Habari za Punde

Mhe Hemed ajumuika na waumini katika Sala ya Ijumaa Masjid Utapoa, Bububu

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar  Alhajj Hemed Suleiman Abdulla amejumuika na waumini wa Masjid Utapoa Bububu Wilaya ya Magharibi “A” katika Ibada ya Sala ya Ijumaa.

 

Akiwasalimia waumini hao baada ya Swala Alhajj Hemed ameeleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar  inayoongozwa na Rais Dkt. Hussein Ali Mwinyi  inachukua jitihada mbali mbali katika kuleta unafuu wa bei za bidhaa ili wananchi waweze kujikimu kimaisha.

Amesema pamoja na jitihada zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar  wapo baadhi ya wafanyabiasha wanapandisha bei  za bidhaa   bila ya kuwa na sababu za msingi  jambo ambalo wanaenda kinyume na jitihada za Serikali za kuwapunguzia ukali wa maisha wananchi wake.

Pamoja na hayo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar  amewakumbusha waumini hao kuwa na tabia ya kupendana na  kusaidiana  kwa kuwajali  watu wenye mahitaji maalumu katika jamii  wakiwemo mayatima,watu wenye ulemavu pamoja na wajane.

Aidha Alhajj Hemed amewahimiza waumini na wananchi kwa ujumla kuendelea kuitunza amani iliyopo ili Serikali iendelee kuwatumikia wananchi wake na kuwaletea maendeleo.

Pamoja na hayo Mhe. Hemed amewakumbusha waumini hao kusimamia misingi ya dini katika maisha yao ya  kila siku na kudumisha ibada  hasa katika miezi hii mitukufu  ili kupata radhi za Allah (S.W.)

 

Nae Maalim Omar Hamad ameiomba Serikali ya mapinduzi ya Zanzibar kusimamia  mila,silka na desturi  ili kuepusha mmomonyoko wa maadili katika jamii.

Ameeleza kuwa katika Jamii kumeibuka mambo mbali mbali yanayoashiria kupotea kwa maadili ya wazanzibari hali ambayo inapaswa kukemewa kwa maslahi ya vizazi vya sasa na vijavyo


 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.