Habari za Punde

Vurugu Zasitisha Masomo


Na Khamisuu Abdallah
KUFUATIA fujo zilizotokea juzi katika mji wa Zanzibar na vitongoji vyake, kumepelekea kusita kwa baadhi ya huduma za elimu katika baadhi ya skuli mbalimbali za mjini Unguja.

Zanzibar Leo ilishuhudia baadhi ya skuli hizo kusimamisha masomo kutokana na vurugu zilizoanza Jumamosi na hivyo baadhi ya skuli za mjini hapa kuwaondosha mapema wanafunzi kabla ya kukamiika kwa viipindi vya masomo.


Gazeti hili lilishuhudia baadhi ya skuli zilizositisha masomo hayo kuwa ni pamoja na skuli za Mwanakwerekwe, Darajabovu, Kajificheni na skuli  za mjini.

Mwalimu Mkuu wa Skuli ya Mwanakwerekwe “H” Hityari Haidhuru Ramadhan, akizungumzia kadhia hiyo alisema wameamua kusitisha huduma hizo kutokana na fujohizo kwani zinawapa wasiwasi mkubwa wa kuendelea na masomo hasa ikizingatiwa kuwa wanafunzi wanaweza kudhurika na fujo hizo kwa njia moja au nyengine.

Alisema pamoja na mambo mengine wameamua kusitisha masomo kutokana na skuli hiyo kuwepo karibu na Mahakama ya Wilaya Mwanakwerekwe, ambapo watuhumiwa wa fujo hizo wamekuwa wakipelekwa mahakamani hapo kujibu tuhuma zinazowakabili.

“Wanafunzi waliohudhuria skuli hapo inawapelekea kutoka madarasani na badala yake kutizama askari waliokuwepo nje ya mahakama hiyo hali ambayo inayowazidisha wasiwasi kwa wanafunzi hao,” alisema mwalimu mkuu huyo.

Sambamba na hilo, Mwalimu  Hityari, alisema kutokana na fujo hizo kumekuwa na mahudhurio madogo ya wanafunzi skulini hapo ambapo wazazi wamekuwa wakizuia watoto wao.

“Tumewasiliana na Afisa wa Elimu Wilaya kuwa hali sio nzuri katika maeneo ya Mwanakwerekwe na hivyo tukatakiwa kuwaondosha wanafunzi mapema pamoja na sisi walimu na hali hii si kwa leo tu tutaendelea na utaratibu huu hali itapotulia ,” alisema Mwalimu huyo.

Hivyo mwalimu huyo aliwataka wazazi kuwazuia watoto wao hadi hapo hali itakaporejea kama kawaida, kwa lengo la kuepusha madhara yatakayoweza kutokea.

Kwa upande wa wazazi wa wanafunzi ambao hawakutaka kutajwa majina yao, walisema wamesikitishwa na vitendo vinavyofanywa na wanaosadikiwa wafuasi wa jumuiya ya muamsho.

Walisema vitendo hivyo kwa kiasi kikubwa vimekuwa vikirejesha nyuma kuwaruhusu watoto wao kwenda maskuli na hata wao kuendelea na kazi zao za ujenzi wa taifa.

Aidha waliwataka watu walioanzisha fujo hizo kuacha mara moja kwani kufanya hivyo kunapelekea kuzorotesha huduma mbalimbali za kijamii na kuifanya nchi kutokuwa na amani.

Wazazi hao waliiomba serikali kudhibiti vitendo hivyo na kuwachukulia hatua za kisheria wale wote wanaohusika na vitendo vya uvunjifu wa amani katika kisiwa cha Unguja.  

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.