RAIS wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi, amezindua kitabu
cha “The Asian Aspiration – Why and How
Africa should Emulate Asia” na kuwapongeza
watunzi wa kitabu hicho, huku akibainisha
kuwa uamuzi wa kukizindua kitabu hicho hapa Zanzibar ni sahihi.
Hafla ya uzinduzi wa kitabu hicho umefanyika katika Hoteli ya Verde Mtoni Jijini Zanzibar, na kuhudhuriwa na watunzi wa kitabu hicho Rais Mstaafu wa Nigeria Olusegun Obasanjo, Waziri Mkuu Mstaafu wa Ethiopia Hailemariam Desalegn, Mchumi Emily Van der Merwe na Mkurugenzi wa Johannesburg based Brenthurst Foundation.
Kitabu cha “The Asian Aspiration – Why and How Africa should Emulate Asia” kimebeba maudhui juu ya mambo yaliofanywa na Nchi za Asia na kupelekea kupiga hatua kubwa za maendeleo ya haraka ya Kiuchumi na kisiasa, hatua ambazo nchi za Afrika zinapaswa kuiga ili kupata mafanikio.
Akizungumza na washiriki wa hafla hiyo Dk. Mwinyi aliwapongeza watunzi wa kitabu hicho ambapo miongoni mwao ni wanasiasa na viongozi wabobezi katika masuala ya sera, uchumi na siasa .
Alisema kuna mambo mengi ya kujifunza kutoka katika kitabu hicho, yanayoonyesha kwa kiasi gani Mataifa ya Bara la Asia yalivyoweza kupambana hadi kutatua changamoto mbali mbali za maendeleo zilizokuwa zikiyakabili na hatimae kupata mafanikio makubwa ya kupigiwa mfano.
Alisema kitabu hicho kinafunza kwa kiasi gani nchi za Bara la Asia lilivyoweza kiujikwamua kutoka hali ngumu ya kiuchumi na kufikia mafanikio yanayoonekana leo.
Alitoa mfano wa mafanikio ya nchi hizo, alisema Vietnam iliweza kujikomboa kutoka hali duni ya kiuchumi mnamo mwanzoni mwa miaka ya 1980 na kupata maendeleo ya haraka kupitia sekta mbali mbali hadi Taifa hilo likaweza kujinasua kutoka Taifa la kipato cha chini na kuwa Taifa lenye uchumi mkubwa unaolingana na nchi zenye kipato cha juu.
Aidha, alitoa mfano wa Taifa la Japan ambalo lililofanikiwa kujikwamua baada ya uchumi wake kuharibika kutokana na Vita vya Pili vya Dunia, kufuatia hatua yake ya kuweka mkazo katika sekta binafsi, elimu na ubunifu, hususan katika masuala ya Teknolojia pamoja na utafutaji wa mitaji kwa njia mbali mbali.
“Leo hii Japan imejikita katika sekta ya utengenezaji wa magari, yakiwamo kampuni ya Toyota, mzalishaji wa magari ambapo Zanzibar ni watumiaji wakuu”, alisema.
Dk. Mwinyi alisema suala la umoja katika kutafuta maendeleo ni la msingi na linaweza kuinufaisha jamii, na akatoa mfano wa Taifa la Singapore lililoweza kupata mafanikio makubwa kutokana na msingi huo.
Alisema Taifa hilo chini ya miongozo sahihi ya mwanzilishi wake Lee Kuan Yew’s aliefariki akiwa na umri wa miaka 91, limeweza kupiga hatua za haraka hadi kufikia kuwa taifa lililoendelea.
Rais Dk. Mwinyi alisitiza haja ya Viongozi wa Afrika katika ngazi mbali mbali pamoja na wale wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupata nakala ya Kitabu hicho na kukisoma ili hatimae waweze kuitumia taaluma iliomo ndani yake kwa maslahi ya Taifa.
Alitoa shukurani kwa watunzi wa kitabu hicho kwa kuja na wazo la kukitunga, kwa msingi kuwa kimesheheni mambo mengi ya kujifunza kwa Wachumi, watunga sera, watafiti pamoja na wapenzi wa kusoma vitabu vyenye maudhui mbali mbali.
Sambamba na hayo , aliwashukuru watunzi hao kwa kuichagua Zanzibar kuwa mahala pa uzinduzi wa kitabu hicho na kubainisha kuwa ni mahala sahihi.
Mapema, Rais Mstaafu wa Nigeria Olusegun Obasanjo, alimshukuru Rais wa Zanzibar na Mwenyektii wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi kwa kuhakikisha uzinduzi huo unafanyika kwa mafanikio.
Katika hotuba yake, Obasanjo alitoa muhtasari wa maudhui ya kitabu hicho na kubainisha jinsi alivyotumia uzoefu wake wa uongozi wa kuliongoza Taifa la Nigeria, kama kichocheo kilichofanikisha utunzi wa kitabu hicho..
Alizitaka nchi za Afrika kubaini maeneo yenye mapungufu na kuweka kipaumbele katika kuyafanyia kazi.
Alisema itakuwa vigumu kupata maendeleo bila ya kutatua matatizo halisi yanayokwamisha maendeleo hayo.
Aidha, alizitaka nchi za Afrika kuweka kipaumbele katika sekta ya elimu ,kwa kuelewa kuwa ndio msingi wa maendeleo.
Alisisitiza umuhimu wa viongozi kukisoma kitabu hicho na kuitumia kikamilifu elimu na maarifa watakayoyapata.
Nae, Waziri Mkuu Mstaafu wa Ethiopia,
Hailemariam Desalegn alibainisha kufanyika utafiti wa kutosha katika nchi mbali
mbali Barani Asia wakati wa utunzi wa
kitabu hicho, sambamba na kukusanya uzoefu na taaluma walizonazo watunzi
kuhusiana na sera za kisiasa na kiuchumi
katika nchi za Afrika hadi kukamilisha kazi
hiyo.
Akizungumza na washiriki wa hafla hiyo, Desalegn alielezea masuala mbali mbali ya kisiasa na kiuchumi yanayoihusu nchi aliiyoingoza (Ethiopia) wakati alipokuwa Waziri Mkuu na kuhimiza suala la ubunifu na kujiamini kwa Viongozi wa Afrika ili kutekeleza na kutimiza malengo ya Mataifa wanayoyaongoza ili kufikia matarajio ya wananachi.
Aidha, aliwapongeza wachapishaji wa kitabu hicho Hurst Publishers kwa kufanikisha kazi hiyo muhimu.
Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822
E-mail: abdya062@gmail.com.
No comments:
Post a Comment