Habari za Punde

Wazanzibari waishio Canada Kushirikiana na Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ Ltd)


ZACADIA
-Wazanzibari waishio Canada wataendelea Kuisaidia Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ Ltd)
Mradi Mpya wa Kuwasaidia Watoto Masikini Zanzibar Wazinduliwa Nchini Canada
Wazanzibari waishio Canada chini ya Kikundi cha ZACADIA (Zanzibar-Canadian Diaspora Association)
Wamekusudia kuendelea kufanya kazi na Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ Ltd) katika juhudi zake za utumaji pesa kwa gharama ndogo na wa kuaminika kwa njia ya haraka hadi Zanzibar wakiwa katika nyumba zao nchini Canada, kwa kutumia njia tafauti ikiwa ni pamoja na kutumia kadi zao za debit/credit na njia ya moja kwa moja kwa kutumia kompyuta. (Online bank transfers).

ZACADIA, ambayo lengo lake kuu ni kusaidia kuitangaza Zanzibar nchini Canada na nchi za nje kwa jumla, pia inafanya kazi ikiwa kama ni kiungo kati ya Wazanzibari waishio Canada na nchi yao asili ya Zanzibar.
ZACADIA ina mawasiliano ya moja kwa moja na Idara ya Uhusiano wa Kimataifa na Kitengo cha “Zanzibar Diaspora” katika Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais wa Zanzibar.


Mwenyekiti wa Mteule wa Kamati Maalum ya ZACADIA aliwasilisha taarifa yake siku ya Jumamosi tarehe 14 Julai, 2012, katika ukumbi wa Driftwood Community Centre, Toronto, ambapo ndipo palipofanyika mkutano wa Kamati hiyo, baada ya kurejea Canada kutoka Zanzibar ambako alikuweko kwa ziara ya kikazi kwa muda usipungua miezi sita, akijaribu kukutana na Jumuia mbali mbali za wananchi wa Zanzibar ambazo zina lengo sawa na Jumuia ya ZACADIA.

Wakiipokea taarifa ya Mwenyekiti Mteule, wajumbe wa Kamati Maalum walifurahishwa na hatua hiyo na wakaonesha moyo wao wa kutaka kuendelea kufanaya kazi na Benki ya Watu wa Zanzibar kwa ajili ya kupata njia yenye gharama ndogo ya huduma ya kutuma pesa kutoka Canada kupitia Benki hiyo. Kwa mujibu wa data za  Benki Kuu ya Dunia (http://remittanceprices.worldbank.org), kuna makampuni mengi ya aina hiyo, lakini jitahada kubwa inahitajika ili kampuni iweze kukubaliwa.

 “Wakati watu wengine katika nchi kadhaa duniani wakiwa wanazisaidia nchi zao kwa juhudi ya hali ya juu kabisa kwa mpango wa kutuma pesa kwa kutumia njia ya Benki kwa Benki, na sisi Wazanzibari tunahitaji kufanya kama hivyo kwa msaada wa taasisi zetu za fedha huko Zanzibar.” Aliwahamasisha wajumbe wa Kamati Maalum walioaminiwa na kupewa jukumu la kutafuta njia za namna ya kuisaidia Zanzibar kuendelea mbele.
“Sisi Wazanzibari tuishio nje tuna hamu  na nia ya kuzipeleka rasilimali zetu chache tulizonazo katika visiwa vyetu kwa ajili ya kuwaboresha wananchi wa nchi yetu, lakini hatutoweza kufanya hivyo kwa kutumia njia zilizopo sasa hivi ambazo zinatoza gharama  kubwa kupita kiasi,”  mjumbe mwengine alikemea miongoni mwa wajumbe wa Kamati Maalum.
Mwenyekiti Mteule aliwaelezawajumbe wa Kamati Maalum kwamba wakati akiwa Zanzibar, alionana na maofisa wa PBZ, na kwa hiyo, ZACADIA sasa inaweza kuwasaidia Wazanzibari wanaoishi Canada kufugua hesabu zao za fedha za kigeni katika Benki ya PBZ bila ya wao kwenda Zanzibar. Ametoa wito kwa Wazanzibari waishio Canada kujitokeza mbele ya Kamati ya Uongozi ya ZACADIA ili waweze kusaidiwa mara moja namna ya kuweza kufungua hesabu hizo ili waweze kuisaidia Zanzibar kiuchumi. Pia aliahidi kuwa ZACADIA itapanua msaada wake kwa taasisi zote za kitaifa za Zanzibar kwa ajili ya kuiokoa Zanzibar kiuchumi-jamii ambao kwa sasa umeenea duniani.
Wakati huo huo, mradi mpya unaotarajiwa kuzinduliwa na ZACADIA ulifikishwa katika kikao hicho. Mradi huo ambao utajulikana kwa jina la “Zanzibar Children’s Fund Program-ZCFP” utawasaidia kuwapatia huduma za kuondoa umasikini kwa kuwapatia elimu miongoni mwa watoto masikini na mayatima katika vijiji vya Zanzibar, Unguja na Pemba ambao wazee wao wamo katika hali duni ya kimaisha na wanashindwa kuwapatia mahitaji ya skuli watoto wao.
Mradi huo utatoa misaada ya kifedha usio wa moja kwa moja kwa watoto hao ikiwa ni  huduma za msingi kama vile viatu, vitabu, madaftari, nguo, n.k. Mradi huu utafanikiwa kwa kuwahamasisha Wazanzibari na wafadhili wengine duniani kwa kila mmoja kumdhamini mtoto mmoja, ambapo kwa kila mdhamini huyo atakuwa akichangia dola 1 ya Kimarekani kwa siku. Hata hivyo, ikiwa hiyo itakuwa ni mzigo kwa mtu mmoja kumchangia mtoto mmoja kwa mwezi dola moja, basi wajumbe wamekubaliana kuwa hata kama watu 4 watashirikiana kumdhamini mtoto mmoja mpaka mtoto huyo atakapomaliza skuli ya sekondari, kwa kuchangia senti 25 za Kimarekani kila mmoja kwa siku. Mradi huo pia umekusudia kuwasaidia wazee wa watoto husika wawe wenye kujitosheleza na kujitegemea wenyewe kwa kuwapatia mafunzo, vifaa na pesa ili waweze kuzitumia katika uzalishaji mdogo mdogo kwa kujiondoshea umasikini na kuweza kuyamudu maisha yao.
Katibu
ZACADIA                                                                                                 
                        

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.