Habari za Punde

Dk.Shein: Serikali kuimarisha bajeti ya afya

Aahidi wagonjwa hospitali kupatiwa chakula bora

Na Mwantanga Ame

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, amesema serikali inataimarisha bajeti ya matumizi ya dawa, ili kutoa matibabu bora katika hospitali za umma.

Pia alisema huduma nyengine ambazo serikali itaziimarisha ni ya chakula kwa wagonjwa na vifaa vya matibabu kutokana  na hivi sasa kutumia fedha nyingi kutafuta matibabu nje.

Dk .Shein aliyasema hayo jana wakati akifungua mradi wa  bohari kuu ya dawa Zanzibar, Maruhubi mkoa wa mjini Unguja.

 Alisema hivi sasa kumekuwa na tatizo kubwa la kuwepo bajeti ndogo katika sekta ya afya hasa inayohusu chakula kwa wagonjwa, dawa na vifaa vya matibabu, lakini tayari inajiandaa kukabiliana na hali hiyo ili  hospitali za serikali zitoe matibabu bora.

“Tutagharamia chakula cha wagonjwa, hivi sasa hali hairidhishi wagonjwa wanapewa wali, nyama moja iko huko, maji ya mchuzi unakolezwa bizari nyingi hatuwezi kwenda hivi kwani kuna wagonjwa wanahitaji mlo maalum kulingana na ugonjwa wake sio tumpe muhogo na makopa,” alisema Dk.Shein.


Alisema serikali inalazimika kuchukua hatua hiyo kutokana na umuhimu wa kutoa matibabu bora, ikiwa ni kuendelza dhana ya Mapinduzi matukufu ya Zanzibar ambapo Rais wa kwanza wa Zanzibar Mzee Abeid Amani Karume, aliwaahidi Wazanzibari kuwapa matibabu bure.

Alisema malengo  ya Mapinduzi bado yataendelezwa, licha ya kukumbwa na changamoto za kiuchumi, jambo ambalo limeifanya serikali kuwataka wananchi kuchangia kiasi kidogo cha fedha.

Hali hiyo, alisema imechangiwa zaidi na ongezeko la idadi ya watu baada ya Mapinduzi ya Zanzibar huku zao la karafuu likiwa limeanguka bei jambo ambalo limesababisha mapato ya nchi kushuka.

Alisema serikali imejikuta ikilazimika ndani ya bajeti yake kutegemea zaidi wafadhili ikiwemo serikali ya China, Marekani na Denmark, ikiwa ni hatua ya kuweza kuimarisha sekta hiyo ya kutoa huduma kwa jamii.

Alisema hivi sasa bajeti inayotengwa kwa ajili ya manunuzi imeanza kuongezwa kutoka shilingi milioni 17.5 ya mwaka 2009 hadi kufikia zaidi ya shilingi bilioni 1.


Hata hivyo, alisema serikali inakabiliwa na tatizo kubwa la kutofahamika mahitaji kamili ya dawa katika hospitali za Zanzibar kunakosababisha kuifanya serikali kutoelewa hali halisi ya mahitaji kwa watu wake.


Alisema katika kukabiliana na hali hiyo serikali tayari imeanza kujipanga kwa kuandaa mazingira bora ya watumishi katika sekta ya afya.

Kutokana na hali hiyo Dk. Shein, aliwataka watendaji katika sekta ya afya kubadilika kwa kutekeleza majukumu yao vizuri badala ya kuendelea kufanya kazi kwa mazoea.

Dk. Shein, alizishukuru serikali za Marekani, Jamhuri ya Watu wa China na Denmark kwa michango inayoitoa kuimarisha sekta ya afya nchini.

Mapema Naibu Waziri wa Wizara ya Afya, Dk. Sira Ubwa Mamboya, alisema kujengwa kwa bohari hiyo itaweza kusaidia kwa kiasi kikubwa uhifadhi wa dawa nyingi.


Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dk. Mohammed Saleh Jidawi, alisema jengo hilo limegharimu dola za Marekani milioni  1.2  ambazo zilitolewa na serikali ya Marekani kwa kushirikiana na DANIDA huku serikali ya Zanzibar ikitoa zaidi ya shilingi milioni 278.

Balozi wa Marekani nchini Tanzania , Alfonso Lenhardt, akitoa maelezo yake alisema serikali yao itaendelea kuisaidia Zanzibar katika kuinua sekta ya afya hasa eneo linalohusu huduma za kijamii kwa wanawake na watoto.

Nae Mwakilishi wa Serikali ya Denmark , Stean Underson, akitoa maelezo yake alisema nchi yao itaendelea kushirikiana na Zanzibar , kwa vile imekuwa ikiipa nafasi kubwa katika bajeti yao.


Nae Mkurugenzi wa bohari hiyo, Mayasa Salum, alisema mfumo wa usalama katika bohari hiyo utaweza kuimarisha utoaji huduma bora za matumizi ya dawa katika hospitali kuu ya Mnazimmoja na vituo vyengine vya afya kwa Unguja na Pemba.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.