Habari za Punde

Zacadia Fundraising Event

Toronto, Canada
November 03, 2013,
Jumuiya ya Diaspora ya Canada, Zanzibar-Canadian Diaspora Association-ZACADIA, ambayo inajulikana rasmi kwa jina la ZACADIA Foundation, juzi November 02, 2013, iliandaa hafla ndogo ya kutunisha mfuko wa kuwasaidia watoto mayatima ambao wamo katika mpango wa mradi maalum wa kuwadhamini watoto hao unaojulikana kwa jina la Zanzibar Children Funds Program.
Hafla hiyo ambayo  ilifanyika katika ukumbi wa kijamii wa “Lawrence Heights Community Centre” ilianza kwa kusomwa risala ambayo imeelezea historia ya ZACADIA na kazi ilizozifanya na mafanikio yaliyofikiwa.
Baada ya risala hiyo, Imam Abdufataah alisimama na kusoma dua ya ufunguzi na baadaye kusimama Maalim Ali kwa kutoa hotuba ya kuhamasisha waliohudhuria na wale wasiokuwapo katika kusaidia mayatima.
Katika hotuba yake, alisema kwamba zamani ilikuwa hakuna suala la watoto mayatima  kuchangiwa kwa sababu kila mmoja miongoni mwa jamii alikuwa akifanya wajibu wake licha ya kuwa hali zao za kiuchumi zilikuwa ni duni kulinganisha na sasa hivi, ambapo watu wengi wana uwezo, lakini wanashindwa kujua nani ameamka salama na ameshinda vipi, amekula nini na anavaa vipi.
“Siyo kwamba zamani kulikuwa hakuna mayatima visiwani kwetu, lakini ilikuwa hukuti kuwaona watu wanawachangia mayatima hao misikitini au katika mihadhara kama hii, kwa sababu kila mmoja alikuwa anamjali mwenzake.

Kabla mtu hajatoka kwenda na shughuli zake, alikuwa akihakikisha kuwa jirani yake ameamka salama na kama kuna mtu ana yatima au mayatima, basi alikuwa akihakikisha familia hiyo hailali na njaa waka kutembea na matambara mwilini. Laiti kila mmoja wetu angalifanya wajibu wake kama tunavyoelezwa na dini yetu, basi mihadhara kama hii ya kuwaombea mayatima isingalikuwapo,” alimalizia maalim Ali.
Katika hafla hiyo, pia ilioneshwa PowerPoint ya mradi wa watoto mayatima ambao umeanza kufanyiwa kazi. Pia ilioneshwa PowerPoint ya mradi wa Wazee na Wanawake ambapo msimamizi wa Idara hiyo aliwasili Zanzibar hivi karibuni na kutoa misaada ya vitu mbali mbali kwa wananchi wanaohitaji Unguja na Pemba.
Hafla kama hii inategemewa kufanyika tena katika mwezi wa December mwaka huu katika ukumbi wa Driftwood Community Center ambapo ni kitovu cha eneo wanaloishi Wazanzibari wengi katika GTA.
Jumla ya dola 125 za Canada zilikusanywa katika hafla hiyo. Baadhi ya waliohudhuria walichukuwa fomu za kuahidi kuchangia kidogo kidogo kwa mwaka. Pia kulifanyika mnada mdogo wa picha za Msahafu na msahafu mmoja wa herufi kubwa ambao vitu hivyo vyote vilitolewa sadaka na wana Diaspora waliohudhuria.
Pia mtoto mmoja miongoni mwa watoto mayatima waliomo katika mradi huo alipata mdhamini wa kumshughulikia kama mwanawe kwa huduma za elimu, afya, nguo, chakula na huduma nyengine hadi atakapomaliza sekondari na baadaye ZACADIA kujaribu kumtafutia scholarship kwa ajili ya masomo ya juu.
Mtoto huyo ambaye anatokea sehemu za Kiungoni huko Kaskazini, Pemba ni Fatma  M. Saleh

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.