Habari za Punde

Taasisi Zinazohusiana na Usimamizi wa Sekta ya Utalii Nchini Kuhakikisha Wajasiriamali wa Ndani Wanapewa Fursa kwenye Sekta ya Utalii Hususan Masoko ya Bidhaa Wanazozalisha

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akihutubia katika Ufunguzi wa Tamasha la Fahari ya Zanzibar na kuadhimisha Mwaka Mmoja wa Wakala wa Uwekezaji  Wananchi Zanzibar (ZEEA) uliofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Golden Tulip Uwanja wa Ndege Zanzibar. 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi, amezitaka taasisi zote zinazohusiana na usimamizi wa sekta ya Utalii nchini, kuhakikisha wajasiriamali wa ndani wanapewa kipaumbale kunufaika na fursa zinazopatikana kwenye sekta ya utalii hususan masoko ya bidhaa wanazozalisha.

Dk. Mwinyi aliyasema hayo alipofungua tamasha la Fahari ya Zanzibar sambamba na maadhimisho ya mwaka mmoja tangu kuanzishwa kwa taasisi ya Wakala wa Uwezeshaji wa nchi kiuchumi Zanzibar (ZEEA) kwenye hoteli ya Golden Tulip, Uwanja wa ndege Mkoa wa Mjini Magharibi.

Alisema hali hiyo itapunguza kwa kiasi kikubwa uingizaji wa bidhaa kutoka nje ya nchi zinazoweza kuzalishwa Zanzibar na kuimarisha soko la ndani kwa wajasiria mali wake.

“Nazika taasisi zote zinazohusiana na usimamizi wa sekta ya utalii nchini, kuhakikisha wajasiriamali wa ndani wawe wanufaika wa kwanza kwa fursa zinazopatikana kwenye sekta ya utalii, hali hiyo itapunguza kwa kiasi kikubwa uingizaji wa bidhaa tunazoweza kuzizalisha, kutoka nje ya nchi na kuimarisha soko la ndani kwa wajasiria mali wetu” Aliagiza Rais Dk. Mwinyi.

Rais Dk. Mwinyi alisema juhudi za kuwawezesha wananchi kiuchumi ni kuhakikisha upatikanaji wa masoko ya ndani na nje ya Zanzibar kwa bidhaa wanazozizalisha, aliongeza uchumi wa Zanzibar una fursa nyingi za masoko kwa bidhaa za wajasiriamali wake kutokana na kuwepo kwa hoteli nyingi za utalii.

Dk. Mwinyi aliwataka wajasiriamali na wafanyabiashara wa ndani kushirikiana na wadau wengine kuzalisha bidhaa zenye ubora kulingana na mahitaji na kunufaika na soko la utalilii liliopo.

Aliongeza, suala la kuwawezesha wananchi kiuchumi ni mtambuka kwa vile linahusisha wadau wengi na sekta mbalimbali zikiwemo Uchumi wa Buluu, Kilimo, Utalii, Biashara, taasisi za fedha, sekta binafsi na asasi zisizo za serikali za kitaifa na kimataifa.

Pia Rais Dk. Mwinyi alieleza taasisi zote hizo zina wajibu na dhima ya kutengeneza fursa za ajira kwa maendeleo ya Zanzibar yanayokwenda sambamba na sera ya taifa ya uwezeshaji wananchi kiuchumi ya mwaka 2022.

Alisema, adhma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kuhakikisha ongezeko la ajira kwa vijana na wanawake linaongezeka kwa kuendelea kutoa fursa nyingi na kuwawezesha kiuchumi kutokana na fursa za mikopo zilizopo.

“Serikali imejidhatiti kutimiza malengo ya ilani ya Uchaguzi ya CCM 2020 /2025 ya kuzalisha fursa za ajira laki tatu kwa kipindi cha miaka mitano, ni dhahiri kasi iliopo idadi hii haiwezi kusalishwa na ajira kutoka serikalini pekee bila shaka fursa nyingi za ajira zitatokana na kuwawesha wananchi kujiajiri ambapo wajibu wa Serikali ni kuandaa mazingira wezeshi kwa wananchi wake ili kujikwamua” alieleza Rais Dk. Mwinyi.

Alisema, Serikali inaendelea na hatua ya kuimarisha na kuinua maeneo ya biashara ikiwemo ujenzi wa masoko na maeneo muhumu ya kufanyia biashara kwenye maeneo ya vituo vya mabasi, lengo ni kuwapatia wafanyabiashara hao wateja wengi wa bidhaa zao kwenye maeneo yenye mikusanyiko mikubwa ya watu.

Alisema tamasha hilo ni jukwaa muhimu la kuwakutanisha na kuwaweka pamoja wadau wote pamoja na wajasiriamali mbalimbali kwa kubadilishana uzoefu kwenye tasnia hiyo. 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Kazi, Uchumi na Uwekezaji, Mudrik Ramadhan Soraga alieleza lengo na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kuendelea kutoa mikopo isiyo na riba kwa wananchi wake na kuwawezesha wajiajiri kupitia mikopo inayowapatia na kuyafikia malengo yao kiuchumi.

Alisema Wizara ilijipangia kuwakopesha wajasiriamali 12,000 kwa mwaka na sasa imefikia idadi ya 19,000 nakuongeza kuwa kiasi cha bilioni 20.2 zimekopeswa kwa wananchi nakueleza mahitaji yameongezeka zaidi kutokana na maombi ya wananchi wengi yamefikia bilioni 80.

Akizungumza kwenye hafla hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Uwezeshaji wananchi Kiuchumi, Juma Burhan Muhamed alisema taasisi hiyo imeingia makubalianao na taasisi mbalimbali wezeshi kwa wananchi zikiwemo, Taasisi ya Mwanamke Initiative Foundation (MIF), Zanzibar Maisha Bora Foundation, Tan Trade na taasisi nyengine ili kuwainua wajasaliriamali wa ndani wakiwemo vijana, wanawake na wakulima wa mwani kwa kuendelea kuwatafutia soko la bidhaa wanazozizalisha.

Pia alieleza taasisi hiyo inaongeza uelewa kwa jamii kuthamini na kutumia bidhaa zinazozalishwa ndani ambapo wajasiriamali 19,373 walikopeshwa kiasi cha shilingi bilioni 20.2 kwa Unguja na Pemba.

Wakala wa uwezeshaji wananchi kiuchumi Zanzibar ni taasisi iliyoundwa mwezi Machi mwaka 2022 ikipewa jukumu la kutekeleza na kuratibu, shughuli zote za uwezeshaji wananchi kiuchumi.

IDARA YA MAWASILIANO IKULU, ZANZIBAR

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.