Habari za Punde

Na.Kitengo cha Habari OMKR .                        

Mwenyekiti wa Chama cha ACT wazalendo Taifa Mhe. Othman Masoud Othman, amewataka wanachama wa Chama hicho pamoja na wananchi kwa jumla kusimama pamoja katika kupigania mageuzi ya kisiasa Zanzibar jambo litakalosaidia kuondoa kero na matatizo ya wananchi  waliyonayo.

Mhe. Othman ameyasema hayo huko katika Kijiji cha Muwi Shehia ya Mjanaza  Jimbo la Pandani wilaya ya Wete Kaskazini Pemba alipojibu hoja mbali mbali za wanakijiji hao baada ya kuwapa fursa ya kuuliza maswali  alipowatembelea kijijini hapo akiwa kwenye ziara ya Kisiasa  na Kiserikali kisiwani Pemba.

Amesema kwamba chama hicho kimejipambanua kutetea mabadiliko na mageuzi ya kisiasa nchini kutokana  na wananchi wengi kuwa na kero mbali mbali zikiwemo za huduma za kijamii wanazostahiki kuzipata bila kuwepo usumbufu wowote.

Amefahamisha kwamba zipo huduma nyingi kama zile vyeti vya Kuzaliwa na Kitambulisho cha Mzanzibari mkaazi  ambazo ni miongoni mwa zilizowekwa rasmi na Serikali na wananchi wote wanastahiki kuzipata bila kuwepo usumbufu jambo ambalo ni kinyume na ilivyo sasa.

Amesema kwamba viongozi wengi wameapa viapo vya uaminifu kulinda Sheria na Katiba kutokana na dhamana zao walizopewa lakini wengi wanavikiuka viapo hivyo kwa kuviendea kinyume na pia kutozingatia matakwa ya sheria ikiwemo sheria mama ambayo ni Katiba.

Amefahamisha kwamba ni muhimu kwa viongozi wa serikali  na watumishi wengine wa umma kuhakikisha kwamba wanawajibika kwa wananchi kwa kuwatumikia kwa mujibu wa sheria na viapo vyao kwa kuwa kufanya hivyo ndio wajibu wao kwa wananchi na ni matakwa ya sheria na katiba ya Zanzibar.

Amesema kwamba viongozi wengi wamekuwa majasiri wa kuropoka kwa kutetea masuala ambayo kisingi ni batili na yanakwenda kinyume na matakwa ya sheria na katiba ya nchi jambo ambalo linahitaji kuondolewa kupitia kura za wananchi na kuleta mageuzi .

Aidha amesema kwamba suala hilo pia ni muhimu katika kurejesha nidhamu ya serikali kwa kuwa na viongozi waliochaguliwa na wananchi wanaowajibika kwao katika kupigania maslahi ya kimaendeleo katika taifa lao.

Mapema baadhi ya wananchi wa Jimbo la pandani kutoka shehia za Mjananza, Mlindo, Muwi na nyenginezo walilamika mbele ya Mhe. Othman kwamba wamekuwa wakipta usumbufu mkubwa wa katika kupatiwa huduma za vitambuliso vya mzanzibari mkaazi pamoja na vyeti vya kuzaliwa.

Mhe. Othman anaendelea na ziara yake ya siasa na Kiserikali kisiwani Pemba na Kesho tarehe 3 Disemba 2024 anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika kilele cha maadhimisho ya siku ya watu wenye ulemavu duniani ambapo kwa Zanzibar yanatarajiwa kufanyika katika viwanja vya Gombani ya Kale wilaya ya Chake chake mkoa wa Kusini Pemba.

Mwisho

Imetolewa na ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzib ar kupitia Kitengo chake cha Habari leo Disemba 2, 2024.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.