Na.
Immaculate Makilika - MAELEZO
Nianzie wapi kumuelezea
Mzee wa Uwazi na Ukweli? Hebu nianzie kwenye kitabu chake cha Maisha Binafsi ya Rais Mstaafu wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania Benjamin William Mkapa chenye jina la “Maisha Yangu, Dhamira Yangu: Rais wa
Tanzania Akumbuka” alichokizindua hapo Novemba 12, 2019 ambapo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe
Magufuli alikuwa Mgeni Rasmi, Mzee Mkapa anasimulia kuwa maono yake: ni maisha ya
hali ya juu, amani, utulivu na umoja, utawala bora, jamii iliyoelimika na
uchumi shindani wenye uwezo wa kukua kiendelevu na mgawanyo shirikishi wa
kipato.
Ni dhahiri kuwa kifo
cha Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania Benjamin William Mkapa kilichotokea hapo jana Julai 24, 2020 ni pigo
kwa taifa, Afrika pamoja na dunia kufuatia mchango wake ulioakisi mabadiliko ya
uchumi, mahusiano ya kimataifa na mapinduzi katika sekta za umma na binafsi.
Kama
mjuavyo ni katika uongozi wa Mzee Mkapa ambapo mikakati mbalimbali ya
kimaendeleo ilianzishwa, baadhi ni Dira ya Taifa 2025, Mkakati
wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini Tanzania (MKUKUTA), Mpango wa
Kurasimisha Biashara na Mali za Wanyonge
Tanzania (MKURABITA) na Mini Tiger Plan
2020.
Aidha, Rais Mkapa alianzisha Bima ya Taifa, Mageuzi katika
Elimu, na Mradi wa Maji ziwa Victoria, halikadhalika Mpango wa Kunusuru Kaya
Maskini (TASAF), mageuzi haya yalihitaji kiongozi makini mwenye mapenzi kwa
taifa lake lakini aliyeishi na kuamini ndoto zake za kuleta maendeleo kwa
wananchi wake.
Shughuli
za maendeleo na ukuaji wa uchumi
Wakati
wa uongozi wake Mzee Mkapa aliyekuwa Rais, mwandishi wa habari na
mwanadiplomasia nguli aliweza kuleta
mabadiliko makubwa ya kiuchumi, kisiasa, na kijamii, ikiwa ni pamoja na
kuongeza ukusanyaji wa mapato kwa kupitiliza malengo na kukusanya kiasi cha sh.
bilioni 133 kwa mwezi kati ya Julai na Novemba 2004, kulingana na takwimu za Serikali,
kudhibiti mfumuko wa bei kutoka asilimia 30 hadi chini ya 5.5 na kukua kwa uchumi kwa asilimia sita.
Duru
za siasa za ndani na kimataifa
Itakumbukwa
kuwa Mkapa ni Rais wa kwanza nchini Tanzania kuingia madarakani kwa tiketi ya
Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika zama za siasa za vyama vingi mnamo mwaka 1995.
Akiwa
amebakiza takriban miezi kumi tu kumaliza kipindi chake cha kuiongoza Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania, Rais Benjamin William Mkapa aliwahi kukemea tabia ya
watu wanaotishia kuvunja amani katika nchi aliyoipokea kutoka kwa wenzake waliomtangulia ikiwa na
amani na utulivu.
Alionesha
wazi kuwa mfumo wa siasa wa vyama vingi haukuanzishwa nchini ili kudhoofisha
utaifa, umoja na mshikamano kwa taifa.
“Hatukuanzisha
mfumo wa siasa wa vyama vingi ili watu wetu wachukiane, watishane kwa kunoa mapanga
waumizane, wauane au waharibiane mali zao,” alisema Mzee Mkapa.
Hakuna shaka kwamba utawala wa Rais Mkapa ulijaa mambo
mengi mazuri ambayo hayataweza kufutika katika kizazi hiki na mara kadhaa
alihubiri juu ya amani, na
kuheshimu haki za binadamu ikiwemo haki
ya kuishi.
Katika kipindi cha kuelekea Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa
kufanyika Oktoba 28 mwaka huu, ni vyema tukakumbuka aliyowahi kusema Rais Mkapa mwaka 2005 wakati ambapo nchi ilifanya
Uchaguzi Mkuu.
“Tuje tuwaogope sana wanaohubiri chuki kwa kisingizio
cha ushindani wa kisiasa. Ushindani tunaotaka sisi ni wa hoja, wa fikŕa, wa
mikakati na mipango ya maendeleo. Tunashindanisha ilani za uchaguzi wa vyama.
Ningependa vyama vyetu vyote vya kisiasa viwe na malengo makuu yanayofanana
yaani umoja, amani, upendo, maendeleo na ustawi wa taifa na wananchi.
Tunachotofautisha na tunachoshindania kiwe mipango na mikakati ya kufikia
malengo hayo makuu,” alisema Mzee Mkapa.
Aidha, Mzee Mkapa alikuwa
mpatanishi wa mgogoro wa Burundi ambapo alizitaka pande husika katika nchi hiyo
kushikamana na kuheshimu mchakato wa amani na hatua zilizopigwa za kuutafutia
ufumbuzi mgogoro wa kisiasa wa nchi hiyo. Pia, alihusika katika upatanisho wa migogoro ya nchi za Sudani ya Kusini, Congo Mashariki, na Kenya.
Katika hali isiyotarajiwa na wengi ni kwa kiongozi
aliyewahi kuwa Rais kukiri wazi juu ya udhaifu wake, ambapo aliyekuwa Makamu
Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Profesa Rwekaza Mukandala amechambua
wasifu wa Mzee Mkapa katika kitabu chake cha Maisha Yangu, Dhamira Yangu: Rais
wa Tanzania Akumbuka, anaandika, “Mheshimiwa Mkapa anakiri kuwa, kabla
hajawa Rais, hakujua kuwa kazi moja wapo ya Rais ni kutoa pole. Mojawapo ya
mapungufu yangu ni kwamba si mwepesi wa kuonyesha hisia zangu. Mrithi wangu
Rais Kikwete ni mzuri sana katika hili. “Anasema Mheshimiwa Mkapa, ameandika
Profesa Mkandala.
Mwisho kabisa Mzee Mkapa, anamalizia kwa kusema;
Nitamuachia Mungu wangu na nyinyi kuamua ni tofauti gani nimeifanya humu
duniani.
Kama taifa yapo mengi ya kujifunza kutoka kwa Mzee
Mkapa na kumuenzi ni pamoja na kuthamini mchango uliosaidia kuleta maendeleo ya
kijamii, kiasiasa na kiuchumi.
No comments:
Post a Comment