RISALA
YA MWEZI MTUKUFU WA RAMADHANI YA RAIS WA ZANZIBAR NA MWENYEKITI WA BARAZA LA
MAPINDUZI, MHE. ALHAJ DK. ALI MOHAMED SHEIN,
JULAI, 2013, RAMADHAN 1434 A.H.
BISMILLAHI
RAHMAN RAHIM.
Namshukuru Mwenyezi Mungu Karim,
Mwenye wingi wa Rehema, aliye muweza wa kila kitu. Yeye ndiye mwenye kustahiki shukurani za waja
wake na viumbe vyote.
Ndugu
Wananchi,
RAMADHANI
KARIM,
Assalam
Alaykum wa Rahmatullahi Wabarakatuhu,
Tumefikiwa na mwezi Mtukufu wa
Ramadhani. Hatuna budi waumini sote kwa
pamoja tumshukuru Mola wetu kwa kutupa uhai na tukaweza kuukaribisha mwezi
huu. Namuomba Muumba wetu atuzidishie umri na afya ili
tuweze kuukaribisha mwezi huu katika ibada kwa salama na amani. Na atufikishe kwa kheri na salama miezi
mengine ijayo mwaka baada ya mwaka.
Ndugu
Wananchi,
Kufikiwa na mwezi Mtukufu wa
Ramadhani ni neema kubwa kwetu. Huu ndio
mwezi ambamo waumini tumepewa ibada ya kufunga, Saumu, tukateremshiwa kitabu kitukufu
cha uongofu, Qurani katika usiku wenye heshima kubwa, Lailatul Qadri.
Haya yameelezwa na mwenyewe Subhana
Wataala katika Qurani Surat Al-Baqara aya ya 183 mpaka 187 yenye maelezo ya
kina juu ya ibada hii ya kufunga. Maimamu na Masheikh wanazieleza aya hizi
katika khutba za Ijumaa na kwengineko.
Ndugu
Wananchi,
Inafaa tukumbushane na kupeana
mafunzo kwamba Mwenyezi Mungu Mtukufu amefaradhisha ibada ya Saumu iwe ni njia
kubwa kwetu ambayo tukifuata tutapata kuongoka na kuzipata rehema za Mola wetu
(SW).
Ibada hiyo inatupa mazoezi ya
kufanya vitendo kwa nia na moyo safi, yaani IKHLAS na ustadi. Vile vile, inastawisha sifa ya mtu kuwa na nidhamu
ya nafsi inayopelekea atekeleze vilivyo wajibu wake na kumzuia kufanya maasi na
yote aliyokataza Mola wetu. Tunafunga
bila ya ria na Mola wetu ndiye anaeziona Saumu zetu.
Bwana Mtume amepokea kutoka kwa Mola
wake, hadithi Qudsi, inayosema:-
“Ikhlas ni siri nimeitia moyoni mwa mja wangu,
hapana malaika atakayejua ila aiandike, au shetani ili aiharibu”
Ni kwa sababu hiyo ndio Mtume
Muhammad (SAW) akatuambia kwamba Mola anasema:-
“Saumu ni kwa ajili yangu na mimi
ndiye ninaelipa”
Hiyo ni neema na kheri kubwa.
Ndugu
Wananchi,
Hii Ikhlas ndiyo inayotufunza
kufanya mema na kuyabeza maovu, tukitambua kuwa Mwenyezi Mungu anatuona kwa
kila tunalofanya au kudhamiria kulifanya, ikiwa la kheri au la shari.
Kwa kauli ya Mtume Muhammad (SAW)
“ Wema ni kumuabudu Mwenyezi Mungu kama
kwamba unamuona; kwa sababu kama wewe humuoni yeye anakuona”
Vile vile, katika sifa mojawapo za
Mwenyezi Mungu ni kuwa:-
“Hakika Mwenyezi Mungu kwa kila jambo
ni shahidi”
Katika Quran, Surat Al-Nakhl, Aya ya
19, Mwenyezi Mungu amesema:
“Na Mwenyezi Mungu anayajua
mnayoyaficha na mnayoyatanguliza”
Pia katika Surat Isra, Aya ya 25
Mola anatuambia:
“Mola wenu anajua kabisa yaliyo nyoyoni
mwenu. Ikiwa mtakuwa wema, basi hakika
Yeye ni Mwenye kuwaghufiria wanaotubu kwake”.
Ndugu
Wananchi,Katika kutafakari hayo, tujue kwamba Ramadhani imetufikia ili tutafute na kupata sifa za usafi wa nia na utu wema. Tumo katika kipindi chenye harakati za kidunia na wakati mwengine tunasahau mwisho wetu. Ni kweli kwamba Bwana Mtume Muhammad (SAW) ametuambia:-
“Fanya
mambo ya kheri kwa dunia yako kama kwamba utaishi milele”
Lakini pia ameongeza kwa kusema :-
“Na fanya kheri kwa Akhera yako kama
kwamba utakufa kesho”
Hasa katika mwezi huu Mtukufu wa
Ramadhani inatupasa tuzifuate sifa zote tulizofunzwa
na Mwenyezi Mungu na Mtume wake, tuondoe sababu zote za utengano na mfarakano na
tuimarishe njia zote za umoja, ushirikiano, ihsani na kupendana.
Tukifanya hivyo tutakuwa
tumewajibika kwa Mola wetu pamoja na kupata malipo yake ya kheri ya Ramadhani
na amani itaenea, usalama utazagaa, maisha yatastawi na wananchi tutazidi kuneemeka.
