Habari za Punde

Muasisi wa ‘Kili Marathon’ amfyagilia JK



Na Mwandishi wetu, Moshi

MWANZILISHI wa mbio za marathoni za Mlima Kilimanjaro Marie Frances kutoka Marekani, amemwagia sifa Rais Jakaya Mrisho Kikwete, kuwa ni kiongozi anayependa nchi yake na anayeona mbali.
Marie Frances ametoa sifa hizo mjini Moshi wakati Rais Kikwete alipokuwa akikutana na viongozi wa Chama cha Riadha Tanzania (AT), kwa ajili ya kupanga mikakati ya kufufua riadha nchini.
Frances ambaye aliwahi kukutana na Rais Kikwete wakati wa ufunguzi wa jengo la Tanzania House katika jiji la Washington DC, amesema kuwa ni nadra sana kuona kiongozi wa nchi akikutana na viongozi wa chama cha mchezo wowote kuzungumzia maendeleo yake, na kusema hiyo ni miujiza hata katika nchi kama Marekani.

Amemuelezea Rais Kikwete kama mtu wa haiba ya kipekee mwenye akili na maono ya kuiendeleza Tanzania kufikia malengo ya Umoja wa Mataifa ya Millenia.
“Nilimpenda sana nilipokutana naye jijini Washington. Ni kiongozi mwenye haiba ya kipekee” alisema Frances ambaye aliombwa na Balozi wa zamani wa Tanzania nchini Misri kuja kuanzisha mbio za marathon nchini Tanzania mwaka 1990.
Marie Frances ambaye alikuwa mkuzaji (producer) wa Miss Universe pamoja na vipindi vya televisheni huko Hollywood nchini Marekani, alihamia Misri mwaka 1984 kufanya kazi ya ABC akiwa mwandishi wa bahari.
Akiwa nchini Mirsi, Marie Frances alianzisha mbio za Pyramid Marathon pamoja na Miss Universe ambazo ziliitangaza sana nchi hiyo.
Ni wakati wa matamasha haya balozi wa Tanzania nchini Misri wakati huo alipomwomba aje Tanzania kuanzisha mbio za marathon ili kuitangaza Tanzania.
Frances alikuja Tanzania mwaka 1990 na kutaka kuanzisha mbio za ‘Mt. Meru Marathon’ lakini alipofika tu mjini Moshi alivutiwa sana na mlima Kilimanjaro na hivyo kuamua kuanzisha mbio za ‘Mt. Kilimanjaro Marathon’ mwaka 1991.
Mbio hizo hufanyika kila Jumapili ya mwisho ya mwezi wa sita na zitatimiza miaka 22 tarehe 24 Juni mwaka huu.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.