Na Rajab Mkasaba, Ikulu
OFISI ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar wamepongeza juhudi za Rais wa
Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein za
kuhakikisha masuala ya Mazingira, UKIMWI, Dawa za kulevya na Watu Wenye Ulemavu
yanashughulikiwa kikamilifu na Serikali pamoja na jamii kwa ujumla.
Uongozi wa Ofisi hiyo, ulieleza hayo katika mkutano wa
kuangalia utekelezaji wa kazi za Wizara hiyo kwa kuangalia robo tatu ya utekelezaji
wa Bajeti ya mwaka wa fedha 2011-2012 na
kulinganisha na robo ya kwanza na ya
pili pamoja na vipaumbele na malengo kwa mwaka wa fedha 2012-2013.
Mkutano huo uliofanyika Ikulu mjini Zanzibar uliongozwa na
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein,
ambao pia, ulihudhuriwa na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif
Sharif Hamad na Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Abdulhamid Yahya Mzee.
Uongozi huo, ulieleza kuwa umekuwa ukishuhudia kuona Dk.
Shein akiwa ameshika usukani katika kutoa mwamko wa masuala ya UKIMWI, dawa za
kulevya, masuala ya watu wenye ulemavu na mazingira kiasi ambacho kila
akizungumza na wananchi masuala hayo huwa anayagusia.
Waziri wa Wizara hiyo Fatma Fereji, akisoma utangulizi wa
taarifa ya utekelezaji wa mpango kazi, alisema kuwa juhudi za Dk. Shein ndizo
zinazoupelekea uongozi wa Ofisi hiyo kuwa na msukumo na hamasa katika
kufanikisha malengo waliyojiwekea.
Ofisi hiyo ilimuahidi Dk. Shein kuwa itaendelea kumuunga
mkono katika kufanikisha juhudi hizo ili Zanzibar
kuwa bila dawa za kulevya, na kuwa mfano katika uhifadhi wa mazingira, udhibiti
wa maambukizi mapya ya UKIMWI na kuwa na jamii jumuishi.
Miongoni mwa vipaumbele ilivyoeleza Ofizi hiyo ni pamoja na
kuandaa Sera ya Dawa za Kulevya na Sera ya Watu Wenye Ulemavu, kuanza ujenzi wa
kituo cha tiba na kurekebisha tabia kwa watu walioacha dawa za kulevya sanjari
na kuingiza somo la dawa za kulevya katika mitaala ya skuli.
Nae Makamu wa Kwanza wa Rais Maalim Seif Sharif Hamad alitoa
pongezi kwa Ofisi hiyo ambayo iko chini yake na kueleza kuwa mafanikio
iliyoyapata yanatokana na mashirikiano ya pamoja ya uongozi wa Ofisi hiyo.
Dk. Shein kwa upande wake, alitoa pongezi kwa Wizara hiyo
kwa mafanikio iliyoyapata katika utekelezaji wa Mpango kazi wake na kusisitiza
haja ya kuwaeleza wananchi mafanikio hayo sambamba na mikakati na mipango
iliyowekwa na Idara, Taasisi zake kupitia vyombo vya habari.
Aidha, Dk. Shein alisisitiza haja ya kuwepo kwa kumbukumbu
pamoja na umuhimu wa kuandaa ripoti kwa viongozi na watendaji wangine pale
wanapofanya ziara za kikazi ndani ya Zanzibar
na hata nje ya nchi.
Wakati huo huo, Dk. Shein alikutana na uongozi wa Ofisi ya
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ambapo Ofisi hiyo katika taarifa yake
ilieleza kuwa Dira yake kubwa ni kuwa na Serikali yenye kutoa huduma bora kwa
jamii na yenye muhimili mzuri wa uchumi, umoja na maendeleo endelevu.
Sambamba na kuratibu na kusimamia utekelezaji wa shughuli
za Serikali katika sekta zote za SMZ na mambo ya Muungano kwa kufuatia misingi
ya Katiba, Sheria na taratibu pamoja na kuhakikisha kufuata misingi ya haki za
binadaamu na ushirikishwaji.
Akisoma utangulizi wa taarifa ya utekelezaji wa mpango
kazi, waziri wa Wizara hiyo Mohamed Aboud Mohamed imeelezea vipaumbele vyake ikiwa ni pamoja na
kuimarisha Kiwanda cha Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali kwa kuyafanyia matengenezo
majengo ya Kiwanda kilichopo Maruhubi na kununua mitambo mipya kwa ajili ya
kiwanda hicho.
Aidha, Ofisi kwa kushirikiana na COSTECH na wadau wengine
itaendelea kuimarisha shughuli za utafiti kwa kuainisha vipaumbele vya utafiti,
kujenga uwezo Kamati za kusimamia masuala ya utafiti, kuwajengenea uwezo
watafiti chipukizi pamoja na kutafuta fedha kwa ajili ya shughuli za utafiti.
Kwa vile nchi inakabiliwa na sherehe kubwa za maadhimisho
ya miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar,
Ofisi imeeleza kuwa imeweka kipaumbele kwa matayarisho ikiwemo ununuzi wa
vifaa, na kuandaa mpango mzima wa maadhimisho hayo.
Pia, Ofisi hiyo imeweka kipaumbele katika kuendelea kujenga
uwezo wa jamii juu ya kukabiliana na maafa kwa kutoa elimu, kutafuta vifaa,
kuazisha vituo vya dharura na kuandaa
majaribio ya kujiandaa na maafa.
Nae Dk. Shein kwa upande wake alitoa pongezi kwa Ofisi hiyo
kwa mafanikio iliyoyapata pamoja na mashirikiano yaliopelekea kupata mafanikio
hayo huku akisisitiza haja ya kwuaeleza wananchi juu ya mafanikio hayo.
No comments:
Post a Comment