Habari za Punde

Dhamira ya Kukiweka Kisiwa cha Pemba Kuwa Eneo la Uwekezaji Linaanza Kufikiwa Kujengwa Viwanda Viwili Ndani ya Mwaka Mmoja.

 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akihutubia katika hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi la kiwanda cha maji cha Watercom kinachojengwa Kijiji cha Kinyikani Mchangamdogo Mkoa wa Kaskazini Pemba, ikiwa ni shamra shamra za kusherehekea Miaka 58 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi amesema dhamira ya kukifanya kisiwa cha Pemba kuwa eneo la uwekezaji linaanza kufikiwa kwa kuwepo viwanda viwili vikubwa ndani ya mwaka mmoja wa Uongozi wake.

Alieleza kuwa amefarajika kuona kumejitokeza wawekezaji wa ndani kuekeza Kisiwani humo na wananchi kuonesha utayari wao kwa kushirikiana na wawekezaji hao ili kuona wanapata maendeleo katika maeneo yao.

Dk. Mwinyi aliyasema hayo huko katika kijiji cha Kinyikani Mchangamdogo, Wilaya ya Wete, wakati akihutubia wananchi mara baada ya kuweka jiwe la msingi la kiwanda cha maji  safi cha Watercom(T) LTD, ikiwa ni miongoni mwa shamra shamra za miaka 58 ya Mapinduzi Zanzibar.

Aliwataka wananchi wa maeneo hayo yaliojengwa kiwanda hicho kuendelea kutowa mashirikiano kwa Wawekezaji wakati Viwanda hivyo vikianza uzalishaji kwani kufanya hivyo kutaendelea kumpa moyo na kuona kuwa amekuja kuwekeza sehemu sahihi.

“Ni dhamira ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuona kuwa kisiwa cha Pemba kimekuwa eneo maalumu la uwekezaji na imepiga hatuwa katika maendeleo ya viwanda na kiuchumi kwa kuweka mikakati maalumu ambayo kila muwekezaji itamvutia na kuwa na hamu ya kuekeza katika kisiwa hichi,”alisema.

Alifahamisha kuwa Serikali  pamoja na kuimarisha mazingira mazuri ya uwekezaji imeweka vivutio maalumu ya kukifanya kisiwa cha Pemba kuwa eneo la kimkakati la uwekezaji .

Rais Dk. Mwinyi aliwatowa hofu Wawekezaji kwamba Pemba iko salama  na eneo zuri na linawavutia wawekezaji  na anawahamasisha watu wenye nia ya uwekezaji kuelewa kwamba Pemba kuna fursa ya uwekezaji ambazo hazijafanyiwa kazi hususan katika uchumi wa Bahari.

Alisema kuwa uchumi wa bahari ndio muelekeo na Sera ya Serikali ya awamu ya nane, ambapo kauli mbiu ya maadhimisho ya miaka 58 ya Mapinduzi Zanzibar  ni Uchumi wa Buluu kwa maendeleo endelevu.

“Nawakaribisha wawekezaji wote kuekeza katika eneo hili ambalo linajumuisha miradi inayohusiana na utalii, uvuvi na mazao mengine ya baharini kama vile Mwani , bandari na shuhuli za mafuta na gesi asilia,”alieleza.

Alifahamisha kuwa Serikali imekwisha andaa na kuongeza jitihada za kuwavutia wawekezaji wa ndani na nje na kuona namna bora za kuwaondolea urasimu na kuhakisha wanashuhulikiwa kwa haraka katika kuhakikisha wanakamilisha taratibu za uwekezaji  kwamuda mfupi sana.

Alisema Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imeiimarisha Mamlaka ya ZIPA kwa kuanzisha kituo cha pamoja cha kutowa huduma (onestop center) kwa masuala yote muhimu yanayohitajika kwa muwekezaji ili kumuondolea usumbufu.

