Habari za Punde

Rais Mstaafu Aboud Jumbe atimiza miaka 93



Na Raya Hamad
Imeelezwa kuwa moja kati ya neema alizopewa mwanaadamu ni umri mrefu hivyo ni wajibu wa kila mmoja wetu kuutumia vyema uhai wake kwa kutenda mema na kushukuru kila siku kwani hapaswi mwanaadamu kuwa aasi bali anachotakiwa ni kumuabudu Mola wake aliyemuumba  .
Kadhi mkuu wa Zanzibar Sheikh Khamis Haji Khamis ameyasema hayo katika dua ya kumshukuru Mwenyezi Mungu  kutimiza miaka 93 ya kuzaliwa kwa Rais Mstaafu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Alhajj Aboud Jumbe Mwinyi iliyofanyika  Kiembe Samaki .
Sheikh Khamis Haji ametowa ukumbusho kwa kusema kuwa “ Ifanye dunia kama kwamba utaishi milele kwa maana ya kutenda mazuri na kumuabudu Allah kama  tulivyoamrishwa katika dini pia ifanye akhera yako kama utakufa sasa kwa maana ya kujiandaa kwa kutenda amali njema na kuomba msamaha kila siku .
Katika khutba yake iliyosomwa na Ustadh Moh’d Yoyota kwa niaba yake Rais Mstaafu Awamu ya Pili Alhajj Aboud Jumbe  amesema kuwa anamshukuru Mola wake kwa  umri aliyomjaalia  kwani  ameshuhudia neema nyingi ambazo hazina kiima kisicho kifani,kina wala mizani katika  maisha yake na kupitia nyanja tofauti za maisha hadi M/Mungu atakapomjaalia mwisho wa maisha yake.

Alhajj Aboud Jumbe ameongeza kusema kuwa  anamshukuru Mola wake kwa kumpa rehema zake huruma na hisani pale alipokabidhiwa dhamana ya kuongoza baadae  kumnusuru na kumfariji na hatimae kumuongoza pale alipoteleza mnamo asiyoyaridhia  kwani  majibu sahihi ya mithani yetu wanaadamu yanasubiri siku ya malipo ambayo yatupasa tutambue kuwa kila mmoja wetu atakutana nayo.
“Namuomba Mwenyezi Mungu kwa unyenyekevu azidi kuitakasa amali yangu na kunipa khusni l khatima mimi pamoja na waislamu wenzangu  
Akitowa shukurani kwa waalikwa waliohudhuria katika dua hiyo kwa niaba ya familia  ndugu Mustafa  Aboud Jumbe ambae ni mtoto wake amesema kuwa lengo la kusoma dua hii ni kukumbushana namna gani tunatumia neema na kila mmoja vipi atautumia uhai wake na kusisitiza kuwa dua hio ni mwenyewe baba yao aliyetowa utaratibu juu ya namna gani isomwe dua hio “Tumekuwa tukipata masuala mengi kuhusu hali ya  mzee wetu  jibu ni kwamba hajambo ila uzee tu ndio unaomsumbua, nuru ya macho imepotea ,kusikia kumekuwa shida kidogo lakini anasikia na anazungumza na hii shughuli yake ya leo amepanga  mwenyewe”alisisitiza Mustafa Jumbe.
Nae Sheikh Moh’d Iddi ametowa wito kwa jamii  kufanya matendo mema kwani kuwepo kwetu ipo historia ambayo M/ Mungu amewashushia waja wake na aliyebahatika kuishi kwa kumuabudu huyo atakuwa amefaulu.
Miongoni mwa waliohudhuria  katika dua hio ni pamoja na Kadhi Mkuu Mstaafu Sheikh Habib Ali Kombo baadhi ya Masheikh, Familia yake, baadhi ya wanafunzi aliwahi kuwasomesha na kuwafundisha kazi .

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.