Habari za Punde

Balozi Seif Awataka Wawekezaji Kuwekeza Zanzibar

 Na Othman Ame USA.
Imeelezwa kwamba ipo haja kwa Taasisi, Makampuni na hata Watu binafsi kuanza kufikiria kujenga nyumba kwa kuziuza kwa bei nafuu au kutoa mkopo ili kuzisaidia jamii kuondokana na matatizo ya makazi.

Ushauri huo umetolewa na Ofisa Mkuu wa Taasisi ya Mtandao wa ushirikiano ya Latin America { Shumake Global Partiners } Bwana Robert Shumake wakati akizungumza na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif ambae yuko ziarani Nchini Marekani hapo katika Hoteli ya Kimataifa ya Marriott Mjini Seattle – Washington.

Bwana Robert Shumake ambaye aliwahi kuwa Bingwa wa mbio za Magari Duniani tayari ameshakubali kuingia ubia na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar { ZSSF } katika mpango wake wa ujenzi wa nyumba za Mkopo nafuu katika eneo la Mbweni nje kidogo ya Mji wa Zanzibar.

Mwanambio za Magari huyo wa Kimataifa alimueleza Balozi Seif kwamba bado ipo idadi kubwa ya Jamii katika Mataifa mbali mbali ulimwenguni imekosa makazi ya kudumu hali ambayo inawapa wakati mgumu katika maisha yao ya kila siku.


Alieleza kwamba baadhi ya watu waliokosa makazi wamekuwa wakikumbwa na madhara mbali mbali na wakati mwengine hufikia kufariki dunia kutokana na kukumbwa na baridi kali.

Bwana Robert Shamake alifahamisha kwamba Taasisi yake imelenga kusaidia huduma za jamii kama Nyumba, Afya pamoja na Sekta ya Elimu katika Mataifa tofauti ulimwenguni.

Alisema kwa kuwa tayari ameshaanza mazungumzo ya awali na Uongozi wa ngazi ya Juu wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar  Mjini Seattle kuhusiana na mpango huo wa ujenzi wa nyumba nakusudia kuitembelea Zanzibar Mwishoni mwa mwezi wa Disemba mwaka huu ili kujionea hali halisi ya mazingira  ya Zanzibar.

Kwa upande wake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi aliupongeza Uongozi wa Taasisi hiyo ya Mtandao wa ushirikiano ya Latin America kwa uamuzi wake iliyochukuwa ambao utasaidia kustawisha jamii ndani ya Visiwa vya Zanzibar.

Balozi Seif alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar mara baada ya Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka 1964 ilianzisha mradi wa ujenzi wa nyumba za maendeleo katika maeneo mbali mbali ya Visiwa vya Unguja na Pemba ili kuwapatia wananchi wake makazi bora.

Alisema mpango huo muhimu wa serikali hivi sasa unastahiki  kuungwa mkono na taasisi tofauti kwa vile nguvu za kuendeleza mpango huo ambao unahitajika zaidi na jamii zimepunguwa kutokana na ongezeko kubwa la idadi ya watu Zanzibar.


XXXXXXXXXXXXXXXXXXXX

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.