Habari za Punde

Mheshimiwa Rais, Rungu la Kuwawajibisha Unalo


Hivi karibuni Rais wa Zanzibar Dk Ali Mohammed Shein alinukuliwa akitoa karipio kali kwa Mawaziri na watendaji wasiotekeleza majukumu yao kwamba ima waondoke wenyewe kabla ya kuondoshwa na Rais.
Dk Shein aliwataka watendaji wote kutekeleza wajibu wao na kufanya kazi kwa bidii ili kuwaletea maendeleo wananchi wa Zanzibar.

Kauli nzito kama hii kutoka kwa kiongozi mkuu wa nchi inaashiria mambo mengi kwa wachambuzi wa habari.


Kwanza kuna viongozi wazembe ndani ya Serikali wasiotekeleza wajibu wao ilhali walipoteuliwa kushika nyadhifa hizi walitarajiwa na Rais kuwajibika ipasavyo.

Pili Kuna viongozi mzigo katika Serikali wamebebwa, wamepewa dhamana, wamepewa semina elekezi na bado hawajijui au hawajitambui kitu gani wanatakiwa kukifanya katika kukabiliana na majukumu ya kazi zao.

Na tatu Mheshimiwa Rais anatumia fursa ya mwisho kuwaonya mbele ya wananchi badala ya kuwaonya nyuma ya pazia ili wajijue kwamba Rais anawafahamu na kuwafuatilia nyendo zao.

Inawezekana Rais alipopendekezewa majina ya viongozi na watendaji aliowateua kushika nyadhifa tofauti  alijenga imani kubwa kwao kama watakabiliana na majukumu yao na kutekeleza wajibu wao kama watendaji  kiufanisi si kwa malengo waliyowekewa  tu bali kupita zaidi na hapo kuweza kuonekana utendaji wao kinadharia na kivitendo. Hili linaonekana sasa kumtesa Rais na ni yeye mwenye dhamana ya kuwaweka na kuwaondoa kwani aliyotarajia siyo yanayotokea..

Dhana ya uwajibikaji Serikalini ima haitambuliki au haitakiwi. Sote tulishuhudia maafa ya MV Spice hakuna aliyewajibika mpaka ilipoundwa Tume. 

Hivi karibuni Tume ya Baraza la Wawailishi ilitoa hadharani taarifa ya uchunguzi ulioagizwa kufanywa na Baraza la Wawakilishi ambayo iliwanyooshea vidole watendaji Serikalini wakiwemo Mawaziri na Watendaji wangine wakuu. Serikali imeipokea na kuthibitishia itaifanyia kazi na hili pia linaashiria nia njema ya Serikali kuvipa nafasi mihimili mengine ya utawala kama Bunge na Mahakama kufanya kazi zake bila ya kuingiliwa na Serikali kuu. Tusubiri tuone khatma yake.

Cheo ni dhamana si utajiri wala ulwa. Cheo ni masuuliyah hatutoulizwa na waliotukabidhi tu dhamana bali pia Muumba naye atakuja kutuuliza.

Hivi kweli kama ni wewe kiongozi/mtendaji unaezembea  au usiejibidiisha katika kutekeleza dhamana na majukumu umemsikia aliyekuteuwa? Ulipoapa mbele ya Mheshimiwa Rais ulielewa uzito wa kiapo chako? Ulipobeba Msahafu au Biblia ulifahamu maana na uzito wa kitabu kitakatifu wakati unaapa?  Unapoingia Ofisini unajitathmini utendaji wako?

Mheshimiwa Rais, wananchi tumekusikia tupo pamoja na wewe lakini kama rungu unalo mwenyewe tumekupa ridhaa kulitumia kwa maslahi ya nchi na wananchi wa Zanzibar. 

1 comment:

  1. Kwetu Z'bar suala la kuwajibishana ni gumu kwani viongozi na watendaji wengi wa serikali wamechaguliwa ama kisiasa(watoto wa wanamapinduzi, au wazee wao walimuwezesha mzee kuingia madarakani) au anatoka shamba fulani.

    Kwa hivyo, Rais amesema lkn. utekelezaji ni 'issue'

    ReplyDelete

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.