Habari za Punde

Dk. Shein Amewataka WanaCCM na Wananchi Wote Zanzibar Kumchagua Mgombea Urais wa Zanzibar Dk. Hussein Mwinyi.


Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Zanzibar na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein akimtambulisha na kumkabidhi Ilani ya Uchaguzi ya CCM Mgombea Urais wa Zanzibar kwa Tiketi ya CCM Mhe. Dk. Hussein Mwinyi, wakati wa hafla ya Mkutano wa Uzinduzi wa Kampeni uliofanyika katika Uwanja wa Demokrasia Kibanda Maiti Jijini Zanzibar.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi ambaye pia ni Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein amewataka wanaCCM pamoja na wananchi wote wa Zanzibar kumchagua Dk. Hussein Ali Hassan Mwinyi kuwa Rais wa Zanzibar kwani ana sifa zote wa Urais.

Dk. Shein aliyasema hayo leo katika mkutano wa uzinduzi wa Kampeni za Chama Cha Mapinduzi (CCM), uliofanyika katika viwanja vya Kibandamaiti maarufu viwanja vya Demokrasia ambavyo vipo Jijini Zanzibar ndani ya Mkoa wa  Mjini Magharibi na kuhudhuriwa na mamia ya wanaCCM waliofurika katika viwanja hivyo.

Katika maelezo yake, Makamo Mwenyekiti huyo wa CCM Zanzibar alisema kuwa CCM imemchagua Dk. Hussein Mwinyi kuwa mgombea nafasi ya Urais kutokana na sifa zote za kuwa Rais hasa ikizingatiwa kuwa yeye si mwanagenzi wa siasa kwani amewahi kuwa kiongozi katika nyadhifa mbali mbali ndani ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Alisema kuwa kutokana na uwezo alionao Dk. Hussein Mwinyi anauwezo mkubwa wa kuipaisha Zanzibar na kuleta maendeleo hasa pale akiendelea kushirikiana na mgombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli pamoja na Mgombea wake Mwenza Mama Samia Suluhu Hassan na wagombea wengine wote wa chama hicho katika nafasi mbali mbali.

Rais Dk. Shein alieleza sifa mbali mbali za Dk. Hussein Mwinyi ikiwa ni pamoja na kuwa muungwana, mwenye heshima kwa wakubwa na wadogo, asiye na mbwembwe za uongozi na pia ni Daktari aliyebobea katika fani yake.

Aidha, alieleza kuwa Dk. Hussein ni mgombea nafasi ya Urais pekee ambaye atayalinda Mapinduzi ya Januari 12, 1964 pamoja na kuulinda Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ambao umeleta mafanikio makubwa nchini.

Makamo Mwenyekiti huyo alitumia fursa hiyo kumuombea kura Dk. Hussein Mwinyi pamoja na  wagombea wengine wote wa CCM huku akitumia fursa hiyo kuwanadi wagombea Ubunge, Uwakilishi na Udiwani wa CCM wa Mkoa wa Mjini Kichama pamoja na kuwakabidhi Ilani ya chama hicho ili waende wakainadi.

Rais Dk. Shein alisema kuwa mikutano ya Kampeni ya Chama hicho itaendelea katika maeneo mengine mbali mbali katika Mikoa, Wilaya ya Zanzibar ikiwa ni pamoja na kuelekea Kisiwani Pemba.

Nae Mgombea Nafasi ya Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM Dk. Hussein Ali Hassan Mwinyi alieleza mafanikio yaliopatikana katika utekeleza wa Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2015-2020 chini ya uongozi wa Rais Dk. Shein na kuaahidi atayaendeleza katika Ilani ya uchaguzi ya mwaka 2020-2025 aliyokabidhiwa.