Dk. Mwinyi alieleza hatuwa hiyo itamuwezesha Muwekezaji aliekwisha kamilisha masharti kupata kibali cha uwekezaji sio zaidi ya siku tatu tu.

Alifahamisha kusikia kwamba kiwanda hicho kitakapoanza uzalishaji kitachangia ajira zaidi ya 550 zitakazotokana na mnyororo wa thamani katika uzalishaji wa maji hatua ambayo itaendana na dhamira ya kutoa ajira laki tatu.

 “Ni matumaini ya Serikali kuwa tunaweza  kulifikia lengo hilo kwa kutokana na  mipango mizuri tulioiandaa na ile tulioanza kuitekeleza ni wazi fursa hizo zitatowa mchango pia katika kuongeza kipato cha mtu mmoja mmoja na kuchangia sana kunyanyuwa uchumi wa taifa kwa ujumla,”alieleza.

Aliwataka wananchi kuelewa kwamba sekta ya viwanda ni chachu ya mafanikio kwa maendeleo ya kiuchumi katika nchi mbali mbali duniani, kwani nchi nyingi zilizoendelea na zile zinazoendelea kwa kasi zimekuwa zikifanya jitihada mbali mbali katika kuhakisha zinawekeza kwenye sekta ya viwanda na hivyo Serikali imeamuwa kuweka maeneo maalumu ya viwanda yakiwemo maeneo ya Dunga na Nungwi kwa Unguja na Chamanangwe kwa upande wa Pemba.

Alisema lengo la kuwepo maeneo hayo ni kuimarisha sekta ya viwanda ambayo itafunguwa fursa mbali mbali ikiwemo kupatikana ajira kwa wananchi , kuchangia pato la Taifa  kupitia kodi na tozo  mbali mbali , kupunguza utegemezi wa bidhaa kutoka nje na kutowa soko zuri la bidhaa za kilimo , uvuvi na ufugaji.

Alifahamisha kuwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar inaendelea na jitihada za kuleta maendeleo ya Viwanda nchini, ikiwemo kujenga kiwanda cha Mwani katika eneo la Chamanangwe ambapo tayari kupitia mfuko wa Uviko 19 imetenga jumla ya fedha TZS Bilioni 2.5 ambazo zitapatiwa mkopo Kampuni ya mwani Zanzibar ili kuhakikisha ujenzi wa kiwanda hicho inaanza na kukamilika ndani ya mwaka huu 2022.

Alieleza mara kiwanda hicho kitakapo kamilika na kuanza kazi kitatowa ufumbuzi wa changamoto wa  bei ya mwani  kuongeza thamani ya zao hilo na bidhaa zake na kila mwenye nia ya uwekezaji Serikali atawapatiwa kila aina ya msaada  anaohitaji ili kuhakikisha mazingira ya uwekezaji yanaimarika Zanzibar na mchango wa sekta ya Viwanda unaongezeka.

Aliwataka vijana wa kisasa kutafsiri  Mapinduzi ya mwaka 1964, kwa vitendo kwa kuchangamkia fursa za kiuchumi na kuleta maendeleo ya nchi yao.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Mwinyi aliahidi kutekeleza ombi la wananchi wa eneo hilo la kutiliwa lami barabara yao inatoka Mzambauni kupitia Kinyikani hadi Mchangamdogo.

Waziri wa Biashara na Maendeleo ya Viwanda Zanzibar, Omar Said Shaaban, alisema uwepo wa viwanda vya vinywaji vitakuwa mkombozi mkubwa wa kisiwa cha Pemba na wananchi wake kwa kupata ajira.

“Maji ni muhimu sana mwekezaji vizuri kupeleka maji hayo nje ya Tanzania, kwa lengo la kuyatangaza maji ya Pemba katika baadhi ya nchi ikiwemo Kenya,”alisema.

Aidha, alimshukuru mwekezaji huyo mzalendo kwa jihudi zake za kuekeza ndani ya kisiwa cha Pemba, kupitia vinywaji mbali mbali nchini, huku akimpongeza Rais Dk. Mwinyi kwamba ndani ya uongozi wake tayari viwanda viwili vimeshajengwa ndani ya kisiwa hicho.

