi na kutokana na zana
zao hizo kuwa duni wanafanya kazi miaka nenda rudi lakini maisha yao
hayabadiliki kutokana wanachopata ni kwa ajili ya chakula tu” alisema Waziri
Mpina.
Ili kujua changamoto
za wavuvi nchini, Wizara ya Mifugo na Uvuvi imefanya tahmini kwa kuzunguka nchi
nzima kujionea wananchi wanavyoendesha shughulizao za uvuvi ikiwemo changamoto
wanazokutana nazo ambapo wamefanikiwa kuwaunganisha wavuvi katika vyama na
vikundi mbalimbali ambavyo vinasaidia kurahisisha utendaji kazi ikiwemo kupata
ruzuku kutoka Serikalini hatua inayowasaidia kufanya shughuli za uvuvi wenye
tija kwa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.
Akitolea mfano wa
vikundi vilivyonufaika na mikopo, Waziri Mpina alisema kuwa Wilaya ya Ukerewe imefanikiwa
kuwa na vikundi vya wavuvi ambao wamenufaika na mikopo ya zaidi ya Sh. milioni
500 na kufanya vyama vya ushirika nchini kufanikiwa kukopeshwa na taasisi za
fedha zaidi ya sh. milioni 800.
Kwa upande wake
Mbunge wa Kyela na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Dkt. Harrison
Mwakyembe amesema kuwa wavuvi nchini wameanza kuchangamkia fursa zinazotolewa
na Serikali ya Awamu ya Tano hatua ambayo itawafanya wawe na mafanikio makubwa
kiuchumi.
Dkt. Mwakyembe
alifafanua kuwa wilaya ya Kyelea ina mito mikubwa ya kudumu mine ikiwemo
Kiwira, Songwe, Lufilio na Mbaka pamoja na ziwa Nyasa, lakini mazao ya samaki
wilayani humo ni duni kutokana na mifaa duni vya uvuvi, hivyo injini ya boti
aliyokabidhiwa itawasaidia wavuvi kuwa na uvuvi ambao utawasaidia kupata samaki
wengi ambao watakidhi mahitaji ya soko.
Amesema injini hiyo
itawasaidia wavuvi kuvua kiutaalamu zaidi na kwa usalama ikizingatiwa ziwa
Nyasa kuna samaki wakubwa aina ya Mbasa ambao ni wakubwa kupita mitumbwi ya
kawaida ambayo inatumiwa na wavuvi hao.
“Nina uhakika
Wanakyela watahamasika kujiunga kwenye vikundi vya ushirika, wakulima hao hao
wa Kyela ni sehemu ya wavuvi, wataunda vikundi imara, tutoke kwenye umasikini,
tuongeze zaidi tija na mbinu za kisasa” alisema Dkt. Mwakyembe.
Aidha, Dkt. Mwakyembe
amemthibitihia Waziri Mpina kuwa injini hiyo itawafikia wananchi na itatunzwa
ili iweze kuwa na manufaa zaidi kwa wananchi wa Kyela.
Naye Katibu Mkuu
Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Sekta ya Uvuvi Dkt. Rashid Tamatama amesema kuwa
wavuvi wadogo wadogo wanachukua asilimia 85 ya wavuvi wote nchini ambapo samaki
wote wanovuliwa ni karibu asilimia 90 wanavuliwa na wavuvi wadogo.
Katika mwaka
2019/2020, Wizara ya Mifugo na Uvuvi imetambua vyama vya ushirika vya wavuvi
vipatavyo 102 katika mikoa yote nchini hatua ambyo imesaidia pia kuhamasisha
kuanzishwa vyama vipya 14 na kufanya jumla ya vyama vya ushirika vinavyotambuliwa
na wizara hiyo kufuikia 116.
Lengo la kuanzishwa
vyama hivyo ni kuwawezesha wavuvi na wakuzaji viumbe maji kuwa na sauti ya
pamoja ili waweze kupata mikopo na masoko ya bidhaa zao.
Vyama vya ushirika
vilivyopata injini hizo za boti ni Magawa, Kisiju, Shungubweni vya mkoa wa
Pwani, Mwamapuri wilaya ya Igunga mkoani Tabora, Mbamba Bay wilaya ya Nyasa
mkoani Ruvuma, kikundi cha wavuvi Kyela mkoani Mbeya, kikundi cha Vita Fishing
group Msanga Mkuu na Kikundi cha Jiwezeshe cha Nanyumbu mkoni Mtwara, Wakulima
wa mwani Kwaigoma wilaya ya Handeni mkoani Tanga, Bukasige Finshing Cooperative
society cha Ukerewe mkoani Mwanza, kikundi cha wavuvi cha Nyamikoma cha Busega
na kikundi cha wavuvi cha Kasanga Kalambo wanaofanya shaghuli zao eneo la ziwa
Tanganyika.
No comments:
Post a Comment