Habari za Punde

Serikali yawakabidhi wavuvi injini za boti kuboresha uvuvi nchini


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Luhaga Mpina  (wa kwanza kushoto) akimkabidhi Mbunge wa Kyela ambaye pia ni Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Dkt. Harrison Mwakyembe injini ya boti iliyotolewa na Serikali kwa ajili ya kikundi cha wavuvi cha Kyela mkoani Mbeya wakati wa hafla ya makabidhiano ya injini hiyo leo jijini Dodoma.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Luhaga Mpina  (wa pili kushoto) akimkabidhi Mkuu wa wilaya ya Kaliua Abel Yeji Busalama injini ya boti iliyotolewa na Serikali kwa ajili ya kikundi cha wavuvi wilayani humo wakati wa hafla ya makabidhiano ya injini hiyo leo jijini Dodoma.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Luhaga Mpina  (wa pili kushoto) akimkabidhi Mbunge wa Mtwara Vijinini Hawa Ghasia (wa kwanza kulia) moja ya injini ya boti kati ya mbili zilizotolewa na Serikali kwa ajili ya kikundi cha Vita Fishing group cha Msanga Mkuu na Kikundi cha Jiwezeshe cha Nanyumbu vya mkoni Mtwara wakati wa hafla ya makabidhiano ya injini hizo leo jijini Dodoma.



Na Eleuteri Mangi, WHUSM, Dodoma
Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imekabidhi injini nane za boti awamu ya pili kwa wabunge wa majimbo mbalimbali kwa lengo la kuvipatia vikundi vya ushirika vya uvuvi vilivyopo katika majimbo yao ili kusawaidia kuboresha utendaji kazi wao na kufanya shughuli za uvuvi wenye tija.

Awali wizara hiyo ilitoa injini za boti tano na kufanya jumla ya injini zilizotolewa na wizara hiyo kufikia 13 ambazo jumla zimegharimu kiasi cha Sh. milioni 60.

Akikabidhi injini hizo za boti leo jijini Dodoma, Waziri wa Mifugo na Uvuvi Luhaga Mpina amesema kuwa Wizara yake inahimiza vyama vingine vya ushirika viboreshe utendaji wao wa kazi ili navyo viweze kupata ruzuku ya Serikali.

“Mtakubaliana na mimi kwamba wavuvi wetu wengi wanatumia zana duni sana na wanashindwa kufanya kazi zao za uvuvi kutokana na zana duni wanazotumia katika uvuvi na kutokana na zana zao hizo kuwa duni wanafanya kazi miaka nenda rudi lakini maisha yao hayabadiliki kutokana wanachopata ni kwa ajili ya chakula tu” alisema Waziri Mpina.

Ili kujua changamoto za wavuvi nchini, Wizara ya Mifugo na Uvuvi imefanya tahmini kwa kuzunguka nchi nzima kujionea wananchi wanavyoendesha shughulizao za uvuvi ikiwemo changamoto wanazokutana nazo ambapo wamefanikiwa kuwaunganisha wavuvi katika vyama na vikundi mbalimbali ambavyo vinasaidia kurahisisha utendaji kazi ikiwemo kupata ruzuku kutoka Serikalini hatua inayowasaidia kufanya shughuli za uvuvi wenye tija kwa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.

Akitolea mfano wa vikundi vilivyonufaika na mikopo, Waziri Mpina alisema kuwa Wilaya ya Ukerewe imefanikiwa kuwa na vikundi vya wavuvi ambao wamenufaika na mikopo ya zaidi ya Sh. milioni 500 na kufanya vyama vya ushirika nchini kufanikiwa kukopeshwa na taasisi za fedha zaidi ya sh. milioni 800.

Kwa upande wake Mbunge wa Kyela na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Dkt. Harrison Mwakyembe amesema kuwa wavuvi nchini wameanza kuchangamkia fursa zinazotolewa na Serikali ya Awamu ya Tano hatua ambayo itawafanya wawe na mafanikio makubwa kiuchumi.

Dkt. Mwakyembe alifafanua kuwa wilaya ya Kyelea ina mito mikubwa ya kudumu mine ikiwemo Kiwira, Songwe, Lufilio na Mbaka pamoja na ziwa Nyasa, lakini mazao ya samaki wilayani humo ni duni kutokana na mifaa duni vya uvuvi, hivyo injini ya boti aliyokabidhiwa itawasaidia wavuvi kuwa na uvuvi ambao utawasaidia kupata samaki wengi ambao watakidhi mahitaji ya soko.

Amesema injini hiyo itawasaidia wavuvi kuvua kiutaalamu zaidi na kwa usalama ikizingatiwa ziwa Nyasa kuna samaki wakubwa aina ya Mbasa ambao ni wakubwa kupita mitumbwi ya kawaida ambayo inatumiwa na wavuvi hao.

“Nina uhakika Wanakyela watahamasika kujiunga kwenye vikundi vya ushirika, wakulima hao hao wa Kyela ni sehemu ya wavuvi, wataunda vikundi imara, tutoke kwenye umasikini, tuongeze zaidi tija na mbinu za kisasa” alisema Dkt. Mwakyembe.

Aidha, Dkt. Mwakyembe amemthibitihia Waziri Mpina kuwa injini hiyo itawafikia wananchi na itatunzwa ili iweze kuwa na manufaa zaidi kwa wananchi wa Kyela.

Naye Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Sekta ya Uvuvi Dkt. Rashid Tamatama amesema kuwa wavuvi wadogo wadogo wanachukua asilimia 85 ya wavuvi wote nchini ambapo samaki wote wanovuliwa ni karibu asilimia 90 wanavuliwa na wavuvi wadogo.

Katika mwaka 2019/2020, Wizara ya Mifugo na Uvuvi imetambua vyama vya ushirika vya wavuvi vipatavyo 102 katika mikoa yote nchini hatua ambyo imesaidia pia kuhamasisha kuanzishwa vyama vipya 14 na kufanya jumla ya vyama vya ushirika vinavyotambuliwa na wizara hiyo kufuikia 116.

Lengo la kuanzishwa vyama hivyo ni kuwawezesha wavuvi na wakuzaji viumbe maji kuwa na sauti ya pamoja ili waweze kupata mikopo na masoko ya bidhaa zao.

Vyama vya ushirika vilivyopata injini hizo za boti ni Magawa, Kisiju, Shungubweni vya mkoa wa Pwani, Mwamapuri wilaya ya Igunga mkoani Tabora, Mbamba Bay wilaya ya Nyasa mkoani Ruvuma, kikundi cha wavuvi Kyela mkoani Mbeya, kikundi cha Vita Fishing group Msanga Mkuu na Kikundi cha Jiwezeshe cha Nanyumbu mkoni Mtwara, Wakulima wa mwani Kwaigoma wilaya ya Handeni mkoani Tanga, Bukasige Finshing Cooperative society cha Ukerewe mkoani Mwanza, kikundi cha wavuvi cha Nyamikoma cha Busega na kikundi cha wavuvi cha Kasanga Kalambo wanaofanya shaghuli zao eneo la ziwa Tanganyika.   

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.