Habari za Punde

“Lala na Ufooo Profesa Ngowi - Buriani Profesa Ngowi”

 


Na.Adeladius Makwega-DODOMA

Asubuhi ya Mchi 28, 2022 taarifa zilitapakaa juu ya ajali mbaya ya gari ndogo kuangukiwa na kontena ambalo lililobebwa na lori huko Mlandizi mkoa wa Pwani. Ikigharimu maisha ya watu wawili Profesa Honest Prosper Ngowi na dereva wake.

Jambo hilo lilinistua kwa kuwa Profesa Ngowi ni mwalimu wangu wa Chuo Kikuu kwa ngazi ya Shahada ya Uzamili huku Chuo Kkuu cha Tumaini Iringa.miaka 14 iliyopita, huku akifundisha pia Chuo Kikuu cha Mzumbe na vyuo vingine vingi ndani ya taifa letu na nje ya Tanzania.

Taarifa ya ajali hiyo binafsi imenihudhunisha si kwa Profesa Ngowi tu kufariki kwake bali pia namna Watanzania wengine watakavyokosa UJUZI, UMAHIRI na UUNGWANA wa mwalimu huyu akiwa katika madarasa ya vyuo vikuu kadhaa akisomesha kozi mbalimbali zikiwamo za uchumi kwa waliobahatika kusomeshwa naye.

Haiba yake ilikuwa ya mtu wa kawaida mno, kwa kupenda mashati ya mikono mifupi huku akichomekea suruali za kawaida kabisa. Uvaaji huu ulinifanya mara ya kwanza kudhani kuwa yeye ni mwanafunzi mwenzetu, lakini hilo lilibadilika kabisa wakati alipoanza kutufundisha.

Hayo ni ya mwaka 2008 huku Tumaini University Iringa Univesirty College ambapo alifundisha kozi ya Decision Making Tools ambayo inahusika na kufanya maamuzi ya mambo kwa viongozi wanaongoza taasisi.

Somo hilo lilikuwa na mahesabu, alafu unachora michoro na ile michoro namna ilivyo ndiyo inayokusaidia kufanya maamuzi juu ya jambo hilo huku ukiambatanisha na maamuzi hayo.

Nakumbuka somo hilo japokuwa lilikuwa linahusisha hesabu na michoro katika uchumi katika darasa letu lililokuwa na wanafunzi zaidi 90 vijana wadogo na watu wazima, hakuna aliyefeli somo hilo, si kwa kuwa lilikuwa jepesi la hasha bali kutokana na Dkt Ngowi (wakati huo ) namna alivyoweza kufundisha vizuri kwa uhodari mkubwa.

Darasa hilo lilikusanya wanafunzi kutoka kada tofauti wakiwamo wanasheria, wanahabari ,Wachumi, Maafisa Utumishi, Watumishi wa Benki, Wafanyabiashara, Wahasibu na kada kadhaa sote kwa pamoja tulifanya vizuri somo hilo narudia kusem hilo.

Kwa watu wengi ambao hawajafanya kazi ya ualimu watambue kuwa jukumu la mwalimu unapokabidhiwa kusomesha wanafunzi, kazi yako ni kuhakikisha wanafunzi wako unawatengenezea mazingira wafaulu somo hilo, kwa kufundisha kutoka jambo wanalolifahamu kwenda kwa jambo jipya. Hilo Prosea Ngowi alikuwa MAHIRI.

Wahadhiri wengi wa vyuo vikuu huwa wanaoujuzi wa masomo wanayofundisha, shida kubwa ni mbinu bora za ufundishaji ili mwanafunzi aweze kuelewa na kupenda kile kinachofundishwa. Hapa Profesa Ngowi alikuwa na KIPAJI

Wahadhiri wengi wa vyuo vikuu huwa wanadhana kuwa wanafunzi wakifanya vibaya kozi yake, wanafunzi hao ndiyo wenye matatizo, mwanakwetu kumbe kufanya vibaya kwa mwanafunzi kunatoa taswira hata ya yule anayefundisia. Kwenye hili Profesa Ngowi HAKULALAMIKIWA.

Profesa Ngowi alikuwa ni mhadhiri mwenye ujuzi wa kuzungumza lugha kadhaa, japokuwa alikuwa anazifahamu lugha hizo, namna alivyokuwa akiongea lugha ya Kiingereza alitumia misamiati ya kawaida mno, namna hiyo ilimwezesha mno mwanafunzi kulielewa somo, kulipenda na hata kulifanya vizuri. Profesa Ngowi alitambua kuwa ujuzi wa lugha wa mtu ni kuwezesha mawasiliano tu. Hapa Profesa Ngowi alikuwa NGULI.

Kwa hakika umahiri huo wa Profesa Ngowi kwa yote niliyosema tutaendelea kumkumbuka kwa kuyaishi haya mema machache ambayo binafsi nimeyashuhudia nikiwa mwanafunzi nimeamua kuyaweka katika maandishi haya.

Godfrey Mbowe ambaye alikuwa mwanafunzi mwezangu wakati huo alinitumie ujumbe juu ya msiba huu baada ya kupata taarifa ya msiba huo.

“Kaka unamkumbuka Dkt Mgowi, jamaa yule aliyekuwa anatufundisha? Hakuwa anatoa alama za upendeleo. Amepata ajali amefariki.”

Binafsi natoa pole kwa familia, nduguze na wote wanaomlilia Profesa huyu.

Raha ya Milele umpe ehe Bwana, Mwanga Milele umuangazie, apumzike kwa amani Amina.

“LALA NA UFOOO PROFESA NGOWI-BURIANI PROPESA NGOWI”

makwadeladius @gmail.com

0717649257

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.