Habari za Punde

WAZIRI MPINA AIPA KIBARUA KIZITO BODI YA TVLA


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina akimkabidhi vitendea kazi Mwenyekiti mpya wa Bodi ya Wakala wa Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA), Profesa Amandus Muhairwa baada ya kuiziduia bodi hiyo na kupokea taarifa ya kutangazwa kwa bei elekezi ya Chanjo Makao Makuu ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi Mtumba jijini Dodoma 
Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina akimkabidhi vitendea kazi Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) baada ya uzinduzi wa Bodi ya TVLA Makao Makuu ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Mtumba jijini Dodoma.




Wajumbe wa Bodi ya Wakala wa Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) wakiwa katika picha ya pamoja na Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina, Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdalah Ullega mara baada ya uzinduzi wa bodi hiyo Makao Makuu ya Wi


zara ya Mifugo na Uvuvi Mtumba jijini Dodoma

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

SERIKALI imetangaza bei elekezi ya chanjo 13 za magonjwa ya mifugo ya kimkakati ambapo sasa wafugaji watapa ahueni kubwa kwa kutumia gharama ndogo kupata chanjo hizo huku Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina akitaka bodi ya Wakala wa Maabara ya Veterinari Tanzania TVLA kuhakikisha Kliniki za mifugo zinajengwa kwenye halmashauri 185 kote nchini ifikapo Juni 2021.


Akitangaza bei elekezi wakati wa uzinduzi wa Bodi ya Wakala wa Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Dodoma, Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo Tanzania, Profesa Hezron Nonga amesema bei hiyo itaanza kutumika leo na kwamba wafugaji na wafanyabiashara wote wanapaswa kufuata bei hiyo iliyotangazwa na Serikali. 
 

Prof. Nonga amezitaja bei elekezi hizo kuwa ni pamoja ya Chanjo ya Homa ya Mapafu ya Ngombe (CBPP) bei ya dukani kwa dozi itauzwa sh. 300 huku bei ya uchanjaji kwa mfugo ikiwa ni sh. 550, Chambavu (Black quarter) dozi dukani shilingi 500 kwa mfugo atachanjiwa sh. 800  

Amesema Kimeta (Anthrax) dozi dukani ni 250 na kwa mfugo itakuwa sh. 500, Mchanganyiko wa Chambavu na Kimeta (TECOBLAX) kwa Ng’ombe dozi dukani sh. 560 na kwa mfugo utachanjwa kwa sh. 800, Mchanganyiko wa Chambavu na Kimeta (TECOBLAX) kwa mbuzi na kondoo dozi kukani sh. 280 kwa mfugo ni sh. 500.


Aidha amesema ugonjwa wa Kutupa Mimba (Brucellosis) dozi dukani ni 1,000 na kwa mfugo ni 1,500, Mdondo (Newcastle disease) dozi ni shilingi 50 na mfugo ni 50, Mapele Ngozi (Lumpy Skin Disease) kwa ng’ombe dozi dukani ni sh. 400 na kwa mfugo ni sh. 600 huku Sotoka ya Mbuzi na Kondoo (PPR) dozi dukani ni sh. 200 na kwa mfugo ni 350. 
 


Pia Homa ya mapafu ya mbuzi (CCPP) dozi dukani ni 200 na mfugo itakuwa ni 350, Ugonjwa wa Miguu na Midomo (FMD) dozi dukani ni sh. 2,500 na kwa mfugo ni 3,000, Kichaa cha Mbwa (Rabies) dozi dukani ni 1,000 kwa mfugaji ni sh. 1,500. 
 


Profesa Nonga ameongeza kuwa ugonjwa wa Ndigana Kali (ECF) dozi dukani ni sh. 10,000 na kwa mfugo ni sh. 17,000
huku Homa ya Bonde la Ufa (RVF) dozi dukani ni sh. 400 huku kwa mfugo ikiwa ni sh. 700. 
 


Akizungumza mara baada ya kuzindua Bodi hiyo ya TVLA, Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina amesema kupitia mabadiliko hayo ya Kanuni za kutoa bei elekezi, Serikali itakuwa imepunguza gharama kwa wafugaji kutoka shilingi bilioni 482.4 walizokuwa wakizutumia kununua chanjo hadi kufikia shilingi bilioni 237 ikiwa ni punguzo la asilimia 51. 
 


Hivyo ameitaka bodi hiyo mpya kufanya kazi usiku na mchana kuwalea wafugaji wa Tanzania kupitia eneo hilo muhimu la chanjo na matibabu ya mifugo na kukuchochea ungezeko la uzalishaji mifugo hali itasaidia kuhudumia viwanda vya mazao ya mifugo vinavyojenga maeneo mbalimbali nchini kwa ajili ya kupeleka kwenye masoko mbalimbali duniani. 
 

Pia ameitaka bodi hiyo kukomesha matumizi ya dawa feki na zilizomaliza muda wake , kurahisisha upatikanaji wa chanjo hatua itakayowezesha kuendelea kupungua kwa magonjwa na kuweza kuongeza masoko na ushindani kimataifa.


Mpina ameigiza bodi hiyo kuhakikisha kuwa ifikapo Juni, 2021 chanjo 7 ambazo ziko katika hatua mbalimbali zizalishwe hapa nchini ili kuwawezesha wafugaji kuzipata kwa urahisi na kwa gharama nafuu. 



Pia Waziri Mpina ameitaka bodi huhakikisha kuwa ujenzi wa Kliniki za mifugo kwa halmashauri zote 185 kote nchini pamoja na mikoa 15 ambayo haina maabara kwa sasa ziwe zimekamilika ifikapo Juni 2021. 



Mwenyekiti wa Bodi ya TVLA, Profesa Amandus Muhairwa amemhakikisha Waziri Mpina kuwa watatumia weledi wao wote kuhakikisha wanatekeleza maagizo yote aliyoyatoa ili kuiwezesha Sekta ya Mifugo kupita hatua kubwa kwa kipindi chote cha uongozi wao. 



Wajumbe wengine wa Bodi hiyo ni Dk. Haruni Mapesa kutoka Chuo Kikuu Mzumbe, Dk. Akida Khea kutoka Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA), Casmir Kyuki kutoka Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania na Selina Lyimo ambaye ni Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu(Mstaafu).

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.