Hivyo, Dk. Hussein alieleza haja kwa wanaCCM na wananchi kukichagua chama hicho ili kuendeleza mafanikio hayo huku akieleza azma yake ya kuyaendeleza Mapinduzi pamoja na kuutunza na kuulinda Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

Aidha, alieleza azma yake pamoja na vipaumbele vyake iwapo atachaguliwa kuwa Rais wa Zanzibar ikiwa ni pamoja na kuiimarisha sekta ya uchumi wa bahari (bule economy), hasa uvuvi wa bahari kuu kwa lengo la kuinua ajira kwa vijana sambamba na kuimarisha pato la Taifa.

Pamoja na hayo, Dk. Hussein aliyaeleza mambo mengine atakayoyapa kipaumbele ikiwa ni pamoja na kuiimarisha sekta ya utalii, sekta ya uvuvi, viwanda ufugaji wa samaki, kuwasaidia wavuvi, kuimarisha sekta ya kilimo na sekta nyenginezo.

Dk. Hussein pia, alieleza kuwa atahakikisha katika kuendelea zoezi la upatikanaji wa mafuta na gesi atahakikisha mikataba itakayofungwa inawanufaisha wananchi wa Zanzibar sambamba na kuhakikisha Wazanzibari wanapata fursa kubwa ya ajira katika sekta hiyo.

Alieleza kuwa katika kuhakikisha uchumi unaimarika ni lazima miundombinu ya barabara, bandari na uwanja wa ndege yote hiyo inaimarisha pamoja na kuhakikisha vinapatikana vyanzo vipya vya umeme kazi ambayo ataiendeleza kwa lengo la kukuza uchumi na maendeleo ya Zanzibar.

Sambamba na hayo alieleza azma yake ya kuimarisha huduma za jamii zikiwemo elimu bora bila ya malipo hadi Sekondari, kuongeza ufaulu kwa wanafunzi na kupitia upya mitaala ya elimu ikiwemo elimu ya ufundi ili vijana waweze kujiajiri wenyewe, kuongeza udahili, fedha kwa wanafunzi vyuoni huduma za afya kuanzia msingi hadi Rufaa, kukuza bajeti ya afya, maji safi na salama.

Sekta ya kilimo, kikiwemo kilimo cha biashara na chakula vyote ataviimarisha  sambamba na kuviendeleza na kuanzisha viwanda vikiwemo vya kusindika.

Pia, alitoa pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa kusimamia amani na utulivu huku akiahidi na  yeye kwa upande wake iwapo atachaguliwa kuwa Rais wa Zanzibar ataiendeleza kwani anatambua umuhimu wake kwa maendeleo ya jamii na taifa kwa jumla.

Dk. Hussein aligusia suala zima la utawala bora katika kukuza uchumi na kusisitiza suala zima la uwajibikaji na kueleza kuwa hatowavumilia wale wote waliokuwa hawawajibiki na kuhakikisha kwamba watu hawatofanya kazi kwa mazoea.

Mapema Naibu Katibu wa CCM Zanzibar Abdalla Juma Mabodi alieleza kuwa Dk. Hussein Mwinyi ana uwezo mkubwa wa kuuinua na kuuendeleza uchumi wa Zanzibar.

Aidha, alieleza kuwa uwezo alionao Dk. Hussein Mwinyi katika kusimamia amani na utulivu pamoja na Muungano ni mkubwa sana hasa ikizingatia historia yake ya uongozi wake ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mkutano huo ulikwenda sambamba na burudani kutoka kwa wasanii mbali mbali wa ndani ya nje ya Zanzibar wakiongozwa na msanii nguli Bongo Flava Ali Kiba pamoja na mwana dada anaeinukia katika miondoko hiyo Zuhura Othman Soud (Zuchu) wakiungana na wasanii wa Bongo Movie na makundi mengine kadhaa ya wasanii.

Viongozi mbali mbali wa CCM walihudhuria akiwemo Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muunganow a Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassan, Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd pamoja na viongozi wengine wastaafu akiawemo Rais Mstaafu Ali Hassan Mwiny, Rais Mstaafu wa Zanzibar Dk. Amani Abeid Karume, Makamo wa Rais Mstaafu Dk. Mohamed Kharib Bilali na viongozi wengine wa CCM kutoka Tanzania Bara.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.