Habari za Punde

FUPECO walia na uharibifu mazingira

Na Kauthar Abdalla
JUMUIYA ya  Kuhifadhi Mazingira Ras Fumba (FUPECO),imeeleza kusikitishwa na tatizo la uharibifu wa mazingira unaofanywa katika eneo hilo.

Akizungumza na gazeti hili, Mwenyekiti wa  Jumuiya hiyo, Maria Shoka Hassan ,alisema tatizo la uharibifu wa misitu katika maeneo ya ghuba ya Minai limekuwa kubwa na kupoteza rasilimali ya msitu.

Alisema katika visiwa vya Kwale,Nyemembe na maeneo ya karibu hali imekuwa mbaya kutokana na kuvamiwa na kukatwa miti ya asili.

Alisema waharibifu wakubwa ni watu wa vijiji vinavyozunguka ghuba hiyo pamoja na watu kutoka maeneo mengine.

Alisema licha ya jitihada za kuwaelimisha wananchi juu ya umuhimu wa kuwepo misitu na uhifadhi wake , bado kuna ongezeko la  uharibifu wa misitu ya asili.


Aliiomba serikali kupitia Idara ya misitu na mali asili zisizorejesheka kuandaa mikakati imara ya kuwadhibiti wahalifu ili kunusuru mali asili.


Kwa upande wake, Msaidizi Ofisa Misitu Idara ya Misitu na Maliasili Zisizorejesheka, Yussuf Haji Kombo, alisema kutokana na sheria eneo la msitu lolote linashughulikiwa na kijiji husika na inaposhindikana Idara inaweza kuchukua hatua.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.