Habari za Punde

SMZ imesema itawachukulia hatua za kisheria watumishi kutoka taasisi na mashirika ya Umma walioshindwa kutoa majibu kwa (CAG)

 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza katika viwanja vya Ikulu Jijini Zanzibar, wakati wa hafla ya kuwasilishwa kwa Taarifa ya Ukaguzi wa Hesabu za Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, iliyowasilishwa leo 3-6-2023 na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Zanzibar Dkt. Othman Abbas Ali.

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema itawachukulia hatua za kisheria watumishi kutoka taasisi na mashirika ya Umma walioshindwa kutoa majibu kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) katika ripoti ya mwaka wa Fedha 2022- 2023 iliyowasilishwa na kusomwa Ikulu, Zanzibar.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi ameyasema hayo alipozungumza kwenye viwanja vya Ikulu, Zanzibar baada ya kuwasilishwa kwa taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Kuu wa Hesabu za Serikali Zanzibar, (CAG).

“Nitatataka kupata majibu kwa wote waliotajwa kwenye ripoti ya CAG ambao hawakutoa majibu, watoe ambao watashindwa kufanya hivyo hatua za kisheria zitachukuliwa” Alilisitiza Rais Dk. Mwinyi

Dk. Mwinyi alisema, ripoti imeonesha mafanikio, changamoto na mapungufu ambayo Ofisi ya CAG iliyabainisha wakati wa uwasilishwaji wake na kueleza kwamba Serikali itachukua hatua mbali mbali zikiwemo za kiutawala na kijinai kwa mujibu wa taratibu na sheria zilizowekwa.

“Kwa wale wote watakaothibitika kufanya ubadhirifu, wizi au uzembe ulioisababishia Serikali kupata hasara, utaratibu wa kuchukua hatua uko wazi” Alibainisha Dk. Mwinyi.

Alisema, kuna baadhi ya maeneo yanahitaji kuchukuliwa hatua za kiutawala na baadhi ya kuchukuliwa hatua za sheria za makosa ya jinai.

Alidha, Rais Dk. Mwinyi alieleza kwamba ataikabidhi ripori hiyo kwa Mamlaka zinazohusika kwa hatua zaidi, ikiwemo Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa na Uhujumu Uchumi, Zanzibar (ZAECA) kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) ili nao waipitie kwa kina mapungufu yote hasa yaliyoashiria wizi kwaajili ya hatua zaidi kwa mujibu wa sheria.

Dk. Mwinyi alisema, ripoti za CAG ni kipimo tosha cha utendaji kwa wale wote waliopewa majukumu na Serikali kwa kufanikiwa ama kushindwa kuyasimamia katika kuitumikia Serikali.

“Utaratibu huu tuliouazisha wakuwasilisha ripoti za CAG hadharani utakuwa wadudumu, nafahamu kuwa haukuzoeleka na unawapa mashaka baadhi ya watu, nataka niwahakikishie kwa wale wenye mashaka, hili litakua zoezi la kila mwaka, na ni moja wapo ya kigezo cha uwazi na utawala bora katika uendeshaji wa Serikali yetu” Alitanabahisha Rais Dk. Mwinyi.

Hata hivyo, aliwataka watendaji na watumishi wa taasisi na mashirika ya Serikali kuendelea kutoa ushirikiano wa kutosha kwa Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, Zanzibar panapokua na wajibu wa kufanya hiyo. Alisema kutofanya hivyo ni kosa kisheria na Serikali haitosita kutimiza wajibu wake.

Akizungumzia mapungufu yaliyojitokeza kwenye ripoti hiyo, Rais Dk. Mwinyi alieleza baadhi ya mapungufu hayo ni ya kiutaratibu, mengi yalisababishwa na wizi na mengine uzembe kwa baadhi ya watu.

Hivyo alieleza, kazi ya CAG kutoa taarifa na mapendekezo kwa Serikali na jukumu la kufanyiakazi ripoti hiyo ni la Serikali.

Mapema, akiwasilisha ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Dk. Othman Abass Ali, aliishauri Serikali kuunganisha pamoja mifumo yote ya fedha ya Serikali, kwa miamala ya fedha zikiwemo fedha zilizoko Benk kuu ya Tanzania (BOT) kupitia mifumo ya Wizara ya Fedha kwa lengo la kuiwezesha mifumo hiyo, kufanya usuluhishi wa upatikanaji wa taarifa za ukusanyaji wa mapato ya Serikali kwa wakati sahihi.

Sambamba na kuziunganisha pamoja sekta zote za Serikali zinazofanyakazi zinazofanana katika mfumo mmoja zikiwemo, Mamlaka ya Mapato Zanzibar (ZRA), Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Zanzibar (ZAA), Kampuni ya Usafirishaji bandarini na nyenginezo ili kupata idadi kamili ya wageni na abiria wanaoondoka Zanzibar kwa lengo la kuwepo kigezo sahihi cha ukokotoaji wa ukusanywaji wa mapato yanayotakiwa kupatikana kutoka kwenye vyanzo hivyo.

Pia aliishauri Serikali kuongeza udhibiti wa dawa, vifaa tiba na vitenganishi, ikiwemo kufanya uteketezaji pamoja na kuvipitia vituo vyote vya afya kwa hospital zote za Wilaya, Mikoa hadi Rufaa kwa dawa zilizomo hospitalini pia kufanya vipimo vya kimaabara ili kugundua dawa na vifaa visivyo salama kwa matumizi wa binaadamu kwa kuzichukulia hatua za haraka na kuziondosha kwa kuziteketeza kwa wakati.

Akizungumzia suala la kulipa fidia kwa wananchi wanaotoa maeneo yao kwaajili ya kupisha miradi ya Serikali ya Maendeleo, CAG akiishauri Serikali kuona umuhimu wa kuwalipa kwa wakati ili kuepusha malalamiko, kucheleweshewa kulipwa kwa wakati kunapunguza thamani ya fidia kutokana na kupungua kwa thamani ya fedha.

Jumla ya ripoti saba ikiwemo ya Serikali Kuu (Mawizara na taasisi zote), Mashirika na Taasisi zinazojitegemea, ripoti ya Idara Maalum na taasisi zake, ripoti ya mifumo yote ya Tehema ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, ripoti ya Mashirika ya Umma, na ripoti ya Ufanisi ya miradi ya Maendeleo iliyofadhiliwa na fedha za Uviko 19 ziliwasilishwa.

Kifungu cha 112 (5) kinamtaka Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali CAG, awasilishe taarifa yote aliyoikagua na aikabidhi kwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa hatua nyengine. Mei 11 mwaka huu alivyanya hivyo na baadae Rais Dk. Mwinyi alimkabidhi Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Katiba, Sheria, Utumishi na Utawala Bora, Haroun Ali Suleiman ambae nae aliikadhiri Baraza la Wawakilishi kwa mujibu wa takwa la kikatiba kwaajili ya kujadiliwa.

IDARA YA MAWASILINO, IKULU ZANZIBAR

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.