Na.Jonas
Kamaleki
Ni majuzi Mzee wetu
Mpendwa, Benjamin William Mkapa ukiwa Dodoma uliongoza Kikao cha Mkutano Mkuu
Maalum wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa umahiri mkubwa, kumbe ndo ulikuwa
ukituaga! Wengine tulijua kuwa utapiga kura Oktoba na kushiriki katika sherehe
za kumwapisha Rais atakayekuwa amechaguliwa, kumbe sivyo, Mkapa umetutangulia
ghafla kwenda kwa Muumba wetu. Burian Mzee wetu wa Uwazi na Ukweli.
Tutakukumbuka kwa
uongozi wako uliotukuka na unyenyekevu uliokuwa nao kwa kuwaheshimu wakubwa kwa
wadogo tangu ukiwa Pugu Sekondari, Chuo Kikuu Makerere hata ulivyorudi nchini
na kuendelea na majukumu yako kwa uzalendo mkubwa. Kwenye Tasnia ya Habari msiba
huu ni pigo kwani Mzee Mkapa alikuwa Mhariri
mahiri wa The Nationalist hadi Daily News. Waliofanya nawe kazi akiwemo
mwandishi nguli, Jenerali Ulimwengu anasema kuwa kwenye chumba cha habari Mzee
Mkapa alikuwa mwalimu na mlezi.
Mkapa atakumbukwa kwa
kupinga na kupambana na rushwa. Katika kudhihirisha hilo, Mzee Mkapa aliunda
Tume ya Warioba kuchunguza vitendo vya rushwa na kutoa mapendekezo. Hakuishia
hapo kwani aliunda Taasisi ya Kuzuia Rushwa (TAKURU) ambayo baadae ikaja
kujulikana kama Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU).
Wakati Mzee Mkapa
anaingia madarakani alikuta uchumi wa nchi unayumba, hivyo alibuni mbinu kadhaa
za kufufua uchumi. Moja ya mbinu aliyoibuni kiongozi huyo ni kuunda Mamlaka ya
Mapato Tanzania (TRA) kwa ajili ya kubuni vyanzo vya mapato na kukusanya kodi.
Hakuishia hapo bali
alitilia mkazo ujenzi wa miundombinu ya barabara, madaraja na kuboresha usafiri
wa majini. Katika hili alianzisha Wakala wa Barabara nchini (TANROADS). Wakala
ambao ulijenga barabara kwa kiwango cha lami za kuunganisha mikoa yote ya
Tanzania Bara. Kwenye hotuba zake za kila mwezi hakuchoka kujinadi na kazi yake
ya kuboresha miundombinu. Mzee Mkapa alisikika akisema, “Tumeboresha
miundombinu, tumejenga shule za msingi na sekondari”.
Mkapa alifanikisha
kuunda Taasisi za udhibiti, Taasisi na mifuko ya kuinua Wananchi kama Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini
Tanzania (MKUKUTA) na Mpango wa Kurasimisha Biashara na
Mali za Wanyonge Tanzania (MKURABITA).
Jambo jingine ambalo
watanzania wanapaswa kulijua au kulikumbuka ni lile la kumuibua Jemedari Mkuu,
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe
Magufuli alipomteua kuwa Naibu Waziri wa Ujenzi chini Waziri Anna Abdallah
mwaka 1995.
Ukweli na Uwazi ndio
ilikuwa Kaulimbiu maarufu ya Mpendwa wetu Benjamin William Mkapa. Aliamini
kuendesha Serikali yake kwa ukweli na uwazi.
No comments:
Post a Comment