Habari za Punde

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO ATOA MAAGIZO MAZITO BASATA, BODI YA FILAMU NA COSOTA


 Sheria na Kanuni iliyopo inayotaka BASATA, BODI ya FILAMU kujiridhisha kwa njia ya kufanya uhakiki imelenga kusimamia maudhui ya sanaa hizi yasiende kinyume na mila, desturi na utamaduni wetu.

Hata hivyo, ninawaelekeza BASATA, BODI ya FILAMU na COSOTA kufanya uhakiki kwa utaratibu ambao haukwamishi kazi za wasanii wetu.

Uhakiki unakusudia kulinda maadili hasa ya watoto kwa kuhakikisha maudhui mabaya hayawafikii. Kwa upande wa filamu, uhakiki unasaidia kujua maudhui yaliyopo kwenye filamu husika ili kuamua ipangiwe daraja gani. Uhakiki pia unasaidia kuepusha maudhui mabaya ya kuharibu maadili ya jamii yetu yadhibitiwe kabla ya kufika kwa mtazamaji/msikilizaji hasa watoto wetu.

Ili kusimamia vyema malengo niliyoyataja ya kulinda maadili ya jamii yetu bila kuathiri ubunifu wa wasanii wetu, maendeleo ya sanaa nchini, na kudumaza ukuaji wa ajira; Wizara inafanya uchambuzi ili kuona kama kuunganishwa kwa BASATA na BODI ya FILAMU kunaleta tija, weledi na ufanisi katika kuhudumia wadau na kusaidia ukuaji wa tasnia. Hili linaenda sambamba na kupitia sera, sheria na kanuni mbalimbali zinazosimamia tasnia na taasisi hizi.

Wizara imeishapata baadhi ya maoni ya wadau na ninatoa wito kwa wadau ambao hawajaleta maoni yao kufanya hivyo.

Hali kadhalika, Kama Waziri mwenye dhamana, pamoja na Wenzangu Wizarani tutaendelea kukutana na wadau ikiwa ni sehemu ya namna ya kuboresha chambuzi na hoja zilizowasilishwa.

Kwa pamoja tushirikiane kujenga tasnia ya habari, sanaa, michezo na urithi wa utamaduni wetu ili kuendelea kuwa na Taifa Imara

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.