Ndugu
Wananchi,
Mashekh wetu wanatufunza kuwa
Mwenyezi Mungu ameichagua na kuitukuza Ramadhani iwe ni wakati wa kujizoesha
kufanya mema ili baadae iwe ndio tabia yetu ya kawaida. Katika mwezi huu tunahimizwa kuongeza ibada
ya Sala kwa kusali Tarawekh na Sala nyengine za Sunna hasa nyakati za usiku. Tumehimizwa kusameheana, kutoa sadaka zaidi na
kuwa wapole na kujikinga na maovu yote ambayo yanavunja Saumu, Bwana Mtume
(SAW) ametuelekeza:-
“Mche Mungu na uongoke kwa vitendo
vyema”.
Tuhimizane kufanya mema na tumche
zaidi Mola wetu.Ndugu Wananchi,
Napenda kugusia machache ambayo yamehusiana na Rehema, hasa katika mwezi huu Mtukufu wa Ramadhani. Nakumbusha kwamba wakati tunatafuta riziki katika mwezi huu tuzingatie haki na kurehemiana sana katika biashara, hasa muuzaji na mnunuzi.
Tunatambua kwamba faida kwa
mfanyabiashara ni lazima, ili aweze kujimudu na kuendelea. Lakini wakati huo huo Mwenyezi Mungu anatwambia
katika Qurani Tukufu Suratu An Nisaa Aya ya 29.
“Enyi mlioamini msiliane mali zenu kwa batili
(dhuluma) isipokuwa iwe biashara kwa kuridhiana baina yenu”
Aya hii inatudhihirishia tufanye
biashara ya haki, bei ziwe za haki na bidhaa ni nzuri sio za kuhadaiana. Kwa upande wa Serikali hatutavumilia kuona
watu wanahatarisha maisha na afya ya wengine kwa kuwauzia bidhaa zilizopitwa na
wakati, mbovu na zisizokuwa na vipimo bora.
Kwa upande wa mazao ya kilimo, kama ndizi zinazouzwa zikiwa changa. Naagiza vyombo husika kuchukua hatua
madhubuti kuhusu hayo niliyoyataja juu ya biashara. Inafaa tumshukuru Mwenyezi Mungu kwa
kutujaalia baraka ya mazao ya aina nyingi ya kilimo wakati huu na vile vile, nawashukuru
wafanyabiashara wetu kwa kujaza madukani mwao bidhaa mbali mbali zinazohitajika
zaidi katika mwezi huo, zikiwemo vyakula na nguo.
Ndugu
Wananchi,
Natoa wito kwetu sote tuwe wenye
kurehemeana kwa njia mbali mbali, hasa katika kutoa Sadaka. Bwana Mtume Muhammad (SAW) amesema:-
“Mwenyezi Mungu humsaidia mja anayemsaidia
nduguye”
na pia akaongeza kwa kusema:-
“Mrehemu (Mfanyie ihsani) aliopo katika ardhi
(duniani) na atakurehemu aliopo mbinguni”
Nawashukuru wakulima wetu Unguja na
Pemba, kwa jitihada za kuzalisha mazao zaidi ya chakula.
Basi tuwakumbuke kwa rehema wenzetu
wasiojiweza, mayatima, masikini, wanafunzi waliopo dakhalia mbali mbali, wagonjwa
waliopo hospitalini na watu wengine wanaohitaji kusaidiwa angalau kwa futari.
Ndugu
Wananchi,
Mwezi huu Mtukufu wa Ramadhani
umekuja wakati wa msimu wa utalii nchini kwetu.
Tutakuwa na wageni wengi na wengine wasiokuwa Waislamu. Wao ni wasafiri na dini yetu inatufundisha
kwamba Waislamu wawe na moyo mzuri kwa wasafiri. Ni vyema kuwa na subira kuwaongoza juu ya taratibu,
mila na kanuni zetu katika mwezi huu bila ya bughudha au uvunjaji wa sheria.
Wafanyabiashara wa vyakula, hotelini
na mikahawani wanapaswa kuheshimu khulka, mila na utamaduni wetu. Tusifanye mambo ya karaha na kuwakasirisha wanaofunga.
Wasiofunga wawaheshimu wanaofunga.
Tufanye Ramadhani yetu iwe ni kivutio cha wageni, kwa utamaduni na
ustarabu wetu.
Ndugu
Wananchi,
Kwa kumalizia natoa wito kwa wananchi
wote kuwa waangalifu na kutumia vyakula na maji bila ya israfu. Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA) itafanya kila
juhudi ili kuhakikisha kuwa maji yanapatikana katika maeneo mbali mbali nchini
mwetu. Tuitumie vyema neema anayotupa Mola wetu huku tukijua kuwa hapendi
uharibifu.
Namuomba Mwenyezi Mungu atujaalie
Ramadhani ya mafanikio kwetu sote, kuanzia kwa wafanyabiashara, Wakulima,
Wavuvi, Washoni, Waendeshaji darsa za dini, Vijana, Wazee na wananchi wote kwa
ujumla. Ewe Mola wetu tupe uongofu wako,
ijaalie nchi yetu idumu na salama, amani, umoja, mshikamano na upendo kati
yetu.
Ramadhani
Karim,
Assalam
Alaykum wa Rahmatullahi Wabarakatuhu,
Ahsanteni
kwa kunisikiliza.
No comments:
Post a Comment