Habari za Punde

Balozi Seif:Hakuna haja kukimbilia nje kutafuta elimu



Na Hafsa Golo
MAKAMU wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi amesema serikali inahitaji wataalamu wengi katika sekta ya kilimo ili kufikia malengo ya uzalishaji mzuri wa chakula nchini.
Aliyasema hayo baada ya kuzindua dakhalia ya chuo cha kilimo Kizimbani katika shamra shamra za miaka 49 ya Mapinduzi Zanzibar.
Alisema mahitaji ya wataalamu ni  makubwa hivyo aliwataka wanafunzi hao kusoma kwa bidii ili taifa liwe na idadi kubwa ya wataalamu watakaokidhi haja ya mahitaji sambamba na kupunguza kwa asilimia 50 za uagizaji wa chakula kutoka nje.
Balozi Seif alisema ndani ya nchi kuna shehia 287 ambazo zinahitaji huduma za ugani ambapo maafisa wa ugani waliopo ni 141 ambapo kuna upungufu wa maafisa 146.
Hata hivyo, alisema hao waliopo hawana elimu ya kutosha ambapo wengi wameishia elimu ya stashahada, hivyo alisema dakhalia hiyo itakuwa chachu ya kuzalisha wataalamu wengi zaidi.

Aidha alisema dakhalia zina umuhimu mkubwa kwa maendeleo ya elimu ya kilimo nchini kwani itasaidia kukijengea uwezo chuo hicho kufikia malengo.
Alisema mashirikiano ya utendaji ndio nyenzo kubwa ya mafanikio ya maendeleo sambamba na kutekeleza majukumu ipasavyo bila ya kukiuka utaratibu wa utoaji elimu.
Pia aliwataka walimu waandae mikakati bora ambayo itawezesha kuwabana wanafunzi hao kushiriki masomo yao kikamilifu ili waweze kufaulu vizuri katika kiwango cha stashahada.
Alisema vijana na wanafunzi wana fursa kubwa ya  kupata elimu ya juu nchini  kutokana na kuongezeka kwa vyuo vikuu ili kupunguza gharama zisizo za lazima.
Alisema utafiti umebainisha kwamba mwanafunzi anayepata shahada ya kwanza  kwanza nchini Uingereza analazimika kulipiwa zaidi ya shilingi milioni 57,000,000 fedha ambazo zinaweza kugharamia wanafunzi kadhaa nchini wakati kiwango na ubora wa elimu kinafanana.
 “Tumefikia wakati Zanzibar hakuna  sababu kwa elimu ya ngazi ya shahada na stashahada  kufuatwa tena nchi za nje hasa tabia iliyojengeka kwa vijana kwenda Ulaya kwani tayari tumeshakuwa na vyuo vikuu vinavyotosheleza mahitaji,” alisema.
Aliutaka uongozi wa chuo cha kilimo Kizimbani kuongeza juhudi za kutoa taaluma ili taifa likidhi mahitaji ya wataalamu wa kilimo ambao hivi sasa wapo 141 wakati mahitaji ni wataalamu 287 kukiwa na upungufu wa wataalamu 146.
Balozi Seif alifahamisha kwamba ujenzi wa dakhalia uliofanywa na chuo ni mabadiliko makubwa yatakayoiwezesha Zanzibar kuwa na wataalamu wake na kuacha mfumo wa kutegemea watalaamu wa kigeni ambao wanaibebesha mzigo serikali.

Naye Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo na Maliasili, Afan Othman Maalim alisema katika kukijengea uwezo zaidi wa kitaaluma chuo, Wizara tayari inawaandaa walimu 10 kupata mafunzo ya juu kwa ajili ya kukiwezesha chuo hicho kutoa elimu ya shahada ya kwanza.
Alisema hatua hiyo imelenga kuondosha tatizo la uhaba wa mabwana na mabibi shamba uliopo ambao unachangia kudumaza juhudi za wakulima katika uzalishaji wa kilimo.
Akitoa taarifa ya ujenzi wa dakhalia hiyo pamoja na mikakati ya baadaye ya chuo, Mkurugenzi wa chuo,Mohammed Khamis Rashid alisema ujenzi wa dakhalia hiyo yenye vyumba saba na kuhudumia wanafunzi 42 umekuja kutokana na changamoto iliyojitokeza ya ongezeko kubwa la vijana wanaotaka kujiunga na chuo hicho.
Alisema mbali ya wanafunzi wa chuo hicho lakini pia dakhalia hiyo itatumiwa na  wakulima wa mafunzo na muda mfupi kipindi ambacho wanafunzi wa chuo hicho watakuwa likizo.
Dakhalia hiyo imegharimu jumla ya shilingi 399,000,000 na kugharamiwa na Mfuko wa Kimataifa wa Kuendeleza Kilimo (IFAD).
Aliwataka kulienzi jengo jipya la Dakhalia hiyo ili liweze kuendelea kutumika muda mrefu likiwa katika mazingira mazuri na wanafunzi wengine waje kutumia bila ya kikwazo chochote.

Naye Mkurugenzi wa Chuo cha Kilimo Kizimbani Mohammed Khamis Rashid alisema chuo hicho kimepata usajili katika baraza linalisimamia Mafunzo ya Ufundi Tanzania (NACTE) usajili huo ambao utakiwezesha chuo hicho kuwa miongoni mwa vyuo vinavyotambulika rasmi katika utoaji wa mafunzo ya Kilimo, Mifugo na Maliasili ambapo sasa kimeanza kutoa ngazi ya Diploma.
Alisema jumla ya shilingi milioni 399,000,000 zimetumika katika ujenzi wa Dakhalia hiyo ambayo ina uwezo wa kuchukuwa wanafunzi 42,na wanafunzi wa kike  ngazi ya Diploma ndio watakaoishi katika dakhalia hiyo, ambaoyo pia itatumika kwa ajili ya wakulima ambao watapatiwa mafunzo ya muda mfupi katika chuo hicho.
Mwalimu Mkuu wa Chuo hicho Nassor Salim Mohammed alisema miongoni mwa mafunzo ya wanayotoa chuoni hapo ntiba ya wanyama,uchunguzi wa maradhi,Udhalishaji bora wa mazao,matunzo na kinga,utumiaji wa dawa kwa kiwango kinachokubalika na sahihi.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo alikiri kuwepo kwa upungufu wa Mabibi shamba na mabwana katika sekta ya kilimo hivyo Wizara imeanza kutafuta mbinu mbadala mbali mbali ikiwemo kusomesha wanafunzi hao hivyo mara tu ya kuhitimu watawaajiri ili waweze kutekeleza jukumu hilo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.