Habari za Punde

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe Hemed Suleiman Abdulla Amewatembelea Wananchi wa Nungwi Walioathirika na Upepo.

Muonekano wa nyumba na maeneo ya kufanyia biashara yaliyoathirika na upepo mkali uliotokea mchana wa jana eneo la kijiji cha Kendwa Nungwi Mkoa wa Kaskazini Unguja.
Mkurugenzi Mtendaji Kamisheni ya kukabiliana na Maafa Zanzibar Ndugu Makame Khatib Makame akitoa maelezo kuhusu hatua watakazochukua kwa wananchi walioathirika na upepo mkali uliotokea mchana wa jana katika eneo la Nungwi 

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla akiwafariji waathirika wa upepo mkali uliotokea Kendwa Nungwi ambapo aliagiza Uongozi wa Kamisheni ya kukabiliana na Maafa kuhakikisha unafanya tathmini ya haraka ya athari iliyotokea katika upepo huo.

Na Ali Muhamed Shaaban , OMPR

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla ameiagiza kamisheni ya kukabiliana na Maafa Zanzibar kufanya Tathmini ya haraka juu ya athari ya upepo uliotokea jana Nungwi Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Mhe. Hemed ambae pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya kukabiliana na Maafa ametoa agizo hilo  alipofika kuwafariji Wananchi walioathirika na upepo huo mkali uliotokea jana Jioni eneo la Nungwi katika kijiji kendwa.

Amesema Serikali imepokea kwa Maskitiko makubwa tukio hilo na kuahidi kuwa pamoja na wananchi hao kwa ukarabati wa majengo hayo kwa kusaidiana na wahisani ili kuyarudisha kama ilivyokuwa awali   .

Mhe. Hemed ameeleza kuwa jukumu la Serikali ni kuhakikisha wananchi wanakuwa katika hali ya usalama kipindi wanapopata maafa ya aina yoyote ile.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amewashukuru wananchi wa maeneo yaliyoathirika na upepo huo kwa kuungana na kuwa wamoja hasa kuwahifadhi wananchi wenzao walioharibikiwa na nyumba zao na kuitaka kamisheni ya kukabiliana na Maafa kuhakikisha huduma ya chakula inapatikana haraka iwezekanavyo kwa wananchi hao.

Sambamba na hayo Mhe. Hemed amewashukuru viongozi wa ngazi zote za Mkoa kwa kuwa karibu kuwafariji wananchi hao na kueleza kufurahishwa kwake kuona Vikosi vya Ulinzi na Usalama vinahakikisha usalama wa kutosha katika maeneo hayo.

Pamoja na mambo mengine Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ameutaka Uongozi wa Shirika la Umeme Zanzibar (ZECO) kuhakikisha wanarejesha huduma ya  umeme kwa muda mchache katika maeneo yaliyokosa huduma hiyo tokea kutokea kwa janga hilo.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Mhe. Ayoub Muhamed Mahmoud ameeleza kufurahishwa kwake kuona wananchi wa maeneo hayo wanaungana kwa pamoja katika kipindi hichi na kuwaeleza wawekezaji walioathirika na upepo huo kuwa jukumu la Serikali ni kuhakikisha usalama wao kwa hali yoyote inayojitokeza.

Nae Mkurugenzi Mtendaji wa Kamisheni ya kukabiliana na Maafa Zanzibar Ndugu Makame Khatib Makame ameeleza kuwa majanga ya Upepo ni hali ya kimaumblie hivyo ni vyema wananchi kuwa wavumilivu na  kumuhakikisha Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kuwa Kamisheni itafanya tathmini ya haraka ili kurudisha hali kuwa ya kawaida. 

Nao wananchi walioathirika na Upepo huo wameishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuungana nao katika kipindi hichi kigumu na kushauri kujengwa kwa makazi ya dharura kwa wananchi watakaoathirika na majanga mbali mbali.

Katika upepo huo uliotokea Mchana wa jana jumla ya Nyumba Arobaini na tatu (43)  na Hoteli Tatu (03) zimeathirika kwa kuezuka mapaa na nyengine kuanguka baadhi ya kuta.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.