Aidha, alisema Wizara ya Biashara bado inaendelea kuwa na imani na uongozi wake wa awamu ya nane, katika mikakati ya kukitangaza kisiwa cha Pemba kuwa ni eneo la uwekezaji.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Pemba Salama Mbarouk Khatib, alisema kumalizika kwa miradi hiyo itatoa faida kubwa kwa vijana wa Kisiwa cha Pemba, hususan wazawa na wataalamu kunufaika na ajira ya moja kwa moja na ile isiyo ya moja kwa moja.

Akitoa salamu za wananchi wa Jimbo la Kojani Mbunge wa Jimbo la Kojani, ambaye pia, ni Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Hamad Hassan Chande alimshukuru mwenkezaji huyo kwa kuekeza kiwanda chake katika Jimbo la Kojani, kwani asilimia 75 ya ajira wanufaika wa kwanza ni wananchi wa Jimbo hilo.

Aidha, aliwataka wananchi kutambua kuwa tayari mwekezaji mwengine kutoka kampuni ya Alhasab yupo njiani kuekeza katika meneo hayo, kujenga kiwanda cha Juisi kitakachotoa fursa kwa wananchi kuuza bidhaa zao moja kwa moja katika kiwanda hicho zikiwemo embe.

Mwakilishi wa Jimbo la Kojani Hassan Hamad Omar, alisema wananchi wa Jimbo la Kojani na Pemba nzima, bado wanaendelea kuwa na imani na Serikali inayoongozwa na Rais Dk. Mwinyi, kutokana na mikakati mbali mbali aliyoiweka ikiwemo katika eneo la uwekezaji na uchumi wa buluu.

Akitoa taarifa ya kitaalamu Katibu Mkuu Wizara ya Biashara na Maendeleo ya Viwanda Zanzibar, Dk. Islam Seif Salim alisema mradi huo wa kiwanda cha maji ulianza Oktoba 2 mwaka 2021, kufuatia maelekezo yake na Mamlaka ya ZIPA kuhamasika kuhimiza wawekezaji na kuondosha urasimu katika eneo la kimkakati la kisiwa cha Pemba.

Alifahamisha kuwa mradi huo hadi kukamilika kwake utagharimu TZS Bilioni 1.2, kiwanda kikijumuisha maeneo mbali mbali pamoja na kisima cha kuzalisha lita 30 elfu za maji kwa saa, huku kikitarajiwa kuanza kuzalisha maji mnamo mwezi Machi, 2022.

Katibu huyo alisema uwezo wa kiwanda ni kuzalisha maji lita 72 elfu kwa masaa 12 au lita  laki moja na 44 kwa siku, huku bidhaa zitakazozalishwa ni maji, soda, askirim, na kuuzwa katika masoko mbali mbali ya Tanzania bara na nje ya Tanzania.

Alisema sekta ya Viwanda imekua ni chachu ya maendeleo ya kiuchumi kwa nchi nyingi duniani, Zanzibar uwepo wa vianda vya kati vinaweza kutoa ajira kwa wasiopungua 230 na viwanda vikubwa vimeweza kutoa ajira 10417 2019 hadi 11601 2020.

Naye mwakilishi kutoka kampuni ya Watercom (T) Aboubakar Ali Faraji, alisema uwepo wakiwanda hicho ni kuunga mkono Uchumi wa buluu na juhudi katika kukipa kisiwa cha Pemba maendeleo.

Alisema kukamilika kwake kitatoa ajira za moja kwa moja 50 na zisizo za moja kwa moja 500, na kuzalisha maji 72000 kwa saa.

Katika hafla hiyo burudani mbali mbali zilitumbuiza ikiwa ni pamoja na burudani ya vijana kutoka Micheweni.

Imetayarishwa na Kitengo cha Habari

Ikulu Zanzibar.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.