Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Mwinyi Awahutubia Wananchi wa Mkoa wa Kazkazini Unguja leo.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na Wananchi wa Mkoa wa Kaskazini Unguja, akiwa katika ziara yake katika Mkoa huo leo 23-10-2023 kutembelea Miradi ya Maendeleo katika Mkoa huo
WAZEE wa Kijiji cha Kivnge Mkoa wa Kaskazini Unguja wakimsikiliza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi (hayupo pichani) akiwa katika ziara yake katika Mkoa huo, kutembelea miradi ya maendeleo.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akiwasalimia Wananchi wa Mkoa wa Kaskazini Unguja, akiwa katika ziara yake katika Mkoa huo kutembelea Miradi ya Maendeleo leo 23-10-2023, baada ya kuifungua Hospitali ya Wilaya Kivunge.

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar imeamua kuweka mfumo wa Rufaa kwa hospitali zote za wilaya nchini.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi aliyasema hayo kwenye ziara ya kuutembelea mkoa wa Kaskazini Unguja alipozindua hospitali ya Wilaya, Kivunge.

Alisema, Serikali imeweka utaratibu huo kwa lengo la kuimarisha huduma bora za Afya ziwe za uhakika zikiwemo Maabara, X-ray, ultrasound mashine za kisasa na dawa na nyengine kwa maradhi yote ya kawaida ikiwemo uzazi, huduma za uchunguzi na mengine ili kupunguza msongamano kwenye hospitali kuu ya Mnazi Moja.

Aidha, aliwataka wananchi wote kurejesha imani zao kwa hospitali za Serikali kwani sasa zinatoa huduma bora na zina dirisha maalum za mfuko wa bima ya afya na kuwasisitiza watoa huduma kwenye hospitali hizo kuharakisha huduma zao sio kuweka misongamano ya wagonjwa.

Pia, Rais Dk. Mwinyi aliwatoa hofu watumishi wa Serikali na ajira zao na kuwaeleza licha ya Serikali kushirikisha sekta binafsi kwenye hospitali hizo ajira zao zitaendelea kuwa salama.

Vilevile, Dk. Mwinyi alihimiza umuhimu wa kuweka kambi maalumu na wataamu wa maradhi mbalimbali ikiwemo macho, moyo, meno na mifupa.

Naye, Waziri wa Afya, Nassor Ahmed Mazrui alisifu juhudi za Rais Dk. Mwinyi kuimarisha miundombinu ya sekta ya Afya kwa ujenzi wa hospitali 10 za Wilaya Unguja na Pemba pamoja na hospitali moja ya Mkoa.

Akiwa ziarani Mkoa wa Kaskazini Unguja, Rais Dk. Mwinyi aliweka jiwe la msingi kwenye ujenzi wa Skuli ya msingi ya ghorofa mbili Donge, itakayokuwa na madarasa 29, ofisi za walimu, mwalimu mkuu, vyumba vya maktaba, maabara, vyumba vya TEHAMA (ICT), vyoo, stoon na chumba cha kusalia.

Pia, Rais Dk. Mwinyi alisifu juhudi za maendeleo zilizofikiwa na sekta ya elimu, Zanzibar kupita malengo ya ilani ya uchaguzi ya CCM ya 2020 – 2025 ikiwemo kukamilika kwa skuli za kisasa za ghorofa na madarasa yatakayochukua wanafunzi 45 kwa mkondo mmoja tuu.

Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali, Lela Muhamed Mussa, alipongeza juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuimarisha miundombinu ya kisasa kwenye sekta ya elimu ndani ya kipindi cha miaka mitatu ya uongozi wa Dk. Mwinyi kwa kuwa na miradi ya kimkakati ya skuli za kisasa.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja, Ayoub Mahmoud alieleza mafaniko ya mkoa huo ikiwemo kuimarika sekta za miundombinu ya barabara, bandari pamoja na huduma za jamiii, maji safi, vituo vya afya, kukamilika kwa soko la kisasa Donge Mtambile litakalotosheleza mahitaji wa wananchi wa eneo hilo na maeneo jirani.

Alisema, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imetoa michango mkubwa kutekeza miradi mikubwa ya maendeleo ya mkoani humo.

Ziara ya Rais Dk. Mwinyi Mkoa wa Kaskazini Unguja ni mwendelezo wa ziara zake za kukagua miradi ya maendeleo ikiwa ni kuanza shamrashamra na sherehe za mafaniko ya uongozi wake unaotimiza miaka mitatu.

IDARA YA MAWASILIANO IKULU, ZANZIBAR

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.