Habari za Punde

Dk. Shein Aipongeza Redio Jamii ya Micheweni Pemba


RADIO Jamii iliyopo Micheweni Pemba imepongezwa kwa mchango wake mkubwa wa kutoa elimu kwa jamii juu ya tahadhari ya ugonjwa unaosababishwa na virusi vya Corona kisiwani humo.

Pongezi hizo zimetolewa wakati viongozi wa Mikoa miwili ya Pemba walipokutana na na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein huko Ikulu ndogo, Chake Chake, Mkoa wa Kusini Pemba.

Akisoma taarifa ya Mkoa wa Kaskazini Pemba, Mkuu wa Mkoa huo Omar Khamis Othman alisema kuwa Redio Jamii iliyopo Micheweni imeweza kutoa vipindi mbali mbali ikiwa ni pamoja na uvaaji wa barakoa, umuhimu wa kunawa maji tiririka na sabuni kama njia ya kujihadhari na ugonjwa huo.

Kiongozi huyo alieleza kuwa jumla ya wananchi 7,689 wananoishi maeneo ya kisiwa cha Fundo, Kokoa, Njau, Kojani, Makangale,Kifundi, Msuka, Micheweni, Shanake na Kiuyu kwa Manda, Tondooni, Tumbe, Shumba Mjini, Maziwa Ngombe, Michenzani, Kiuyu Mbuyuni wamepata elimu ya kuelewa ugonjwa wa Corona na hatua za kujikinga na ugonjwa huo.

Alieleza kuwa redio hiyo imeweza kusaidia jitihada hizo za kutoa elimu katika maeneo hayo yakiwemo yale ya visiwa na maeneo mengineyo ikiwa ni pamoja na kueleza katika vipindi vyake juu ya umuhimu wa kutoa taarifa pale wanapogundua kuna mtu ama watu wameingia kutoka nje ya nchi.

Mkuu wa Mkoa huo alieleza kuwa elimu iliyolenga kuutambua ugonjwa wa Corona na mbinu zote muhimu za kujikinga na ugonjwa huo imetolewa kupitia mikutano ya jamii kwa Shehia 61 za Mkoa wa Kaskazini Pemba.

Aidha, aliongeza kuwa elimu kwa wachuuzi na wanunuzi wa samaki 2,651 ilitolewa katika Shehia nne ambazo zina bandari za kuuzia samaki ikiwemo Msuka, Kiuyu, Shumba Mjini, Wete, Mtambwe, Gando na Tumbe.

Vile vile, Mkuu wa Mkoa huyo alieleza kuwa Mkoa huo umetoa elimu kwa makundi tofauti wakiwemo Maimamu, Mashehe, Watu maarufu, Madalali na Kamati za afya za Shehia kwa Shehia zote 61 za Mkoa wa Kaskazini Pemba ambapo elimu imetolewa juu ya kuelewa ugonjwa wa Corona.

Ambapo pia kiongozi huyo alieleza kuwa hatua muhimu za kujikinga na ugonjwa huo zikiwemo uvaaji wa barakoa, kutekeleza maelekezo ya Serikali pamoja na umhimu wa kutoa taarifa pale wanapogundua kuna mtu ama watu wana dalili za maradhi ya Corona.

Kwa maelezo ya Mkuu wa Mkoa huyo juhudi zimechukuliwa za kufanya ukaguzi na uchunguzi wa wasafiri wanaotoka nje ya Kisiwa cha Pemba sambamba na kufanya usimamizi wa kambi ambazo zilifunguliwa kwa ajili ya kuwaweka wasafiri waloingia nchini kutoka Kenya.

Pamoja na hayo, kiongozi huyo  alieleza hatua zilizochukuliwa katika kufanya ukaguzi wa bandari bubu ambapo Mkoa huo una jumla ya bandari bubu 172 ambazo zinatumiwa  na wananchi kwa shughuli mbali mbali.

Aliongeza kuwa Shehia 17 zenye bandari bubu zilikaguliwa na kufuatiliwa ambapo jumla ya wananchi 725 walipitia bandari zisizo rasmi walipatikana ambapo pia, juhudi zilifanywa za ziara katika maeneo hatarishi yenye mikusanyiko ya watu.

Nae Mkuu wa Mkoa wa Kusini Pemba Hemed Suleiman Abdallah alieleza kuwa Mkoa huo kwa kushirikiana na Wizara ya Habari, Utalii na Mambo ya Kale kupitia Idara ya Habari Maelezo umeweza kutoa taaluma ya kutosha katika maeneo mbali mbali mjini na vijijini kwa kutumia gari la matangazo.

Aliongeza kuwa  kwa kushirikiana na wataalamu wa afya vipindi mbali mbali vimeweza  kutengeneza katika redio za Jamii ikiwemo redio hiyo ya Micheweni pamoja na Redio Istiqama na Redio pamoja na Televisheni ya ZBC.

Aidha, alieleza kuwa mashirikiano makubwa baina ya uongozi wa Kusini Pemba na Mkoa wa Tanga katika kufuatilia wananchi wanaotoka Mombasa ili kujikinga na ugonjwa wa Corona yamefanyika kwa mafanikio  

Mkuu huyo wa Mkoa aliongeza kuwa hali ya upatikanaji wa chakula kwa kipindi hichi cha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani ni nzuri ambapo mahitaji ya vyakula vya msingi ukiwemo mchele, sukari, unga wa sembe na ngano yanaendelea kupatikana madukani na vipo vya kutosha.

Aliongeza kuwa kutokana na uhamasishaji na uimarishaji wa huduma za kilimo wananchi wameweza kuzalisha mazao ya ndizi na muhogo kwa wingi na kwa sasa Mkoa huo tatizo la upatikanaji wa chakula halipo.

Kuhusu bei ya vyakula, Mkuu wa Mkoa huyo alisema kuwa bado haijabadilika na Serikali ya Mkoa inaendelea kufuatilia kwa karibu ili kuhakikisha kwamba bei hazipandi kiholela lwa kisingizio cha mwezi wa Ramadhani ama maradhi ya Corona.

Pamoja na hayo, Mkuu huyo wa Mkoa alieleza kuwa katika utekelezaji wa mikakati ya kupambana na janga la Corona Mkoa huo umeweza kuchukua hatua mbali mbali katika maeneo yote ya mikusanyiko kama vile masoko,maeneo ya biashara, maeneo ya michezo, sehemu za ibada, vituo vya daladala na katika Taasisi za Serikali na binafsi ili kuthibiti ugonjwa huo.

Kwa maelezo ya kiongozi huyo alieleza kuwa Afisi ya Uhamiaji Mkoa wa Kusini Pemba kwa kushirikiana na vikosi vyengine vya Ulinzi na Usalama vya Mkoa wa Kusini kwa kushirikiana na Masheha na Madiwani imefanya doria maalum ya kuzikagua na kuzitambua bandari bubu zote 253 kwa Mkoa wa Kusini.

Sambamba na hayo, viongozi hao walieleza hali ya amani na utulivu iliyopo katika Mikoa yote miwili na kueleza kuwa wananchi wanaendelea kufanya shughuli zao za kijamii na kiuchumi kama kawaida pamoja na kushirikiana na Serikali katika kufanikisha shughuli mbali mbali za kijamiii na kimaendeleo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.