Habari za Punde

Mashine ya DNA kupatikana mwezi ujao


Na Othman Khamis, OMPR
CHUO Kikuu cha Brown kilichopo mjini Boston nchini Marekani, chini ya taasisi inayoshughulikia taaluma ya teknolojia ya afya (MED International), kinakusudia kuipatia Zanzibar mashine ya uchunguzi wa vinasaba (DNA).

Mashine hiyo inatarajiwa kuwasili nchini muda wowote kuanzia mwezi Julai mwaka huu, ambapo kupatikana kwake kunatokana na ziara ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi, aliyoifanya mwezi Oktoba mwaka jana.


Mkurugenzi wa MED International, Jayson Marwaha, alithibitisha kuwa taasisi yake itaipatia mashine ya DNA, wakati alipofanya mazungumzo na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi huko ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar.

Katika zaiara hiyo, Jayson alifuatana na Mkurugenzi mwenza wa Han Sheng Chia, walimueleza Balozi Seif,  sambamba na msaada huo wamekuja Zanzibar kufanya utafiti wa afya katika hospitali tofauti za serikali za Unguja na Pemba.

“Lengo letu kufanya utafiti wa afya hapa Zanzibar, lakini pia tutaangalia maeneo na vifaa vinavyohitajika na tutakaporejea kwenye taasisi yetu tuweze kuchukua kwa nia ya kuimarisha ustawi wa Jamii hasa ile ya kawaida”, alisema Mkurugenzi huyo.

Jayson, alieleza kwamba katika kuona taaluma ya kiuhandisi ndani ya sekta ya afya inakuwa kiteknolojia taasisi yake inatarajia pia kuleta mabingwa wa fani hiyo mnamo mwezi wa Agosti mwaka huu.

Katika mazungumzo yao nchini Marekani mwaka jana, Jayson aliwahi kumuahidi Balozi Seif kwamba taasisi yake itaandaa taratibu kwa wataalamu wake kufanya kazi za kujitolea hapa Zanzibar.

Naye Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi aliipongeza taasisi hiyo inayoshughulikia taaluma ya teknolojia ya afya kwa uamuzi wake wa kusaidia huduma za afya hapa Zanzibar.

Balozi Seif, alielezea kufarajika kwake na ujio wa uongozi wa juu wa taasisi hiyo ambao umeonyesha uungwana katika kutimiza ahadi zake ilizozitowa mwaka jana.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliueleza ujumbe huo kwamba serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inakusudia kuimarisha zaidi huduma za afya katika hospitali zake zote Unguja na Pemba.

Mapema Naibu waziri wa Afya Zanzibar Dk. Sira Ubwa Mwamboya, alisema ujumbe huo umekuja wakati muwafaka kwa vile bado eneo la fani ya sayansi katika chuo cha Sayansi ya Afya Mbweni inahitajika.

Wakati huo huo, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi, alikabidhi msaada wa gari moja kwa ajili ya matumizi ya shughuli za Jumuiya ya Fiy Sabilillah Markaz ya Fuoni.

Balozi Seif, alisema yeye binafsi, familia yake na wafadhili wameamua kutoa msaada huo kutokana na mchango mkubwa unaotolewa na Jumuiya hiyo ndani katika kueneza Daawa kwa jamii.

Mapema katibu wa Jumuiya ya Fiy Sabilillah Markaz ya Fuoni, Sheikh Mwalimu Hafidh Jabu, aliuomba uongozi wa serikali kuwa karibu zaidi na Jumuiya hiyo kwa lengo la kufanikisha majukumu waliyojipangia.






No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.